Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Pata Kimbilio Katika Jina la Yehova’

‘Pata Kimbilio Katika Jina la Yehova’

‘Pata Kimbilio Katika Jina la Yehova’

“Nami nitaacha wabaki . . . watu wanyenyekevu na wa hali ya chini, nao watapata kimbilio katika jina la Yehova.”—SEF. 3:12.

1, 2. Ni dhoruba gani ya mfano ambayo itawapata wanadamu hivi karibuni?

 JE, UMEWAHI kusimama chini ya daraja ili kujificha dhoruba au mvua ya mawe? Daraja linaweza kukulinda kutokana na dhoruba au mvua ya mawe, lakini huenda lisiweze kukulinda inavyofaa wakati wa kimbunga au tufani.

2 Kuna dhoruba ya aina tofauti inayokaribia, dhoruba ambayo inatisha kuangamiza wanadamu wote. Ni “siku ya dhoruba” ya mfano. ‘Siku hiyo kuu ya Yehova’ itakuja juu ya wanadamu wote. Hata hivyo, tunaweza kupata kimbilio tunalohitaji. (Soma Sefania 1:14-18.) Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani wakati wa “siku ya ghadhabu ya Yehova” ambayo itaanza hivi karibuni?

Siku za Dhoruba Katika Nyakati za Biblia

3. Ni ‘dhoruba gani yenye mngurumo’ ambayo ilikuja juu ya ufalme wa makabila kumi ya Israeli?

3 Siku ya Yehova itaanza na kuharibiwa kwa mifumo yote ya dini ya uwongo duniani. Ili tujue jinsi tunavyoweza kupata kimbilio, tunaweza kuchunguza historia ya watu wa kale wa Mungu. Isaya, ambaye aliishi katika karne ya nane K.W.K., alifananisha hukumu ya Yehova juu ya ufalme wenye kuasi imani wa makabila kumi ya Israeli na “dhoruba yenye mngurumo” ambayo watu hawangeweza kuizuia. (Soma Isaya 28:1, 2.) Unabii huo ulitimizwa mwaka wa 740 K.W.K. wakati Ashuru ilipovamia nchi ya makabila hayo, na Efraimu lilikuwa ndilo kabila kuu zaidi kati ya makabila hayo kumi.

4. “Siku kuu ya Yehova” ilikuja juu ya Yerusalemu jinsi gani mwaka wa 607 K.W.K.?

4 Katika mwaka wa 607 K.W.K., hukumu juu ya taifa la Israeli ambalo lilikosa uaminifu ilifuatwa na “siku kuu ya Yehova” juu ya Yerusalemu na ufalme wa Yuda. Jambo hilo lilitukia kwa sababu watu wa Yuda walikuwa pia wameasi imani. Wababiloni wakiongozwa na Nebukadneza walitisha kushambulia Yuda na jiji lake kuu, Yerusalemu. Wayudea walitafuta msaada kutoka kwa “kimbilio la uwongo,” yaani, walifanya mapatano ya kisiasa pamoja na Misri. Ingawa hivyo, kama mvua ya mawe yenye kuharibu, Wababiloni walifagilia mbali “kimbilio” hilo.—Isa. 28:14, 17.

5. Ni nini kitakachowapata watu wa Mungu wakiwa kikundi wakati wa uharibifu wa dini yote ya uwongo?

5 Siku kuu ya Yehova ambayo ilikuja juu ya Yerusalemu ilionyesha kimbele hukumu ambayo itakuja juu ya dini zinazodai kuwa za Kikristo ambazo zimeasi imani katika wakati wetu. Zaidi ya hilo, sehemu inayobaki ya “Babiloni Mkubwa,” milki ya dini ya uwongo ulimwenguni, itaharibiwa. Kisha, sehemu zinazobaki za mfumo mwovu wa mambo wa Shetani zitaangamizwa. Hata hivyo, watu wa Mungu wakiwa kikundi wataokoka kwa sababu wanapata kimbilio katika Yehova.—Ufu. 7:14; 18:2, 8; 19:19-21.

Kimbilio la Kiroho na Kimwili

6. Watu wa Yehova wanaweza kupata kimbilio jinsi gani?

6 Watu wa Mungu wanaweza kupata kimbilio jinsi gani hata sasa wakati huu wa mwisho? Tunapata kimbilio la kiroho kwa kusali na ‘kulifikiria jina la Mungu’ na kumtumikia kwa bidii. (Soma Malaki 3:16-18.) Hata hivyo, tunajua kwamba tunahitaji kufanya mengi zaidi kuliko kulifikiria tu jina lake. Tunasoma hivi: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.” (Rom. 10:13) Kuna uhusiano kati ya kuliitia jina la Yehova na kuokolewa naye. Na watu wengi wenye mioyo minyoofu wanaweza kuona tofauti kati ya wanadamu ambao hawamtumikii Yehova na Wakristo wa kweli, ambao kwa woga na heshima ‘wanalifikiria jina lake’ na kumtumikia wakiwa Mashahidi wake.

7, 8. Wakristo wa karne ya kwanza waliokolewa jinsi gani kimwili, na hilo linalingana na nini leo?

7 Hata hivyo, wokovu wetu unatia ndani mengi zaidi ya kupata kimbilio la kiroho. Watu wa Mungu wameahidiwa pia wokovu wa kimwili. Tunaona hilo tunapochunguza mambo yaliyotukia mwaka wa 66 W.K. baada ya jeshi la Roma kushambulia Yerusalemu likiongozwa na Sesho Galo. Yesu alikuwa ametabiri kwamba siku za dhiki hiyo ‘zingefupishwa.’ (Mt. 24:15, 16, 21, 22) Hilo lilitokea wakati wanajeshi wa Roma walipoacha kuzingira jiji na kuondoka kwa ghafula, na hivyo kuruhusu ‘miili’ fulani, yaani, Wakristo wa kweli ‘waokolewe.’ Wakristo hao walifanikiwa kukimbia kutoka katika jiji hilo na eneo la karibu. Wengine wao walivuka Yordani na kukimbilia kwenye milima iliyo upande wa mashariki wa mto huo.

8 Tunaweza kulinganisha Wakristo hao na watu wa Mungu leo. Zamani, Wakristo wa karne ya kwanza walitafuta kimbilio, na watumishi wa Mungu leo watafanya hivyo pia. Hata hivyo, mara hii hawatahitaji kukimbilia kwenye eneo fulani, kwa kuwa Wakristo wa kweli wanapatikana duniani pote. Lakini bado, wakiwa kikundi, Wakristo hao “waliochaguliwa” na waandamani wao washikamanifu wataokoka kimwili kwa kupata kimbilio katika Yehova na tengenezo lake ambalo ni kama mlima wakati dini zinazodai kuwa za Kikristo ambazo zimeasi imani zitakapoharibiwa.

9. Ni nani ambao wamejaribu kufanya jina la Yehova lisahauliwe? Toa mfano.

9 Kwa upande mwingine, dini zinazodai kuwa za Kikristo zinastahili kuharibiwa kwa sababu zimewafanya watu wanaoenda kanisani wakose ujuzi wa mambo ya kiroho na kwa sababu zinalichukia jina la Mungu waziwazi. Katika Enzi za Kati, jina la kibinafsi la Mungu lilijulikana sana huko Ulaya. Jina hilo, ambalo linawakilishwa na herufi nne za Kiebrania zinazoitwa Tetragramatoni ambazo kwa kawaida zinatafsiriwa YHWH (au JHVH), liliandikwa kwenye sarafu, kwenye ukuta wa mbele wa nyumba nyingi, katika Biblia na vitabu vingi, na hata ndani ya makanisa fulani ya Kikatoliki na Kiprotestanti. Hata hivyo, hivi karibuni kumekuwa na mwelekeo wa kuondoa jina la Mungu katika tafsiri za Biblia na kutolitumia kwa njia nyingine. Jambo moja linaloonyesha hivyo ni Barua iliyotumwa kwa Mikutano ya Maaskofu kuhusu ‘Jina la Mungu,’ iliyoandikwa Juni 29, 2008, (29/6/2008), na Baraza la Usimamizi la Kanisa Katoliki. Katika barua hiyo, Kanisa Katoliki liliagiza kwamba tafsiri zote za Tetragramatoni ziondolewe na badala yake watumie neno “Bwana.” Vatikani iliagiza kwamba jina la kibinafsi la Mungu halipaswi kutumiwa au kutamkwa katika nyimbo na sala wakati wa ibada ya Wakatoliki. Na pia, viongozi wa dini nyingine zinazodai kuwa za Kikristo na dini zisizo za Kikristo wamewaficha mamilioni na mamilioni ya waabudu jina la Mungu wa kweli.

Wale Wanaolitakasa Jina la Mungu Wanalindwa

10. Jina la Mungu linaheshimiwa jinsi gani leo?

10 Tofauti kabisa na jinsi dini nyingine zinavyotenda, Mashahidi wa Yehova wanaliheshimu na kulitukuza jina la Mungu. Wanalitakasa kwa kulitumia kwa njia ya heshima. Yehova anapendezwa na wale wanaomtegemea, naye anakuwa chochote kinachohitajiwa ili awabariki na kuwalinda watu wake. “Hutambua wale wanaotafuta kimbilio kwake.”—Nah. 1:7; Mdo. 15:14.

11, 12. Ni nani ambao waliunga mkono jina la Yehova katika taifa la kale la Yuda, na ni nani ambao wamefanya hivyo siku hizi?

11 Ingawa watu wengi katika taifa la kale la Yuda walikuwa wameasi imani, kuna wengine ambao ‘walipata kimbilio katika jina la Yehova.’ (Soma Sefania 3:12, 13.) Ndiyo, Mungu alipoadhibu taifa la Yuda lililokosa imani kwa kuruhusu Wababiloni washinde nchi hiyo na kuwapeleka watu wake utekwani, watu fulani, kama vile Yeremia, Baruku, na Ebed-meleki, walilindwa. Walikuwa wameishi “katikati” ya taifa lililoasi imani. Wengine waliendelea kuwa waaminifu utekwani. Katika mwaka wa 539 K.W.K., taifa la Babiloni lilishindwa na Wamedi na Waajemi wakiongozwa na Koreshi. Baada ya muda mfupi, Koreshi alitoa agizo la kuruhusu mabaki ya Wayahudi warudi katika nchi yao.

12 Kuhusu wale ambao wangefurahia kurudishwa kwa ibada ya kweli, Sefania alitabiri kwamba Yehova angewaokoa na kushangilia juu yao. (Soma Sefania 3:14-17.) Hilo limethibitika kuwa kweli katika nyakati zetu pia. Baada ya Ufalme wa Mungu kusimamishwa mbinguni, Yehova aliwakomboa mabaki ya watiwa-mafuta waaminifu kutoka katika utekwa wa kiroho wa Babiloni Mkubwa. Na anaendelea kushangilia juu yao mpaka leo.

13. Watu kutoka katika mataifa yote wanafurahia uhuru gani?

13 Wale walio na tumaini la kuishi milele duniani wametoka pia katika Babiloni Mkubwa na wanafurahia uhuru wa kiroho kutokana na mafundisho ya uwongo ya kidini. (Ufu. 18:4) Hivyo, andiko la Sefania 2:3 linatimizwa kwa njia kubwa zaidi katika siku zetu: “Mtafuteni Yehova, ninyi nyote mlio wapole wa dunia.” Watu wapole kutoka katika mataifa yote, iwe wana tumaini la kuishi mbinguni au duniani, sasa wanapata kimbilio katika jina la Yehova.

Jina la Mungu Si Hirizi

14, 15. (a) Watu fulani wametumia nini kama hirizi? (b) Ni nini ambacho hakipaswi kutumiwa kama kitu cha kujilinda kimuujiza?

14 Waisraeli fulani waliona hekalu kuwa kama hirizi ambayo ingewalinda kutokana na maadui. (Yer. 7:1-4) Mwanzoni, Waisraeli waliona sanduku la agano kuwa kama hirizi ambayo ingewalinda katika vita. (1 Sam. 4:3, 10, 11) Konstantino Mkuu alichora kwenye ngao za askari-jeshi wake herufi khi na rho za Kigiriki, ambazo ni herufi mbili za kwanza za jina “Kristo” katika Kigiriki, akitumaini kwamba zingewalinda askari-jeshi wake vitani. Inasemekana kwamba Mfalme Gustav Adolph wa Pili wa Sweden, ambaye alipigana katika vile Vita vya Miaka 30, alivaa vazi la kivita ambalo limeonyeshwa kwenye ukurasa wa 7. Ona kwamba jina Iehova limeandikwa waziwazi kwenye vazi hilo.

15 Watu fulani wa Mungu ambao wameshambuliwa na roho waovu wamepata kimbilio katika Yehova kwa kuliitia jina lake kwa sauti. Ingawa hivyo, kitu kilicho na jina la Mungu hakipaswi kuonwa kuwa hirizi na kutumiwa kila siku kana kwamba kina nguvu za kumlinda mtu kimuujiza. Kupata kimbilio katika jina la Yehova hakumaanishi hivyo.

Jinsi Tunavyopata Kimbilio Leo

16. Tunaweza kupata jinsi gani kimbilio la kiroho leo?

16 Tunapata kimbilio leo katika usalama wa kiroho unaofurahiwa na watu wa Mungu wakiwa kikundi. (Zab. 91:1) Kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” na wazee katika makutaniko, tunaonywa kuhusu mazoea ya kilimwengu ambayo yanaweza kuhatarisha usalama huo. (Mt. 24:45-47; Isa. 32:1, 2) Fikiria jinsi ambavyo tumeonywa mara nyingi kuhusu kupenda vitu vya kimwili, na utafakari jinsi ambavyo maonyo hayo yametulinda ili tusipatwe na msiba wa kiroho. Namna gani kuhusu hatari ya kusitawisha mtazamo wa kutojali, ambao unaweza kufanya tuwe wasiotenda katika utumishi wa Yehova? Neno la Mungu linasema hivi: “Kutojali kwa wajinga kutawaangamiza wao. Kwa habari yake mtu anayenisikiliza, yeye atakaa salama wala hatasumbuliwa na hofu ya msiba.” (Met. 1:32, 33) Kujitahidi kuendelea kuwa safi kiadili kunatusaidia pia kudumisha usalama wetu wa kiroho.

17, 18. Ni nini kinachowasaidia mamilioni ya watu kupata kimbilio katika jina la Yehova leo?

17 Pia, fikiria jinsi mtumwa mwaminifu anavyotutia moyo tufuate amri ya Yesu ya kuhubiri habari njema ya Ufalme katika dunia yote inayokaliwa. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Sefania alitaja badiliko ambalo lingewasaidia watu kupata kimbilio katika jina la Mungu. Tunasoma hivi: “Ndipo nitakapobadilisha lugha ya vikundi vya watu na kuwapa lugha safi, ili wote waliitie jina la Yehova, wamtumikie bega kwa bega.”—Sef. 3:9.

18 Lugha hiyo safi ni nini? Lugha hiyo safi ni kweli kumhusu Yehova Mungu na makusudi yake ambayo yameandikwa katika Neno lake lililoongozwa na roho yake. Kwa njia fulani, unatumia lugha hiyo unapowasaidia wengine kupata ujuzi sahihi kuhusu Ufalme wa Mungu na jinsi Ufalme huo utakavyolitakasa jina lake, unapokazia kutetewa kwa enzi kuu ya Mungu, na unapozungumza kwa furaha kuhusu baraka za milele ambazo wanadamu waaminifu watafurahia. Kwa kuwa wengi wanazungumza lugha hiyo ya mfano, hesabu inayoongezeka ya watu ‘wanaliitia jina la Yehova’ na ‘kumtumikia bega kwa bega.’ Ndiyo, mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanapata sasa kimbilio katika Yehova.—Zab. 1:1, 3.

19, 20. “Kimbilio la uwongo” lilishindwa jinsi gani kuwalinda watu waliolitegemea katika nyakati za Biblia?

19 Watu katika ulimwengu wanalazimika kupambana na matatizo ambayo yanaonekana hayawezi kutatuliwa. Kwa kuwa wanahangaika sana kutatua matatizo yao, wengi wanatafuta msaada kutoka kwa wanadamu wasio wakamilifu. Au wanatazamia kupata suluhisho kutoka kwa mashirika ya kisiasa, kama vile ambavyo nyakati nyingine taifa la kale la Israeli lilitafuta msaada kutoka kwa mataifa jirani kwa kufanya mapatano nayo. Hata hivyo, unajua kwamba kufanya hivyo hakukuwasaidia Waisraeli. Leo pia, matatizo ya wanadamu hayatatatuliwa kabisa na taifa lolote la kisiasa wala na shirika la Umoja wa Mataifa. Basi, kwa nini mtu afikiri kwamba mashirika na mapatano ya kisiasa ni kimbilio? Biblia inatabiri kwamba mashirika na mapatano hayo ni “kimbilio la uwongo.” Kwa kweli, unaweza kuyaona hivyo kwa sababu watu wote wanaoyatumaini watakatishwa tamaa kabisa.—Soma Isaya 28:15, 17.

20 Hivi karibuni siku ya Yehova ambayo ni kama dhoruba ya mawe itakuja ghafula juu ya dunia. Mbinu za wanadamu hazitaweza kuwalinda; wala majengo ya kujilinda kutokana na silaha za nyuklia wala utajiri hautawalinda. Andiko la Isaya 28:17 linasema hivi: “Mvua ya mawe itafagilia mbali lile kimbilio la uwongo, na maji yatafurika mahali pa maficho.”

21. Tunaweza kupata faida gani tukitii andiko la mwaka wa 2011?

21 Hivi sasa na pia wakati huo ujao, watu wa Mungu watapata usalama wa kweli katika Mungu wao, Yehova. Jina la Sefania, ambalo linamaanisha “Yehova Ameficha,” linaonyesha chanzo hicho cha kweli cha mahali pa kujificha. Kwa kufaa, andiko letu la mwaka wa 2011 ni shauri hili lenye hekima: ‘Pata kimbilio katika jina la Yehova.’ (Sef. 3:12) Hata sasa tunaweza na tunapaswa kupata kimbilio katika jina la Yehova na kumtegemea kabisa. (Zab. 9:10) Acheni kila siku tukumbuke uhakikisho huu uliongozwa na roho ya Mungu: “Jina la Yehova ni mnara wenye nguvu. Mwadilifu hukimbilia humo na kupewa ulinzi.”—Met. 18:10.

Je, Unakumbuka?

• Tunaweza kupata kimbilio katika jina la Yehova jinsi gani sasa?

• Kwa nini hatupaswi kutegemea “kimbilio la uwongo”?

• Ni kimbilio gani ambalo tumehakikishiwa wakati ujao?

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Andiko la mwaka wa 2011 ni: ‘Pata kimbilio katika jina la Yehova.’—Sefania 3:12.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 7]

Thüringer Landesmuseum Heidecksburg Rudolstadt, Waffensammlung “Schwarzburger Zeughaus”