Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAZUNGUMZO PAMOJA NA JIRANI

Ufalme wa Mungu Ulianza Kutawala Lini?(Sehemu ya 1)

Ufalme wa Mungu Ulianza Kutawala Lini?(Sehemu ya 1)

Mazungumzo yafuatayo yanaonyesha jinsi Shahidi wa Yehova anavyoweza kuzungumza na jirani yake. Hebu tuwazie Shahidi anayeitwa Cameron amemtembelea mwanamume anayeitwa Jon nyumbani kwake.

“ENDELEENI KUTAFUTA” UELEWAJI

Cameron: Jon, ninafurahia sana mazungumzo yetu ya Biblia. * Unakumbuka swali uliloniuliza kuhusu Ufalme wa Mungu? Ulitaka kujua kwa nini Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba Ufalme ulianza kutawala mwaka 1914.

Jon: Ndiyo, nilipokuwa nikisoma mojawapo ya machapisho yenu, niliona kwamba Ufalme wa Mungu ulianza kutawala mwaka 1914. Hilo lilinifanya niwe na udadisi kwa sababu mnasema kwamba mafundisho yenu yote yanategemea Biblia.

Cameron: Ni kweli, ndivyo ilivyo.

Jon: Sawa, mimi mwenyewe nimesoma Biblia nzima. Lakini sijawahi kuona sehemu yoyote inayotaja mwaka 1914. Kwa hiyo niliamua kutumia Biblia inayopatikana kwenye Intaneti na kufanya utafiti zaidi kuhusu mwaka 1914. Kwa kweli, sikupata jibu lolote.

Cameron: Nakupongeza kwa mambo mawili, Jon. Kwanza, umefaulu kusoma Biblia nzima. Huo ni uthibitisho kwamba unapenda Neno la Mungu.

Jon: Ni kweli. Hakuna kitabu bora kuliko Biblia.

Cameron: Nakubaliana nawe. Jambo la pili, nakupongeza kwa sababu umetafuta majibu kwa kutumia Biblia. Umefanya kile ambacho Biblia inatuhimiza kufanya: “Endeleeni kutafuta” uelewaji. * Hongera sana kwa jitihada zako.

Jon: Asante. Nataka kuendelea kujifunza. Kwa kweli, nilifanya utafiti zaidi kuhusu mwaka 1914 kwenye kitabu hiki ambacho tumekuwa tukisoma. Kinataja ndoto ambayo mfalme aliota—kuhusu mti mkubwa ambao ulikatwa na ukachipuka tena au kitu kama hicho.

Cameron: Aah, kweli kabisa! Unabii huo umeandikwa kwenye kitabu cha Danieli sura ya 4. Unahusu ndoto ambayo Mfalme Nebukadneza wa Babiloni aliota.

Jon: Kweli, ni sura hiyo. Nilisoma unabii huo tena na tena. Lakini kusema kweli, sioni unabii huo unahusianaje na Ufalme wa Mungu au mwaka 1914.

Cameron: Kwa kweli, Jon, hata nabii Danieli mwenyewe hakuelewa kwa ukamili unabii alioandika!

Jon: Eti hakuelewa!

Cameron: Ndiyo. Hapa kwenye andiko la Danieli 12:8, anasema hivi: “Mimi nami nikasikia, lakini sikuweza kuelewa.”

Jon: Kumbe si mimi peke yangu! Sasa afadhali!

Cameron: Ukweli ni kwamba Danieli hakuelewa kwa sababu haukuwa wakati wa Mungu kuwafunulia wanadamu maana ya unabii wa kitabu  cha Danieli. Lakini sasa, katika wakati wetu, tunaweza kuelewa unabii huo.

Jon: Kwa nini unasema hivyo?

Cameron: Vema, ona mstari unaofuata unavyosema. Danieli 12:9 inasema hivi: “Maneno hayo yamewekwa siri na kufungwa kwa muhuri mpaka wakati wa mwisho.” Kwa hiyo unabii huo ungeeleweka vizuri baada ya muda mrefu kupita, yaani, “wakati wa mwisho.” Kama tutakavyojifunza baadaye, uthibitisho unaonyesha kwamba tunaishi katika siku za mwisho. *

Jon: Kwa hiyo, unaweza kunifafanulia unabii wa Danieli?

Cameron: Nitajitahidi.

NDOTO YA NEBUKADNEZA

Cameron: Kwanza acha nieleze kwa ufupi kile ambacho Mfalme Nebukadneza aliona kwenye ndoto yake. Kisha tutazungumzia maana yake.

Jon: Sawa.

Cameron: Katika ndoto hiyo, Nebukadneza aliona mti mkubwa ambao ulifika mbinguni. Kisha akasikia mjumbe wa Mungu akiamuru kwamba mti huo ukatwe. Hata hivyo, Mungu alisema kisiki chake kising’olewe. Baada ya kipindi cha “nyakati saba,” mti huo ungechipuka tena. * Mwanzoni unabii huo ulimhusu Mfalme Nebukadneza mwenyewe. Ingawa alikuwa mfalme mashuhuri—kama mti wenye matawi yake mbinguni—aliangushwa chini kwa kipindi cha “nyakati saba.” Unakumbuka kilichompata?

Jon: Wala, sikumbuki.

Cameron: Hakuna tatizo. Biblia inaonyesha kwamba Nebukadneza alipatwa na wazimu, kwa miaka saba. Katika kipindi hicho, hakuweza kutawala akiwa mfalme. Lakini baada ya nyakati saba, Nebukadneza alirudiwa na akili na akaanza tena kutawala. *

Jon: Sawa, tuko pamoja hadi sasa. Lakini mambo hayo yanahusuje Ufalme wa Mungu na mwaka 1914?

Cameron: Kwa ufupi, unabii huu ulitimizwa kwa njia mbili. Utimizo wa kwanza ulitukia wakati utawala wa Mfalme Nebukadneza ulipokatizwa. Utimizo wa pili unahusu kukatizwa kwa utawala wa Mungu. Kwa hiyo utimizo huu wa pili ndio unaohusu Ufalme wa Mungu.

Jon: Unajuaje kwamba unabii huo una utimizo wa pili unaohusiana na Ufalme wa Mungu?

Cameron: Kwanza kabisa, tunapata uhakika kwa sababu ya unabii wenyewe. Kulingana na andiko la Danieli 4:17, unabii ulitolewa “kusudi watu wanaoishi wajue kwamba Aliye Juu Zaidi ni Mtawala katika ufalme wa wanadamu na kwamba humpa yeyote yule amtakaye.” Je, unaona maneno “ufalme wa wanadamu”?

Jon: Ndiyo, panasema “Aliye Juu Zaidi ni Mtawala katika ufalme wa wanadamu.”

Cameron: Sawa kabisa. Unafikiri “Aliye Juu Zaidi” ni nani?

Jon: Nadhani maneno hayo yanamhusu Mungu.

Cameron: Uko sahihi. Kwa hiyo maneno hayo yanaonyesha kwamba unabii huo haumhusu tu Nebukadneza. Pia, unahusisha “ufalme wa wanadamu,” yaani, utawala wa Mungu juu ya wanadamu. Na hilo pia linapatana na muktadha wa unabii huo.

Jon: Unamaanisha nini?

UJUMBE WA KITABU CHA DANIELI

Cameron: Mara kwa mara kitabu cha Danieli hukazia ujumbe fulani wa msingi. Kinaeleza kuhusu kuanzishwa kwa Ufalme wa Mungu chini ya utawala wa Mwana wa Mungu, Yesu. Kwa mfano, acha turudi nyuma sura kadhaa. Tafadhali soma Danieli 2:44.

Jon: Sawa. Andiko hilo linasema: “Katika siku za wafalme hao, Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na  ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”

Cameron: Asante. Je, mstari huu unazungumza kuhusu Ufalme wa Mungu?

Jon: Mmmhh. Sina uhakika.

Cameron: Sawa, lakini unaona mstari huo unasema kwamba Ufalme huo “utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” Je, kuna serikali yoyote ya wanadamu inayoweza kudumu milele, isipokuwa Ufalme wa Mungu?

Jon: Hakuna.

Cameron: Kuna unabii mwingine wa Danieli unaotaja Ufalme wa Mungu. Unapatikana katika andiko la Danieli 7:13, 14. Kuhusu mtawala wa wakati ujao, unabii unasema hivi: “Akapewa utawala na heshima na ufalme, ili vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha vimtumikie yeye. Utawala wake ni utawala unaodumu mpaka wakati usio na kipimo ambao hautapitilia mbali, na ufalme wake ni ufalme ambao hautaharibiwa.” Je, kuna jambo lolote katika unabii huo ambalo unalijua?

Jon: Andiko hilo linataja ufalme.

Cameron: Umesema kweli. Na mstari huo hautaji ufalme wowote tu. Ona kwamba Ufalme huo ungekuwa na mamlaka juu ya “vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha.” Yaani, Ufalme huu utatawala dunia nzima.

Jon: Sikuona hilo, lakini uko sahihi. Biblia inasema hivyo.

Cameron: Pia, ona jambo lingine linalotajwa kwenye unabii huo: “Utawala wake ni utawala unaodumu mpaka wakati usio na kipimo ambao hautapitilia mbali, na ufalme wake ni ufalme ambao hautaharibiwa.” Unabii huu unafanana na maneno tuliyosoma kwenye Danieli 2:44, au sivyo?

Jon: Ndiyo, unafanana.

Cameron: Acha turudie mambo tuliyojifunza. Unabii kwenye Danieli sura 4 ulitolewa ili watu wajue kwamba “Aliye Juu Zaidi ni Mtawala katika ufalme wa wanadamu.” Maneno haya yanathibitisha kwamba unabii huo haukumhusu tu Mfalme Nebukadneza bali pia ulikuwa na utimizo mkubwa zaidi. Katika kitabu chote cha Danieli, kuna unabii mbalimbali unaohusu kuanzishwa kwa Ufalme wa Mungu chini ya utawala wa Yesu. Je, huoni kwamba unabii kwenye kitabu cha Danieli sura ya 4 unahusu pia Ufalme wa Mungu?

Jon: Ni kweli. Hata hivyo, mwaka 1914 unahusikaje?

“NYAKATI SABA ZIPITE”

Cameron: Sawa acha tuzungumzie tena kuhusu Mfalme Nebukadneza. Aliwakilishwa na ule mti kwenye ndoto katika utimizo wa kwanza. Utawala wake ulikatizwa mti ulipokatwa na kuachwa kwa nyakati saba, yaani, alipopatwa na wazimu kwa kipindi fulani. Kipindi hicho cha nyakati saba kiliisha Nebukadneza aliporudiwa na akili zake na kurudi kwenye utawala. Katika utimizo wa pili wa unabii huo, utawala wa Mungu ungekatizwa kwa muda fulani—hata hivyo si kwa sababu Mungu hana uwezo.

Jon: Unamaanisha nini?

Cameron: Katika nyakati za Biblia, wafalme wa Israeli waliotawala katika Yerusalemu walisemekana kuketi katika “kiti cha ufalme cha Yehova.” * Walimwakilisha Mungu katika kutawala  watu wake. Kwa hiyo, utawala wa wafalme hao uliwakilisha utawala wa Mungu. Hata hivyo, baadaye, wengi kati ya wafalme hao walikosa kumtii Mungu na raia zao wakawafuata. Kwa sababu ya uasi wa Waisraeli, Mungu aliruhusu washindwe na Wababiloni mwaka 607 K.W.K. Kuanzia wakati huo, hakuna mfalme katika Yerusalemu aliyemwakilisha Yehova. Kwa hiyo, utawala wa Mungu ulikatizwa. Je, tuko pamoja mpaka hapo?

Jon: Ndiyo.

Cameron: Kwa hiyo mwaka 607 K.W.K. ulikuwa mwanzo wa nyakati saba, au kipindi ambacho utawala wa Mungu ungekatizwa. Mwishoni mwa nyakati saba, Mungu angeweka mtawala ambaye angemwakilisha, hangekuwa duniani, bali mbinguni. Hapo ndipo unabii mwingine tuliosoma katika kitabu cha Danieli ungetimizwa. Kwa hiyo swali kuu ni: Nyakati saba zilikamilika lini? Tukijibu swali hilo, tutajua wakati ambapo Ufalme wa Mungu ulianza kutawala.

Jon: Aaahh kumbe! Acha nijaribu—nyakati saba zilikamilika mwaka 1914?

Cameron: Umepata! Kweli kabisa.

Jon: Lakini tunajuaje?

Cameron: Alipokuwa hapa duniani, Yesu alionyesha kwamba nyakati saba hazikuwa zimeisha. * Kwa hiyo, inaonekana ni kipindi kirefu sana cha wakati. Nyakati saba zilianza miaka mingi kabla Yesu hajaja duniani, na ziliendelea hata baada ya yeye kurudi mbinguni. Pia, kumbuka kwamba unabii wa Danieli ungeeleweka kikamili “wakati wa mwisho.” * Jambo la kupendeza, katika karne ya 19, wanafunzi wanyoofu wa Biblia walianza kuchunguza unabii huo pamoja na unabii mwingine kwa makini sana. Walianza kutambua kwamba nyakati saba zingekamilika mwaka 1914. Matukio ya ulimwengu tangu 1914 yanathibitisha kwamba kwa kweli mwaka huo Ufalme wa Mungu ulianza kutawala mbinguni. Kuanzia mwaka huo ulimwengu uliingia katika siku zake za mwisho, yaani wakati wa mwisho. Sasa, naona haya ni mambo mengi sana ya kufikiria . . .

Jon: Ndiyo. Ninahitaji kusoma tena mambo hayo ili niyaelewe.

Cameron: Usiwe na wasiwasi. Mimi pia sikuelewa jambo hilo mara moja. Lakini natumaini mazungumzo yetu yamekusaidia kuona kwamba mafundisho ya Mashahidi wa Yehova kuhusu Ufalme yanategemea Biblia.

Jon: Ni kweli. Mimi huvutiwa na jinsi mafundisho yenu yanavyotegemea Biblia.

Cameron: Naona wewe pia una lengo hilo. Kama nilivyosema, ni vigumu kuelewa mambo hayo yote mara moja. Huenda bado una maswali fulani. Kwa mfano, tumeona kwamba nyakati saba zinahusiana na Ufalme wa Mungu na kwamba zilianza mwaka 607 K.W.K. Lakini, tunajuaje kwamba nyakati saba zilikamilika mwaka 1914? *

Jon: Ndiyo, hata mimi najiuliza swali hilo.

Cameron: Biblia yenyewe inatusaidia kujua urefu wa zile nyakati saba. Je, ungependa tuzungumzie jambo hilo nitakaporudi? *

Jon: Ni sawa.

Je, kuna jambo lolote kuhusu Biblia ambalo limekuwa likikutatiza? Je, kuna jambo lolote ambalo Mashahidi wa Yehova wanaamini au kufanya ambalo ungependa kulifahamu zaidi? Ikiwa ndivyo, utakapokutana tena na Mashahidi wa Yehova usikose kuwauliza. Watafurahi kuzungumzia jambo hilo pamoja nawe.

^ fu. 5 Kupitia mpango wao wa kujifunza Biblia na watu nyumbani kwao bila malipo, Mashahidi wa Yehova hutumia utaratibu fulani ili kuwafundisha Biblia.

^ fu. 21 Ona sura ya 9 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Pia, kinapatikana kwenye www.ps8318.com/sw.

^ fu. 63 Katika unabii wake kuhusu siku za mwisho, Yesu alisema hivi: “Yerusalemu [jiji lililowakilisha utawala wa Mungu] litakanyagwa-kanyagwa na mataifa, mpaka nyakati zilizowekwa za mataifa zitimie.” (Luka 21:24) Kwa hiyo kukatizwa kwa utawala wa Mungu kulikuwa kunaendelea Yesu alipokuwa duniani na kungeendelea hadi siku za mwisho.

^ fu. 69 Makala itakayofuata ya mfululizo huu itazungumzia mistari ya Biblia inayotusaidia kuelewa urefu wa zile nyakati saba.