Hamia kwenye habari

Kuhitimu kwa Darasa la 137 la Shule ya Gileadi

Kuhitimu kwa Darasa la 137 la Shule ya Gileadi

Septemba 13, 2014, darasa la 137 la Shule ya Gileadi lilihitimu katika kituo cha elimu cha Mashahidi wa Yehova huko Patterson, New York. Shule hiyo huwazoeza wahudumu ambao tayari wana uzoefu mwingi ili wawe na matokeo zaidi katika kuimarisha makutaniko na ofisi za tawi ambazo wanatumwa. Wasikilizaji 12,333 walihudhuria programu hiyo. Baadhi yao walikuwepo kwenye kituo cha elimu cha Mashahidi wa Yehova cha Patterson na wengine waliunganishwa kupita Intaneti katika maeneo mbalimbali nchini Jamaika, Kanada, Marekani, na Puerto Rico.

Samuel Herd, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova alikuwa mwenyekiti wa programu hiyo. Katika maneno yake ya ufunguzi, alikazia jinsi mawazo ya Yehova yalivyo juu kuliko mawazo yetu. (Isaya 55:​8, 9) Alisema kwamba hata baada ya miezi mitano ya kujazwa akilini mawazo ya Mungu, wanafunzi hao wa Gileadi walikuwa wameanza tu kupata ujuzi juu ya Mungu, wamejua tu “kingo za njia za [Mungu].” (Ayubu 26:14) Ndugu Herd alisema kwamba kila mara tunapokutana ili kuzungumzia mawazo ya Mungu, tunafaidika na akasema kwamba programu ya kuhitimu ingetimiza jambo hilo pia.

“Tunda la Roho Ni . . . Ustahimilivu.” (Wagalatia 5:​22) John Larson, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi la Marekani, alikazia njia mbili ambazo tunaweza kuonyesha ustahimilivu, sifa ya tunda la roho ya Mungu. Kwanza, tunapaswa kuwa wenye ustahimilivu kumwelekea Yehova anapotuzoeza na kutusaidia kuwa wenye imani yenye nguvu. (1 Petro 5:​10) Abrahamu alikuwa mmoja wa watu walioweka mfano mzuri wa ustahimilivu Yehova alipokuwa akimzoeza na mwishowe Yehova alitimiza ahadi yake.​—Waebrania 6:​15.

Pili, tunahitaji kuwa wenye ustahimilivu kujielekea. Baada ya kupokea mazoezi ya Gileadi, wanafunzi wanaweza kujiwekea miradi mikubwa sana. Mambo yasipoenda kama wanavyotarajia, wanaweza kujiuliza, ‘Kwani nina tatizo gani?’ Ndugu Larson aliwaeleza mambo aliyojionea mwenyewe, na akawahakikishia kwamba wanaweza kushinda hali yoyote ngumu iwapo wataendelea kuwa wenye ustahimilivu kujielekea na kuwa wenye bidii huku Mungu akimaliza mazoezi yao.​—Waebrania 6:​11, 12.

“Dumisheni Unyenyekevu Mioyoni Mwenu na Mwishi Milele!” Kichwa cha hotuba ya Anthony Morris wa Baraza Linaloongoza kilitegemea Zaburi 22:26, sehemu ya mwisho ya andiko hilo inamaanisha kihalisi “mioyo yenu na iishi milele.” Ili kupokea baraka hiyo, lazima tuwe wanyenyekevu. Ndugu Morris alikazia kwamba tunakosa thamani mbele ya Yehova ikiwa sisi si wanyenyekevu. Yeyote kati yetu, hata Wakristo wa muda mrefu, wanaweza kujikuta wakipuuza umuhimu wa kuwa kama Kristo Yesu.​—2 Petro 1:9.

Biblia huonyesha mifano ya watu waliokuwa wanyenyekevu na wale ambao hawakuwa wanyenyekevu. Herode Agripa alikubali kwa kiburi sifa ya watu walipompa utukufu ambao ni Mungu peke yake aliyestahili kupewa, kwa sababu hiyo malaika wa Mungu akampiga na “akaliwa na wadudu.” (Matendo 12:21-​23) Kinyume chake, Petro, baada ya kukemewa na Yesu kwa kuwa alifikiri “si fikira za Mungu, bali za wanadamu,” hakununa wala kukasirika. (Mathayo 16:21-​23) Alikubali nidhamu na akawa mfano mzuri wa unyenyekevu.​—1 Petro 5:5.

Baadhi ya wanafunzi wataanza utumishi wa Betheli kwenye ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova, na Ndugu Morris aliwaonya kwamba ikiwa hawatakuwa wanyenyekevu hawatafurahia mgawo wao. Hata hivyo, si rahisi kutambua kwamba tunakosa sifa ya unyenyekevu. Ili kukazia jambo hilo, alisema miaka mingi iliyopita mzee fulani aliposhauriwa kwa kukosa unyenyekevu, aliandikia ofisi ya tawi barua akisema hivi, “Sijakutana na mtu mwingine mnyenyekevu kama mimi.” Ndugu Morris aliwatia moyo wanafunzi waepuke mtazamo kama huo. Wataendelea kuwa wanyenyekevu ikiwa wataepuka kujiona kuwa wenye mamlaka kupita kiasi na badala yake kutambua kwamba mamlaka halisi ni ya Yehova Mungu na Kristo Yesu.

“Hatoi ‘Roho kwa Kipimio.’” (Yohana 3:​34) Michael Burnett, mwalimu wa Gileadi, aliwakumbusha wanafunzi kwamba roho takatifu itawasaidia kushinda hali ngumu au mashaka ambayo watakabili kwenye migawo yao. Roho ya Mungu ilimwezesha Bezaleli kushinda hali ngumu katika mgawo wake wa kujenga maskani. (Kutoka 35:30-​35) Roho takatifu iliboresha kipawa cha Bezaleli cha usanii na kumwezesha pia kuwafundisha wengine. Roho takatifu inaweza kufanya vivyo hivyo kwa wahitimu wa shule ya Gileadi, hasa wanapofuata kielelezo cha kufundisha kutoka kwenye Biblia, jambo ambalo walijifunza darasani.

Wakati wa Bezaleli, wanawake Waisraeli walitimiza jukumu muhimu katika kujenga maskani. (Kutoka 35:25, 26) Vivyo hivyo, dada waliokuwa darasani walithibitika kuwa “wenye hekima ya moyo” kwa kuwaunga mkono waume zao. Ndugu Burnett alimalizia kwa kuwashauri wanafunzi hivi: “Vipawa vyako na viongozwe na unyenyekevu na roho ya utii. Ukifanya hivyo, Yehova atakupa roho yake kikamili.”

“Je, Utacheza Dansi na Mimi?” Mark Noumair, msaidizi wa Halmashauri ya Ufundishaji, alizungumzia kichwa hicho kwa kutumia mfano wa Mfalme Daudi wakati ambapo sanduku la agano lililetwa Yerusalemu. (2 Samweli 6:​12-​14) Kwa unyenyekevu Daudi alicheza dansi pamoja na “vijakazi wa watumishi wake” sanduku la agano lilipokuwa linaingizwa Yerusalemu. (2 Samweli 6:​20-​22) Vijakazi hao hawangesahau kamwe siku ambayo Mfalme Daudi alicheza dansi pamoja nao. Kisha Ndugu Noumair akawatia moyo wanafunzi ‘wacheze dansi na vijakazi.’ Aliwauliza hivi: “Je, utajulikana kama mtu anayewasaidia wale wasio na madaraka makubwa au wasio na madaraka yoyote? . . . Je, utawathamini wengine kwa sababu ya sifa zao za kiroho?”

Wahitimu watakuwa wakimwiga Yehova wakiendelea kuonyesha upendo mshikamanifu katika njia hiyo. (Zaburi 113:​6, 7) Hata ikiwa baadhi ya watu wanaowazunguka wanashindwa kuonyesha unyenyekevu, wanafunzi hawapaswi kuruhusu kutokamilika kwa wengine kuwaathiri. Ndugu Noumair alisema hivi: “Jione kana kwamba wewe si kitu,” kisha akaongezea: “Watendee kondoo za Yehova jinsi ambavyo Yeye angewatendea.”

“Kutoa Ushahidi Kila Unapopata Fursa.” William Samuelson, mwangalizi wa Idara ya Shule za Kitheokrasi, alisema kuwa mtume Paulo alitumia kila fursa kuhubiri habari njema. (Matendo 17:17) Kisha Ndugu Samuelson akaongoza sehemu ambayo wanafunzi waliigiza mambo yaliyoonwa waliyofurahia katika utumishi wa shambani wakati wa shule. Kwa mfano, wenzi fulani wa ndoa walikutana na mhudumu wa duka moja. Walisubiri hadi wateja walipopungua kisha wakamwonyesha video Kwa Nini Ujifunze Biblia? Pia walimwelekeza kwenye tovuti ya jw.org, ambako alipata habari zaidi katika lugha yake ya Kilao. Wenzi hao walifaulu pia kurudi na kuchochea upendezi wa mwanamke huyo.

“Endelea Kuwa Tayari kwa Utumishi wa Ufalme.” William Nonkes, anayefanya kazi kwenye Idara ya Utumishi kwenye ofisi ya tawi ya Marekani, aliwahoji wanafunzi wanne waliohitimu. Kupatana na andiko la Isaya 6:8 walikuwa wamejitoa kwa ajili ya utumishi wa Ufalme, lakini shule hiyo iliwasaidia kufanya hivyo zaidi. Dada Snolia Maseko alieleza kwamba Gileadi ilifunua mambo ambayo angefanyia maendeleo, hasa kutumia wakati kwa hekima baada ya siku yenye shughuli nyingi katika utumishi. Alisema hivi, “Mazoezi hayo yamenisaidia kuboresha uwezo wangu kuliko nilivyofikiri ningeweza.” Ndugu Dennis Nielsen alijifunza jinsi wazo lililo katika Sefania 3:​17 linavyoweza kumsaidia kuepuka kuvunjika moyo katika utumishi wake. Ndugu Nielsen alisema, “Hata nisipopata matokeo mazuri katika utumishi, Yehova anashangilia kwa sababu ninamwonyesha upendo, nami napaswa kushangilia pia.”

“Waangalieni kwa Makini Ndege wa Mbinguni.” (Mathayo 6:​26) Stephen Lett wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya msingi kwenye programu hiyo. Akitegemeza hotuba yake kwenye maneno ya Yesu kwamba tunapaswa ‘kuwaangalia ndege kwa makini,’ au kuwachunguza kwa uangalifu, Ndugu Lett alionyesha mambo fulani ambayo ndege wanaweza kutufunza.​—Ayubu 12:7.

Kwa mfano, kama tu Yehova anavyowalisha ndege, ndivyo atakavyotuandalia pia. Sisi ni washiriki wa “nyumba ya Mungu,” na anatuhakikishia kwamba ‘atawaandalia mahitaji wale walio wake mwenyewe.’ (1 Timotheo 3:​15; 5:8) Ni kweli, lazima tutimize sehemu yetu. Kwa kuwa ndege lazima wajitahidi kutafuta chakula ambacho Mungu anaandaa, lazima tuendelee “kuutafuta kwanza ufalme” ili tupate baraka zake.​—Mathayo 6:​33.

Ndugu Lett alitaja pia kwamba ndege wengi hutoa onyo wanapoona hatari. Vivyo hivyo, tunawaonya wengine wakati unaofaa, kwa mfano, ndugu “akijikwaa katika kosa fulani kabla ya yeye kulijua.” (Wagalatia 6:1) Na kupitia kazi yetu ya kuhubiri, tunawaonya watu kuhusu “siku ya Yehova” inayokaribia kwa kasi. (Sefania 1:​14) Katika mfano mwingine, Ndugu Lett alieleza kwamba kama vile ndege ambao huhama kutoka mahali pamoja hadi pengine wanavyolazimika kupaa juu ya milima mirefu, sisi pia tunashinda magumu ambayo yanaonekana kuwa makubwa kwa msaada wa Yehova.​—Mathayo 17:20.

Umalizio. Wanafunzi walipokea diploma zao, na baadaye mmoja wa wanafunzi akasoma barua ya shukrani kwa niaba ya darasa. Kwa kumalizia, Ndugu Herd alilinganisha kuingiza mawazo ya Yehova ndani ya moyo wetu na kazi ya kuunganisha vyuma vya reli ya garimoshi kwa kutumia misumari mikubwa. Lazima ugonge misumari hiyo mara kadhaa kwa nyundo ili kuhakikisha imezama kabisa ndani ya chuma cha reli. Vivyo hivyo, wanafunzi wanapaswa kuendelea kufikiria mambo ambayo wamejifunza katika shule ya Gileadi. Ndugu Herd alisema hivi, “Tumia wakati kugonga misumari hiyo iingie ndani kabisa ya moyo wako.” Kisha akaongezea hivi: “Fuata mawazo ya Mungu, nawe utakuwa baraka kwa wengine.”