Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

BIBLIA INABADILISHA MAISHA YA WATU

Nilijifunza Kujiheshimia na Kuheshimia Wanawake

Nilijifunza Kujiheshimia na Kuheshimia Wanawake
  • ALIZALIWA: 1960

  • NCHI : UFARANSA

  • ALIKUWA: MUTUMWA WA DAWA ZA KULEWESHA MWENYE JEURI, NA HAKUHESHIMIA WANAWAKE

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilizaliwa katika muji wa Mulhouse, kaskazini-mashariki mwa inchi ya Ufaransa, katika eneo la watu wa hali ya chini wenye kufanya kazi za mikono. Eneo hilo lilijulikana sana kwa sababu ya jeuri. Mambo ninakumbuka juu ya utoto wangu ni mabishano makubwa kati ya familia mbalimbali za eneo letu. Katika familia yetu, wanawake walizarauliwa na wanaume hawakuzoea kuwauliza mawazo yao. Nilifundishwa kama nafasi ya mwanamuke ni kwenye mafiga, ili kuhangaikia wanaume na watoto.

Maisha yangu ya utoto yalikuwa magumu. Wakati nilikuwa na miaka 10, baba yangu alikufa kwa sababu ya ulevi wake. Miaka tano kisha hapo, mumoja kati ya ndugu zangu wakubwa alijiua. Mwaka uleule, nilijionea mutu anauawa katika pigano la watu wa familia yetu na jambo hilo lilinihuzunisha sana. Watu wa familia yetu walinifundisha namna ya kutumikisha visu na bunduki na kupigana wakati wowote hali iliomba vile. Kwa sababu nilikuwa kijana mwenye kuvurugika akili, nilianza kujichanja mwili wote na kunywa pombe.

Wakati nilikuwa na miaka 16, nilikuwa ninakunywa kati ya chupa 10 na 15 za pombe kila siku, na bila kukawia nilianza kutumia dawa za kulewesha. Ili kuuza dawa za kulewesha na pombe, nilikuwa ninauzisha vyuma vya zamani na kuiba. Wakati nilikuwa na miaka 17, nilikuwa nilisha kuonja gereza. Kwa ujumla, nilihukumiwa mara 18 kwa sababu ya wizi na jeuri.

Wakati nilikuwa na miaka 20 hivi, hali yangu ikaharibika sana. Nilivuta miti 20 ya marijuana kila siku na kutumikisha bangi yenye kuitwa heroini na vitu vingine vyenye vilikatazwa na sheria. Mara nyingi, nilikuwa karibu kufa kwa sababu ya kupitisha kipimo. Nilianza kuuzisha dawa za kulewesha, kwa hiyo, kila wakati nilikuwa na visu na bunduki. Siku moja, nilijaribu kupiga mwanaume mumoja risasi, lakini jambo la kufurahisha ni kwamba risasi iliponyoka na kupita kwenye chuma cha kufungia mushipi wake! Wakati nilikuwa na miaka 24, mama yangu alikufa, na hasira yangu iliongezeka. Watu wenye kutembea kwa miguu waliogopa sana na kuenda ngambo ingine ya barabara wakati walikuwa wanaona ninakaribia. Kwa sababu ya kupigana, mara nyingi nilipitisha mwisho wa juma kwenye biro ya polisi ao kwenye hospitali ili wanganga wanishone vidonda.

Wakati nilikuwa na miaka 28, nilioa. Kama vile unaweza kuwazia, sikukuwa ninatendea bibi yangu kwa heshima. Nilikuwa ninamutukana na kumupiga. Hatukufanya jambo lolote pamoja kama bibi na bwana. Niliwaza kama ilitosha tu kumujaza vitu vya mapambo vya wizi. Kisha, jambo fulani lenye sikuwazia lilitokea. Bibi yangu alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Kisha kujifunza kwa mara ya kwanza, aliacha kuvuta tumbako, alikataa kukamata tena feza za wizi, na alinirudishia vitu vyake vya mapambo vyenye nilikuwa nimemupatia. Nilikasirika. Nilipinga funzo lake la Biblia na nilikuwa ninamupulizia moshi wa tumbako kwenye sura. Tena, nilikuwa ninamuzarau mbele ya majirani wetu.

Siku moja usiku, katika hali ya ulevi, niliwasha moto kwenye nyumba yetu bila kujua. Bibi yangu aliniokoa pamoja na mutoto wetu mwanamuke wa miaka tano. Wakati ulevi uliisha, zamiri yangu ilinihangaisha sana. Ndani ya moyo wangu, nilijisikia kuwa Mungu hawezi kunisamehe hata siku moja. Nilikumbuka kama padri alisema wakati fulani kuwa watu wabaya wanaendaka katika moto wa mateso. Hata munganga wangu wa akili aliniambia hivi: “Hakuna tena tumaini! Hauwezi tena kubadilika.”

BIBLIA ILIBADILISHA MAISHA YANGU:

Kisha kuokoka katika moto huo, tulihamia kwa wazazi wa bibi yangu. Wakati Mashahidi walikuja kutembelea bibi yangu, niliwauliza, “Mungu anaweza kunisamehe zambi zangu zote?” Walinionyesha andiko la 1 Wakorintho 6:9-11 katika Biblia. Andiko hilo linaonyesha matendo mbalimbali yenye Mungu anachukia, lakini linaongeza hivi: ‘Na bado wengine wenu mulikuwa hivyo.’ Maneno hayo yalinihakikishia kama ingewezekana nibadilike. Kisha Mashahidi walinihakikishia kama Mungu alinipenda kwa kunionyesha andiko la 1 Yohana 4:8. Kwa sababu nilitiwa moyo, niliomba Mashahidi hao wajifunze na mimi Biblia mara mbili kwa juma, na nilianza kuenda kwenye mikutano yao ya Kikristo. Nilisali tena na tena kwa Yehova.

Mwezi moja kisha kuanza kujifunza, niliamua kuacha dawa za kulewesha na pombe. Bila kukawia, nilisikia kama vita ilianza katika mwili wangu! Nilihangaishwa na ndoto za mubaya, maumivu ya kichwa, ya misuli (muscles), na mambo mengine yenye kutokea kisha mutu kuachana na dawa za kulewesha na pombe. Lakini, wakati uleule, nilijisikia sawa vile Yehova alikuwa ananikamata mukono na kunitia nguvu. Nilijisikia kama mutume Paulo. Juu ya musaada wenye Mungu alimupatia, Paulo aliandika hivi: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.” (Wafilipi 4:13) Kisha wakati fulani, niliweza kuacha kuvuta tumbako.—2 Wakorintho 7:1.

Biblia imenisaidia kuongoza maisha yangu na pia kufanya familia yangu ikuwe ya muzuri. Namna ya kutendea bibi yangu ilibadilika. Nilianza kumuonyesha heshima sana na kumuambia “tafazali” na “aksanti.” Tena, nilianza kuwa baba wa kweli kwa mutoto wangu mwanamuke. Kisha kujifunza Biblia kwa mwaka moja, nilijitoa kwa Yehova na kubatizwa, kwa kufuata mufano wa bibi yangu.

FAIDA YENYE NIMEPATA:

Niko hakika kama kanuni za Biblia zimeokoa maisha yangu. Hata watu wa familia yetu wenye hawako Mashahidi wanaona kama pengine ningekufa zamani kwa sababu ya kutumia dawa za kulewesha ao ningeuawa katika kupigana.

Mafundisho ya Biblia yenye kueleza daraka la bwana na la baba yamebadilisha kabisa maisha ya familia yangu. (Waefeso 5:25; 6:4) Tulianza kufanya mambo pamoja kama familia. Leo, simuone tena bibi yangu kuwa mutu wa mafiga tu. Yeye ni muhubiri wa wakati wote na ninamuunga mukono kwa furaha katika kazi hiyo ya kuhubiri. Na yeye anafurahia kuniunga mukono kutimiza kazi yangu ya muzee wa kutaniko.

Upendo wa Yehova na rehema yake vimegusa kabisa maisha yangu. Ninatamani sana kuelezea sifa zake watu wenye kuonwa kuwa hawawezi kubadilika tena, kwa sababu watu wengi waliniona pia vile. Ninajua kama Biblia iko na uwezo wa kusaidia mutu yeyote akuwe na maisha safi na yenye kusudi. Biblia imenifundisha kupenda watu wengine na kuwaheshimia, wanaume na wanawake, na pia imeniwezesha kujiheshimia mimi mwenyewe.