Hamia kwenye habari

Waunganishwa Katika Upendo​—Kusanyiko Jijini Frankfurt, Ujerumani

Waunganishwa Katika Upendo​—Kusanyiko Jijini Frankfurt, Ujerumani

“Ni Kama Sherehe ya Familia” ndivyo kilivyosema kichwa kikuu cha gazeti la Frankfurter Rundschau. Waliohudhuria walikubaliana na maneno hayo.

“Walinifanya nijihisi nimestarehe!” akasema Karla, anayeishi nchini Puerto Riko.

“Nilihisi kana kwamba nilikuwa ninaitembelea familia yangu inayoishi sehemu nyingine ya dunia,” akasema Sara, anayeishi nchini Australia.

Ni nini kilichowafanya wahisi hivyo? Ni kusanyiko la kimataifa la Mashahidi wa Yehova lililofanyika Julai 18 hadi 20, 2014 katika uwanja wa Commerzbank-Arena, jijini Frankfurt am Main, Ujerumani. Karibu watu 37,000 walihudhuria kusanyiko hilo.

Walikusanyika ili kujifunza Biblia. Programu hiyo ya elimu ilitia ndani usomaji wa Biblia, kuimba nyimbo, sala, drama mbili, na hotuba zenye kusisimua zinazotegemea Biblia.

Mbali na Mashahidi wanaoishi katika nchi hiyo, zaidi ya wajumbe 3,000 kutoka Afrika Kusini, Australia, Lebanoni, Marekani, Serbia, Ugiriki, na Uingereza walihudhuria kusanyiko hilo. Mashahidi 234 kutoka nchi 70 walio katika utumishi wa pekee, kama vile wamishonari, walihudhuria pia.

Maeneo 19 nchini Ujerumani na mengine nchini Austria na Uswisi yaliunganishwa kupitia Intaneti kwa ajili ya sehemu za programu hiyo. Jumla ya watu waliohudhuria kusanyiko hilo ilikuwa 204,046.

Kukabili Tofauti za Lugha

Jijini Frankfurt, programu ilikuwa katika Kiingereza, Kijerumani, na Kigiriki. Katika maeneo mengine, hotuba zilitafsiriwa katika lugha 17, kutia ndani Kiarabu, Kichina, Kitamili, Kituruki, na katika lugha mbili za ishara.

Ingawa Mashahidi hao walizumgumza lugha tofauti na walitoka nchi na tamaduni mbalimbali, hawakuwa na migawanyiko​—waliunganishwa na upendo. (Yohana 13:34, 35) Walitendeana kama ndugu na dada.

Tobias, anayeishi nchini Uingereza alisema hivi: “Tulijionea wazi kwamba undugu wetu ni wa kimataifa.”

Davianna, mjumbe kutoka Puerto Riko alieleza hivi: “Nilikutana na Mashahidi kutoka zaidi ya nchi 20. Sote tuna umoja kwa sababu tunampenda Mungu na pia tunapendana.”

Malcom mjumbe kutoka Australia alieleza hivi: “Nilipobatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova nilikuwa nikiishi katika kijiji kidogo. Nilisoma na hata kutazama video kuhusu undugu wetu wa pekee. Lakini hapa, nimeushuhudia undugu huo. Kwa hiyo, ninauthamini hata zaidi. Imani yangu imeimarishwa sana kwa sababu ya kuwa hapa.”

Ukaribishaji wa Pekee

Mashahidi wa makutaniko 58 jijini Frankfurt na maeneo jirani waliwaandalia wajumbe zawadi na burudani wakati wa jioni.

Cynthia, anayeishi Marekani alisema hivi: “Tulikaribishwa vizuri sana. Sitasahau kamwe upendo, fadhili, na ukarimu ambao ndugu hao walituonyesha.”

“Tulionyeshwa upendo mwingi na watu walicheka kwa furaha. Tulijifunza mengi kutoka kwa ndugu zetu,” alieleza Simon, anayeishi Ujerumani.

“Burudani zilizokuwepo jioni zilinithibitishia kuwa Mashahidi wa Yehova wanajua jinsi ya kujifurahisha. Burudani zetu ni safi na zenye kustarehesha,” akaeleza Amy, mjumbe kutoka Australia.

Mambo Mazuri ya Kukumbuka

Kusanyiko hilo la Frankfurt ni mojawapo ya makusanyiko ya kimataifa yaliyofanywa katika nchi tisa ulimwenguni pote.

Mjumbe mmoja alipoulizwa alihisije alipohudhuria kusanyiko jijini Frankfurt, alisema hivi: “Hebu wazi unakutana kwa mara ya kwanza na mtu ambaye hukujua kwamba ni ndugu yako. Mnapokutana anakupenda na kukukaribisha nyumbani kwake. Unafurahia sana. Hebu wazia kuwa kati ya watu 37,000 wanaokufanya uwe na shangwe kama hiyo. Hivyo ndivyo tulivyohisi.”