Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sayansi na Kitabu cha Mwanzo

Sayansi na Kitabu cha Mwanzo

Watu wengi hudai kwamba sayansi huthibitisha kwamba masimulizi ya Biblia kuhusu uumbaji si ya kweli. Lakini, tofauti iliyopo, si kati ya sayansi na Biblia, bali ni kati ya sayansi na vikundi vya Wakristo Wahafidhina. Baadhi ya vikundi hivyo hudai isivyo kweli kwamba kulingana na Biblia, vitu vyote viliumbwa kwa siku sita zenye urefu wa saa 24, miaka 10,000 hivi iliyopita.

Hata hivyo, Biblia haiungi mkono dhana hiyo. Ikiwa ingekuwa hivyo, basi mambo mengi ambayo yamevumbuliwa na wanasayansi katika kipindi cha miaka 100 ambayo imepita bila shaka yangethibitisha kwamba Biblia si ya kweli. Ukiichunguza Biblia kwa makini, utaona kwamba haipingani hata kidogo na mambo ya kisayansi ambayo yamethibitishwa. Kwa sababu hiyo, Mashahidi wa Yehova hawakubaliani na dhana za vikundi hivyo au wengine wenye imani kama hizo. Mambo yafuatayo yanaonyesha yale ambayo Biblia inafundisha hasa.

Kitabu cha Mwanzo hakifundishi kwamba dunia na ulimwengu ziliumbwa katika siku sita zenye urefu wa saa 24, miaka 10,000 hivi iliyopita

“Mwanzo” ni Lini?

Masimulizi ya kitabu cha Mwanzo yanaanza kwa taarifa hii sahili lakini yenye kujaa maana: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1) Wasomi kadhaa wa Biblia wanakiri kwamba taarifa hiyo inafafanua jambo tofauti na mambo yaliyofanywa katika zile siku za uumbaji zinazozungumziwa kuanzia mstari wa 3. Yaani, kulingana na maneno ya ufunguzi ya Biblia, tayari ulimwengu, kutia ndani Dunia yetu, ulikuwako kwa muda usiojulikana kabla ya siku za uumbaji.

Wanajiolojia wanakadiria kwamba dunia imekuwako kwa muda wa miaka bilioni 4, nao waastronomia hukadiria kwamba huenda ulimwengu umekuwako kwa muda wa miaka bilioni 15. Je, mavumbuzi hayo—na mengine yatakayovumbuliwa wakati ujao—yanapingana na Mwanzo 1:1? Hapana. Biblia haitaji muda hususa ambao “mbingu na dunia” zimekuwako. Sayansi haipingani na mambo yanayosemwa katika Biblia.

Urefu wa Siku za Uumbaji

Siku za uumbaji zilikuwa na urefu gani? Je, zilikuwa siku halisi, zenye urefu wa saa 24? Watu fulani hudai kwamba kwa kuwa Musa, aliyeandika kitabu cha Mwanzo, alirejelea siku iliyofuata siku sita za uumbaji kuwa kigezo cha Sabato ya kila juma, kila moja ya siku za uumbaji lazima ilikuwa siku yenye urefu wa saa 24. (Kutoka 20:11) Je, maneno ya kitabu cha Mwanzo yanaunga mkono maoni hayo?

Hapana. Mbali na kipindi cha saa 24, neno la Kiebrania linalotafsiriwa “siku” laweza pia kurejelea vipindi vyenye urefu tofauti-tofauti. Kwa mfano, akitoa muhtasari wa kazi za Mungu za uumbaji, Musa anazirejelea siku zote sita za uumbaji kana kwamba ni siku moja. (Mwanzo 2:4) Bila shaka, hakuna msingi wowote wa Kimaandiko unaoonyesha kwamba kila siku ya uumbaji ilikuwa na urefu wa saa 24.

Hivyo basi, siku za uumbaji zilikuwa na urefu gani? Biblia haijibu; hata hivyo, maneno ya Mwanzo sura ya 1 na ya 2 yanadokeza kwamba siku zinazozungumziwa ni vipindi virefu vya wakati.

Vipindi Sita vya Uumbaji

Musa aliandika masimulizi yake katika Kiebrania, naye aliyaandika kwa njia inayopatana na maoni ya mtu aliye duniani. Mambo hayo mawili pamoja na ukweli wa kwamba ulimwengu ulikuwako kabla ya mwanzo wa vile vipindi au siku za uumbaji, yanasaidia kutatua ubishi mwingi kuhusu masimulizi ya uumbaji. Jinsi gani?

Matukio yaliyoanza “siku” moja yaliendelea katika “siku” ya pili au zaidi zilizofuata

Kuchunguza kwa makini masimulizi ya kitabu cha Mwanzo kunafunua kwamba matukio yaliyoanza “siku” moja yaliendelea katika “siku” ya pili au zaidi zilizofuata. Kwa mfano, kabla ya “siku” ya kwanza ya uumbaji, mwanga wa jua, ambalo tayari lilikuwako, haukuwa ukifika duniani, labda kwa sababu ya mawingu mazito. (Ayubu 38:9) Katika “siku” ya kwanza, mawingu hayo yalianza kutanzuka na kuuruhusu mwanga upenye angani. *

Katika “siku” ya pili, yaonekana kwamba anga lilizidi kutanzuka na kutokeza mgawanyiko kati ya mawingu mazito yaliyo juu na bahari. Katika “siku” ya nne, anga lilikuwa limetanzuka vya kutosha hivi kwamba jua na mwezi vingeweza kuonekana “katika anga la mbingu.” (Mwanzo 1:14-16) Yaani, kwa mtu aliye duniani, jua na mwezi vilianza kuonekana. Yote hayo yalitukia hatua kwa hatua.

Pia, kulingana na masimulizi ya Mwanzo, kadiri anga lilivyozidi kutanzuka, viumbe vinavyoruka—kutia ndani wadudu na viumbe vingine vyenye mabawa—vilianza kuonekana katika “siku” ya tano.

Kutokana na masimulizi ya Biblia, inawezekana kwamba matukio fulani muhimu ya kila siku, au kipindi cha uumbaji, hayakutendeka mara moja bali hatua kwa hatua, huenda hata baadhi ya matukio hayo yaliendelea hadi “siku” ya uumbaji iliyofuata. *

Kulingana na aina yake

Kwa kuwa mimea na wanyama walitokezwa hatua kwa hatua, je, hilo linamaanisha kwamba Mungu alitumia mageuzi kutokeza aina mbalimbali za vitu vilivyo hai? Hapana. Masimulizi yanataja waziwazi kwamba Mungu aliumba “aina” zote za msingi za mimea na wanyama. (Mwanzo 1:11, 12, 20-25) Je, “aina” hizo za awali za mimea na wanyama ziliumbwa zikiwa na uwezo wa kiasili wa kuzoeleana na mazingira mapya? Ni nini kinachomaanishwa na neno “aina”? Biblia haifafanui. Hata hivyo, inasema kwamba viumbe vyenye uhai ‘vilijaa kulingana na aina zake.’ (Mwanzo 1:21) Taarifa hiyo inadokeza kwamba kuna mipaka ya kiasili inayodhibiti tofauti za viumbe katika kila “aina.” Rekodi ya visukuku na utafiti wa karibuni zinaonyesha wazi kwamba kumekuwa na mabadiliko madogo sana katika aina za msingi za mimea na wanyama hata baada ya vipindi virefu sana vya wakati.

Watafiti wa siku zetu wanathibitisha kwamba viumbe vyote vyenye uhai huzaana “kulingana na aina yake”

Tofauti na madai ya wahafidhina wa kidini, kitabu cha Mwanzo hakifundishi kwamba ulimwengu, kutia ndani dunia na viumbe vyenye uhai, uliumbwa katika kipindi kifupi cha wakati, miaka 10,000 hivi iliyopita. Badala yake, masimulizi ya Mwanzo kuhusu kuumbwa kwa ulimwengu na viumbe vyenye uhai duniani yanapatana na mavumbuzi ya karibuni ya kisayansi.

Kwa sababu ya imani zao za kifalsafa, wanasayansi wengi hupinga fundisho la Biblia kwamba Mungu aliumba vitu vyote. Hata hivyo, katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo kilichoandikwa zamani za kale, Musa aliandika kuwa ulimwengu ulikuwa na mwanzo na uhai ulitokezwa hatua kwa hatua, katika vipindi virefu vya wakati. Musa angewezaje kupata habari hizo zilizo sahihi kisayansi yapata miaka 3,500 hivi iliyopita? Kuna jibu moja tu linalopatana na akili. Mwenye hekima na nguvu za kuumba mbingu na dunia ndiye aliyempa Musa habari hizo zilizo sahihi kisayansi. Hilo linaunga mkono dai la Biblia kwamba ‘imeongozwa na roho ya Mungu.’ *2 Timotheo 3:16.

Huenda ukasema, kile ninachoamini si hoja, iwe ninaamini masimulizi ya Biblia kuhusu uumbaji au hapana, yote ni mamoja. Hata hivyo, fikiria sababu kadhaa zinazoonyesha uzito wa suala hilo.

^ fu. 13 Katika masimulizi kuhusu “siku” ya kwanza, neno la Kiebrania linalotafsiriwa mwanga ni ’ohr, linaloweza kurejelea mwanga wowote ule, lakini kuhusu “siku” ya nne, neno lililotumiwa ni ma·’ohrʹ, linalorejelea chanzo cha mwanga.

^ fu. 16 Kwa mfano, katika siku ya sita ya uumbaji, Mungu aliagiza kwamba wanadamu ‘wawe wengi waijaze dunia.’ (Mwanzo 1:28, 31) Hata hivyo, hilo lilianza kutimia katika “siku” inayofuata.—Mwanzo 2:2.

^ fu. 20 Unaweza kupata habari zaidi kwa kutazama video fupi yenye kichwa Tunawezaje Kuwa na Hakika Kwamba Yale Yaliyoandikwa Katika Biblia Ni ya Kweli? inayopatikana kwenye tovuti ya jw.org/sw.