Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mababu Zangu Wana Tumaini Gani?

Mababu Zangu Wana Tumaini Gani?

GAZETI The Chosun Ilbo la Korea lilikuwa na kichwa kilichowavutia wengi. Kilisema hivi: “‘Shim Cheong Mzuri,’ Ambaye Hakumjua Yesu—Je, Alienda Motoni?”

Kichwa hicho kilizua ubishi kwa sababu Shim Cheong ni msichana anayesimuliwa katika hadithi ya Kikorea ambaye alidhabihu uhai wake ili kumsaidia baba yake aliyekuwa kipofu. Kwa miaka mingi, amesifiwa sana. Nchini Korea, Shim Cheong anaonwa kama kielelezo cha binti mwenye upendo.

Kwa wengi, wazo la kwamba mtu kama huyo angeteswa motoni kwa sababu tu hakuwa Mkristo aliyebatizwa lilionekana lisilo la haki, hata la kuudhi. Zaidi ya hayo, inadhaniwa kwamba hadithi hiyo ilitokea mapema kabla ujumbe kumhusu Kristo haujafika kwenye kijiji chao.

Makala hiyo ilitia ndani mahojiano na kasisi fulani. Aliulizwa ikiwa wale wote waliokufa bila kupata nafasi ya kujifunza kumhusu Yesu walikuwa wamehukumiwa kuteswa motoni. Alijibuje? “Hatujui. Tunadhani tu kwamba lazima Mungu amewafanyia mpango fulani.”

JE, NI LAZIMA MTU ABATIZWE ILI APATE WOKOVU?

Kitabu The New Catholic Encyclopedia kinasema hivi: “Ubatizo ni muhimu ili kuokolewa. Kama Kristo mwenyewe alivyosema, mtu asipozaliwa tena kwa maji na Roho Takatifu, hawezi kuingia katika Ufalme wa Mungu (Yoh 3.5).” Hivyo, wengine huamini kwamba wale waliokufa bila kubatizwa wanatupwa ndani ya moto wa mateso au wanateseka katika njia nyingine baada ya kufa.

Hata hivyo, kuna wengine wengi, ambao wanafikiri fundisho hilo halipatani na akili. Mamilioni ya watu wamekufa bila kujifunza Biblia. Je, wanastahili kuteswa milele? Biblia inasema nini kuhusu jambo hilo?

TUMAINI LILILOAHIDIWA KATIKA BIBLIA

Biblia inaonyesha waziwazi kwamba Mungu hawapuuzi watu walioishi bila kujua sheria zake. Andiko la Matendo 17:30 linatuhakikishia hivi: “Mungu ameachilia mbali nyakati hizo za kutojua.” Hivyo basi, Biblia inatoa tumaini gani kwa wale waliokufa bila kupata nafasi ya kujifunza kumhusu Mungu?

Ni nini maana ya ahadi hii ya Yesu: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso”?

Tunaweza kupata jibu katika maneno ambayo Yesu alimwambia mmoja wa wahalifu waliokufa pamoja naye. Mwanamume huyo alimwambia Yesu hivi: “Unikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.” Yesu alimjibuje? “Kwa kweli mimi nakuambia leo, utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”—Luka 23:39-43.

Je, Yesu alikuwa anaahidi kwamba mwanamume huyo angeenda mbinguni? La. Mwanamume huyo hakuwa ‘amezaliwa tena’ kwa maji na roho, jambo lililohitajiwa ili kuingia kwenye Ufalme wa mbinguni. (Yohana 3:3-6) Badala yake, Yesu alikuwa anaahidi kwamba mhalifu huyo ataishi tena, katika Paradiso. Akiwa Myahudi, inaelekea mwanamume huyo alijua kuhusu Paradiso ya kidunia, bustani ya Edeni inayoelezewa katika kitabu cha kwanza cha Biblia. (Mwanzo 2:8) Ahadi ya Yesu ilimpa tumaini hakika la kufufuliwa na kuishi katika Paradiso itakaporudishwa tena duniani.

Kwa kweli, Biblia inaahidi “ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) “Wasio waadilifu” ni wale ambao hawakufuata viwango vya Mungu vya uadilifu kwa sababu hawakujua mapenzi ya Mungu. Yesu atamfufua mhalifu huyo asiye mwadilifu aliyezungumza naye, na pia mamilioni, au labda mabilioni ya wengine ambao walikufa bila kupata ujuzi. Kisha, katika dunia iliyo Paradiso, watafundishwa matakwa ya Mungu, na watapata nafasi ya kuthibitisha kwamba wanampenda Mungu kwa kutii amri zake.

 WASIO WAADILIFU WATAKAPOFUFULIWA

Je, wasio waadilifu watakapofufuliwa, watahukumiwa kwa msingi wa matendo yao ya zamani? La. Andiko la Waroma 6:7 linasema hivi: “Kwa maana yeye ambaye amekufa ameondolewa hatia ya dhambi yake.” Wasio waadilifu watakuwa wamelipia dhambi zao kwa kufa. Hivyo, watahukumiwa kwa msingi wa yale watakayofanya baada ya kufufuliwa, si yale waliyofanya bila kujua kabla ya kufa. Watafaidikaje?

Baada ya ufufuo, wasio waadilifu watapata nafasi ya kujifunza sheria za Mungu, ambazo zitafunuliwa vitabu vya mfano vya kukunjwa vitakapofunguliwa. Kisha watahukumiwa ‘kulingana na matendo yao,’ yaani, ikiwa watatii sheria za Mungu au la. (Ufunuo 20:12, 13) Kwa wengi wa wasio waadilifu, hiyo haitakuwa fursa ya pili, bali nafasi yao ya kwanza ya kupata uzima wa milele duniani kwa kujifunza na kufanya mapenzi ya Mungu.

Fundisho hilo la Biblia limewasaidia wengi kumwamini tena Mungu. Yeong Sug ni mmoja wao. Alilelewa katika familia ya Kikatoliki. Watu fulani katika familia yao walikuwa makasisi. Kwa vile alitaka kuwa mtawa alijiunga na makao ya watawa. Baadaye, akaondoka kwa sababu alivunjwa moyo na mambo aliyoona huko. Isitoshe, alishindwa kuamini fundisho la moto wa mateso kwani alifikiri kwamba kuwatesa watu motoni ni jambo la kikatili na lisilo la haki.

Kisha, Shahidi wa Yehova akamwonyesha Yeong Sug maneno haya kwenye Biblia: “Kwa maana walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe, wala hawana malipo tena.” (Mhubiri 9:5) Shahidi huyo alimsaidia kutambua kwamba mababu zake hawateswi motoni. Badala yake, wamelala usingizi katika kifo, wakingoja kufufuliwa.

Akijua kwamba watu wengi hawajasikia ukweli ulio katika Biblia, Yeong Sug alichukua kwa uzito maneno ya Yesu kwenye Mathayo 24:14: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” Sasa yeye huhubiri habari njema na kuwaambia wengine kuhusu tumaini lake zuri linalotegemea Biblia.

“MUNGU HANA UBAGUZI”

Biblia hutueleza hivi: “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Hiyo ndiyo haki ambayo tunaweza kutazamia kutoka kwa Mungu ambaye “anapenda uadilifu na haki.”​—Zaburi 33:5.