Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ufufuo wa Yesu Humaanisha Uzima!

Ufufuo wa Yesu Humaanisha Uzima!

UFUFUO wa Yesu sio tukio la zamani tu, lisilo na umuhimu wowote kwetu leo. Mtume Paulo alionyesha umuhimu wake alipoandika hivi: “Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu, matunda ya kwanza ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo. Kwa kuwa kifo ni kupitia mwanadamu, ufufuo wa wafu pia ni kupitia mwanadamu. Kwa maana kama vile katika Adamu wote wanakufa, vivyo hivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.”—1 Wakorintho 15:20-22.

Yesu alifufuliwa Nisani 16, 33 W.K., tarehe ambayo Wayahudi walimtolea Yehova Mungu matunda ya kwanza ya mazao yao katika patakatifu pa hekalu huko Yerusalemu. Kwa kumwita Yesu matunda ya kwanza, Paulo alimaanisha kwamba kungekuwa na watu wengine ambao wangefufuliwa.

Maneno yanayofuata ya Paulo yanaeleza jambo ambalo limewezekana kwa sababu ya ufufuo wa Yesu. Paulo alisema: “Kwa kuwa kifo ni kupitia mwanadamu ufufuo wa wafu pia ni kupitia mwanadamu.” Sote tunakufa kwa sababu tulirithi dhambi na kutokamilika kutoka kwa Adamu. Hata hivyo, kwa kutoa mwili wake mkamilifu wa kibinadamu kuwa dhabihu, Yesu alifanya iwezekane kwa wanadamu kukombolewa kutoka kwenye utumwa wa dhambi na kifo kupitia ufufuo. Akihitimisha hoja yake vizuri, Paulo aliandika hivi kwenye Waroma 6:23: “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.”

Yesu mwenyewe alifafanua umuhimu wa kifo na ufufuo wake kwetu. Akizungumza kujihusu alisema: “Mwana wa binadamu atainuliwa, ili kila mtu anayemwamini apate kuwa na uzima wa milele. Kwa maana Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:14-16.

Wazia—uzima wa milele bila maumivu, kuteseka, wala huzuni! (Ufunuo 21:3, 4) Tazamio zuri kama nini! Msomi mmoja anasema hivi: “Ingawa makaburi yanatukumbusha kuhusu ufupi wa maisha, ufufuo unatuhakikishia ufupi wa kifo.” Naam, ufufuo wa Yesu unamaanisha uzima!