Hamia kwenye habari

Kuchapisha Biblia Katika Lugha Zao za Asili

Kuchapisha Biblia Katika Lugha Zao za Asili

Mashahidi wa Yehova humpa yeyote anayetaka kusoma, Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

Ingawa mabilioni ya Biblia na tafsiri nyingi zimechapishwa na mashirika mbalimbali yanayotafsiri Biblia, umaskini na ubaguzi wa kidini umesababisha watu wengi wasipate Biblia katika lugha zao. Kwa sababu hiyo, Mashahidi wa Yehova wametafsiri Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika zaidi ya lugha 115.

Soma mifano ifuatayo:

  • Rwanda: Silvestre na Venantie walio na watoto wanne walisema hivi: “Sisi ni maskini sana, hivyo hatuwezi kumnunulia kila mtu katika familia yetu Biblia, lakini sasa kila mmoja wetu ana Biblia yake mwenyewe ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kinyarwanda. Nasi tunasoma Biblia kila siku tukiwa pamoja.”

    Kasisi mmoja wa kanisa la Kianglikana kutoka sehemu hiyo anasema hivi: “Hii ndiyo Biblia ninayoweza kuilewa. Ni nzuri kuliko Biblia nyingine ambazo nimewahi kusoma. Mashahidi wa Yehova wanawajali watu kwelikweli!”

  • Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo: Makanisa fulani yamekataa kuwauzia Mashahidi wa Yehova Biblia ya Kilingala ambayo ndiyo lugha inayozungumzwa sana huko Kongo.

    Basi haishangazi kwamba tangu kutolewa kwa Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kilingala, Mashahidi wa Yehova huko Kongo huisoma Biblia hiyo na kuwapa wengine. Isitoshe, watu wengi walisisimka Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilipotolewa katika kusanyiko moja la Mashahidi wa Yehova, hata polisi waliokuwepo katika uwanja huo wa kusanyiko walichukua Biblia zao.

  • Fiji: Huko Fiji Biblia ni ghali sana hivi kwamba hapo awali Mashahidi wa Yehova walikuwa wakitumia Biblia ya Kiingereza ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Hata hivyo katika mwaka 2009, wenyeji wa Fiji walipokea Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo (Agano Jipya) katika lugha yao.

    Mwanamume mmoja alivutia sana na jinsi Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilivyotafsiriwa kwa lugha rahisi hivi kwamba aliomba apewe Biblia yake mwenyewe. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wa eneo hilo walimweleza kwamba angehitaji kusubiri kwa mwezi mmoja hivi ili apate Biblia hiyo. Kwa sababu hakutaka kungoja, aliamua kusafiri zaidi ya kilometa 35 ili akutane na Shahidi mwingine ambaye alikuwa tayari kumpa Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Mwanamume huyo alisema hivi: “Tafsiri hii ya Biblia ni nzuri zaidi kuliko ile ambayo tumezoea. Imetumia lugha inayoeleweka kwa urahisi.”

  • Malawi: Davide alipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, washiriki wa kanisa la Kibaptisti walienda nyumbani kwake na kuchukua Biblia waliyokuwa wamempa. Hivyo, Davide hakuamini macho yake alipopokea Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kichichewa!

    Kwa kuwa Biblia ni ghali sana huko Malawi, Davide hakujua angetoa wapi Biblia nyingine. Lakini alipopewa Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, alisema: “Sasa nina Biblia nzuri zaidi kuliko ile niliyokuwa nayo!”

Zaidi ya miaka 60 iliyopita, sehemu ya kwanza ya Biblia ya Kiingereza ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilipotolewa katika kusanyiko moja huko New York City wasikilizaji walitiwa moyo hivi: “Isomeni. Jifunzeni . . . Mwape wengine.” Ili kutimiza kusudi hilo Mashahidi wa Yehova wamechapisha zaidi ya nakala milioni 175 za Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Sasa unaweza kusoma Biblia kwenye mtandao katika lugha 50 hivi.