Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Unaweza Kuona Jina la Mungu Katika Bonde Hili

Unaweza Kuona Jina la Mungu Katika Bonde Hili

Unaweza Kuona Jina la Mungu Katika Bonde Hili

ST. MORITZ. Je, umewahi kusikia jina hilo? Labda umewahi kulisikia kwa sababu ni eneo maarufu sana duniani linalotembelewa na watalii katika Bonde la Engadine, huko Uswisi. St. Moritz ni eneo ambalo kwa miaka mingi limewavutia watu kwenye bonde hilo lenye kuvutia sana lililo katikati ya milima iliyofunikwa na theluji ya Alps kwenye pembe ya kusini-mashariki ya Uswisi karibu na mpaka wa Italia. Pia, katika eneo hilo kuna Mbuga ya Kitaifa ya Wanyama ya Uswisi, ambayo ina umaridadi wa kiasili na wanyama na mimea mbalimbali ambayo inamletea sifa Muumba wetu Mkuu, Yehova. (Zab. 148:7-10) Na ndivyo ilivyo pia na desturi fulani ambayo ilianza katikati ya karne ya 17.

Huenda ukavutiwa na jambo fulani lisilo la kawaida kwenye nyumba nyingi katika bonde hilo. Ni jambo la kawaida kuona jina la Mungu likiwa limeandikwa upande wa mbele wa nyumba, kwa mfano, juu ya mlango wa mbele wa nyumba. Karne nyingi zilizopita, kulikuwa na desturi ya kurembesha sehemu ya nje ya nyumba kwa maandishi, labda kwa kuandika kwa rangi, kukwaruza kwenye ukuta, au kuchonga maandishi kwenye mawe. Hapa chini unaweza kuona picha ya nyumba katika kijiji cha Bever. Maandishi yaliyo kwenye ukuta yanatafsiriwa hivi: “Katika mwaka wa 1715. Yehova ndiye mwanzo, na Yehova ndiye mwisho. Mambo yote yanawezekana kwa Mungu, na hakuna jambo asiloweza kufanya.” Ndiyo, maandishi hayo ya zamani yanatumia jina la kibinafsi la Mungu mara mbili.

Katika kijiji cha Madulain, unaweza kuona maandishi ya kale hata zaidi. Maandishi hayo yanasema: “Zaburi 127. Yehova asipoijenga nyumba, ni bure kwamba wajenzi wake wameifanyia kazi ngumu. Lucius Rumedius. Katika mwaka wa 1654.”

Kwa nini jina la Mungu limeandikwa waziwazi hivyo katika bonde hilo? Katika kipindi cha Marekebisho Makubwa ya Kidini, Biblia ilichapishwa katika Kiromanshi, lugha yenye asili ya Kilatini inayozungumzwa huko Engadine. Kwa kweli, hicho ndicho kilichokuwa kitabu cha kwanza kutafsiriwa katika lugha hiyo. Wakichochewa na mambo waliyosoma katika Neno la Mungu, wakaaji wengi wa eneo hilo waliandika kwenye ukuta wa nje wa nyumba zao majina yao na pia maandishi kutoka katika Biblia yaliyokuwa na jina la kibinafsi la Mungu.

Ndiyo, mpaka leo hii, maandishi hayo bado yanatangaza jina la Yehova na kumletea sifa, karne nyingi baada ya kuandikwa kwenye nyumba hizo. Wageni na wakaaji katika bonde hilo wanakaribishwa kujifunza mengi kumhusu Mungu mzuri ajabu, Yehova, kwa kutembelea jengo lingine lililo na jina lake—Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova huko Bever.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 7]

© Stähli Rolf A/age fotostock