Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIMULIZI LA MAISHA

Uamuzi wa Kutumia Maisha Yangu Katika Utumishi wa Yehova

Uamuzi wa Kutumia Maisha Yangu Katika Utumishi wa Yehova

Baada ya kumaliza shule ya sekondari mnamo Januari 1937, nilijiunga na Chuo Kikuu cha Iowa kilicho karibu na mahali tulipoishi magharibi mwa Marekani. Nilitumia muda mwingi kusoma na kufanya kazi ili niweze kujilipia masomo. Tangu nikiwa kijana nilipendezwa sana na majengo marefu na madaraja yanayoning’inia.

Mwanzoni mwa mwaka wa 1942, Marekani ilipoingia katika Vita vya Pili vya Ulimwengu, nilikuwa katika mwaka wangu wa tano chuoni na miezi michache ilibaki kabla sijapokea shahada ya uhandisi wa majengo. Nilikuwa nikiishi na vijana wawili. Mmoja wao alipendekeza nizungumze na mtu aliyekuwa “akiwatembelea vijana wa ghorofa ya chini.” Huko nilikutana na Shahidi wa Yehova anayeitwa John O. (Johnny) Brehmer. Nilishangazwa na jinsi alivyopata jibu la Biblia kwa swali lolote. Nilivutiwa sana na jambo hilo, hivyo nikaanza kujifunza Biblia na Johnny kwa ukawaida na kila nilipopata nafasi nilienda kuhubiri pamoja naye.

Baba yake Johnny anayeitwa Otto, alijiunga na Mashahidi alipokuwa rais wa benki ya Walnut, Iowa. Otto aliacha kazi yake na kuanza utumishi wa wakati wote. Baada ya muda, mfano wake mzuri na wa familia yake ulinichochea kufanya uamuzi muhimu.

WAKATI WA KUFANYA UAMUZI

Siku moja, mkuu wa chuo alinieleza kwamba nilikuwa nikipata alama za chini na singehitimu kwa kutegemea alama za wakati uliopita. Nakumbuka nikisali kwa Yehova Mungu kwa bidii ili anipe mwongozo. Muda mfupi baadaye, profesa wangu wa uhandisi aliniita kwenye mkutano. Aliniambia alipokea taarifa kwamba kulikuwa na nafasi ya kazi ya uhandisi na bila kunieleza alijibu kupitia telegramu kuwa ningekubali nafasi hiyo. Nilimshukuru lakini nikamweleza nilikuwa nimeamua kutumia maisha yangu katika utumishi wa Yehova. Nilibatizwa Juni 17, 1942, na mara moja niliwekwa kuwa painia, yaani, mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova.

Baadaye mwaka wa 1942, niliambiwa nijiunge na jeshi hivyo nilienda kwenye baraza la kuwaandikisha watu katika jeshi ili kueleza msimamo wangu wa kutoshiriki vita kwa sababu ya dhamiri. Niliwaonyesha hati ambazo maprofesa wangu wa chuo walikuwa wameandika kuhusu tabia yangu nzuri na ustadi wangu wa pekee nikiwa mhandisi wa majengo. Ijapokuwa ushuhuda wote huo mzuri, hatimaye nilitozwa faini ya dola 10,000 za Marekani pamoja na kifungo cha miaka mitano katika gereza la Leavenworth, Kansas, huko Marekani.

NIKIWA GEREZANI

Gereza la Leavenworth, Marekani leo. Nilikuwa miongoni mwa Mashahidi 230 waliofungwa humo

Zaidi ya Mashahidi vijana 230 walikuwa wamefungwa katika shamba la gereza la Leavenworth.  Katika shamba hilo tulifanya kazi chini ya usimamizi wa walinzi. Baadhi yao walijua msimamo wetu wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote na walituheshimu.

Walinzi wachache walitusaidia kufanya mikutano yetu ya Biblia kwa ukawaida. Pia, walitusaidia kuingiza machapisho ya Biblia gerezani. Hata mlinzi wa gereza alijiandikisha ili atumiwe gazeti la Consolation (sasa ni Amkeni!).

KUACHILIWA, KISHA UTUMISHI WA UMISHONARI

Mnamo Februari 16, 1946, miezi michache baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, niliachiliwa baada ya kufungwa kwa miaka mitatu gerezani. Mara moja, nilianza tena utumishi wa wakati wote nikiwa painia. Nilipewa mgawo wa kuhubiri katika mji wa Leavenworth, Kansas. Niliogopa mno kwa sababu Mashahidi wa Yehova walibaguliwa sana katika eneo hilo. Pia ilikuwa vigumu kupata kazi na mahali pa kuishi.

Nakumbuka nikikutana na mlinzi mmoja aliyepiga kelele hivi kwa hasira: “Toka hapa!” Nilichanganyikiwa nilipoona ametoka na fimbo mkononi, hivyo nikaondoka haraka. Katika nyumba nyingine mwanamke mmoja alisema “Subiri kidogo,” na kisha akafunga mlango. Nilisubiri na kwa ghafula akafungua dirisha la ghorofani na kunimwagia maji machafu. Hata hivyo, nilipata baraka nyingi katika huduma. Baadaye nilijua kwamba baadhi ya watu niliowapa machapisho ya Biblia walikuja kuwa Mashahidi.

Katika mwaka wa 1943 shule mpya ya wamishonari ilianzishwa huko New York. Nilialikwa kuhudhuria, na nilihitimu darasa la kumi la shule hiyo Februari 8, 1948. Baadaye iliitwa Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead). Nilipohitimu nilitumwa nikatumikie nchini Gold Coast, ambayo sasa inajulikana kama Ghana.

Nilipowasili Gold Coast, mgawo wangu ulikuwa kuwahubiria maofisa wa serikali na wazungu. Mwishoni mwa juma nilikuwa nikishirikiana na washiriki wa kutaniko la Mashahidi wa Yehova na kuwasaidia kuhubiri nyumba kwa nyumba. Pia niliwatembelea Mashahidi walioishi maeneo ya mbali na kuwazoeza jinsi ya kuhubiri. Kwa kuongezea, nilitumikia nikiwa mwangalizi anayesafiri kwenye nchi jirani ya Ivory Coast, ambayo sasa inaitwa Côte d’Ivoire.

Nilipokuwa nikitumikia maeneo hayo, nilijifunza kuishi kama wenyeji wa Afrika, yaani, kulala kwenye nyumba ya udongo, kula kwa mikono, na kuchuchumaa “nje” kama Waisraeli walivyofanya huko nyikani. (Kumbukumbu la Torati 23:12-14) Jambo hilo lilifanya mimi na wamishonari wenzangu  tupendwe na watu wa eneo hilo. Wake wa wakuu wa serikali walianza kujifunza Biblia pamoja nasi. Hivyo, wapinzani walipoanza kutusumbua na kupewa ruhusa ya kutunyang’anya vibali vyetu, wanawake hao waliwashinikiza waume zao na uamuzi ukabatilishwa!

Kama ilivyokuwa kwa wamishonari wengi katika Afrika, hatimaye nilipatwa na malaria. Nilipatwa na homa iliyonifanya niweweseke. Nyakati nyingine, hata nilihitaji kushikilia utaya wangu wa chini ili usitikisike. Licha ya hayo, nilipata shangwe na niliridhika katika utumishi wangu.

Miaka minne ya kwanza nikiwa Afrika, mimi na Eva Hallquist tuliandikiana barua, nilikuwa nimekutana naye kabla sijaondoka Marekani. Nilijua kwamba angehitimu darasa la 21 la shule ya Gileadi Julai 19, 1953, kwenye kusanyiko la kimataifa la Mashahidi wa Yehova katika uwanja wa Yankee Stadium huko New York. Nilifanya mpango na nahodha wa meli nifanye kazi kwenye meli yake ili anisafirishe mpaka Marekani.

Baada ya kusafiri kwa siku 22, nyakati nyingine kwenye bahari iliyochafuka, nilifika na kwenda kukutana na Eva kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn. Tukiwa kwenye paa la makao makuu tukiangalia mandhari nzuri ya jiji la New York, nilimwomba tufunge ndoa. Baadaye, Eva aliungana nami katika utumishi huko Gold Coast.

KUSHUGHULIKIA MAJUKUMU YA FAMILIA

Baada ya kutumikia pamoja na Eva kwa miaka kadhaa barani Afrika, mama yangu alinitumia barua akinieleza kuwa Baba anaugua kansa. Baada ya kupata ruhusa ya kutokuwapo kwenye mgawo wetu, tulirudi Marekani. Afya ya baba ilizorota haraka, na akafa baada ya muda mfupi.

Miaka minne baada ya kurudi Ghana, tulipata habari kuwa Mama anaugua. Marafiki fulani walipendekeza mimi na Eva turudi nyumbani kumtunza Mama. Huo ulikuwa uamuzi mgumu sana. Hatimaye tulirudi Marekani baada ya kutumikia miaka 15 nikiwa mmishonari na 11 tukiwa pamoja.

Tukiwa pamoja na chifu nchini Gold Coast, sasa ni Ghana

Kwa miaka mingi, tulisaidiana kumtunza Mama, na hali ilipomruhusu tulimsaidia kufika mikutanoni. Alikufa Januari 17, 1976 akiwa na miaka 86. Miaka tisa baadaye tulipata pigo kubwa zaidi. Iligunduliwa kwamba Eva alikuwa na kansa. Tulijaribu kupambana na ugonjwa huo kwa kila njia lakini alikufa Juni 4, 1985, akiwa na umri wa miaka 70.

MABADILIKO ZAIDI KATIKA UTUMISHI WANGU

Mwaka wa 1988, nilialikwa kwenye programu ya kuweka wakfu ofisi ya tawi iliyopanuliwa ya Ghana. Lilikuwa tukio lisilosahaulika! Miaka 40 mapema, nilipofika Ghana baada ya kuhitimu Shule ya Gileadi, kulikuwa na Mashahidi wachache. Kufikia mwaka wa 1988, kulikuwa na zaidi ya Mashahidi 34,000, na sasa wamefikia karibu 114,000!

Miaka miwili baadaye, mnamo Agosti 6, 1990, nilimwoa Betty Miller, rafiki wa karibu wa Eva. Tumeendelea kumtumikia Yehova pamoja. Tunasubiri kwa hamu wakati ambapo tutamwona Eva, wazazi wetu, na wazazi wa wazazi wetu watakapofufuliwa katika Paradiso duniani.—Matendo 24:15.

Machozi hunitoka ninapofikiria pendeleo kubwa la kumtumikia Yehova kwa zaidi ya miaka 70. Mara kwa mara ninamshukuru kwa kuniongoza katika utumishi wake. Ingawa sasa nina umri wa zaidi ya miaka 90, bado Yehova, ambaye ni mhandisi mkuu zaidi ameendelea kunipa nguvu na ujasiri wa kuendelea kumtumikia.