Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Uwe Hodari Yehova Yupo Pamoja Nawe!

Uwe Hodari Yehova Yupo Pamoja Nawe!

“Uwe hodari na mwenye nguvu.  . . . Yehova Mungu wako yupo pamoja nawe.”​—YOS. 1:9.

1, 2. (a) Ni sifa gani ambazo zitatusaidia kushinda majaribu? (b) Imani ni nini? Toa mufano.

 KAZI ya Yehova inatuletea furaha. Hata hivyo, tunapambana na magumu ambayo kwa kawaida yanawapata wanadamu wote, na tunaweza pia ‘kuteseka kwa ajili ya uadilifu [haki].’ (1 Pet. 3:14; 5:8, 9; 1 Kor. 10:13) Ili kushinda, tuna lazima ya imani na uhodari.

2 Imani ni nini? Mutume Paulo aliandika hivi: ‘Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, usibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekane.’ (Ebr. 11:1) Katika tafsiri moja, andiko hilo linasema hivi: ‘Imani ni cheti cha kuriti mambo tunayotumainia. Imani ni kuwa hakika na mambo ambayo hatuweze kuona.’ Tunapopewa cheti cha kuriti, cheti hicho kinatupa uhakika kwamba kitu hicho ni chetu. Kwa kuwa tunaamini kwamba siku zote Mungu anatimiza ahadi zake, ni kama vile tuna cheti kinachoonyesha kwamba tumepewa kitu fulani chenye samani. Imani yetu inatufanya tuwe hakika kwamba tutaona utimizo wa ahadi zote zilizo katika Biblia, na tuko hakika kwamba mambo yote ambayo Biblia inasema ni kweli, hata yale ambayo hatuweze kuona.

3, 4. (a) Uhodari ni nini? (b) Ni njia moja gani inayoweza kutusaidia tuwe na imani na uhodari zaidi?

3 Kitabu kimoja kinafasiria uhodari kuwa ‘ni nguvu za kiroho, kiakili, na kuamini kabisa kile unachofanya kuwa ni haki, sifa hizo zinamusukuma mutu kusema ao kufanya jambo fulani bila kuogopa hata ikiwa kuna vizuizi na hatari fulani.’ Ikiwa sisi tuko hodari, tutakuwa wenye nguvu, wenye ujasiri na wasioogopa.​—Mk. 6:49, 50; 2 Tim. 1:7.

4 Imani na uhodari ni sifa zenye kuvutia. Lakini, namna gani ikiwa tunatambua kama tuna lazima ya kuwa na imani na uhodari zaidi? Katika Biblia kuna mifano mingi ya watu walioonyesha sifa hizo. Kwa hiyo, njia moja inayoweza kutusaidia kuwa na imani na uhodari zaidi ni kuchunguza mifano hiyo.

YEHOVA ALIKUWA PAMOJA NA YOSHUA

5. Yoshua alihitaji nini ili awaongoze watu wa Mungu vizuri?

5 Acheni tuzungumuzie mambo yaliyotokea miaka 3 500 hivi iliyopita. Kwa mukono wake wa nguvu Yehova aliwakomboa Waisraeli kutoka katika utumwa wa Misri. Nabii Musa alikuwa kiongozi wao kwa miaka 40. Sasa Musa ana miaka 120, anapanda kwenye Mulima Nebo, anatazama Inchi ya Ahadi kwa mbali, na kisha anakufa hapo. Yoshua, mwanaume mwenye ‘kujaa roho ya hekima,’ ndiye anayekamata nafasi yake. (Kum. 34:1-9) Waisraeli wanakaribia kuchukua inchi ya Kanaani. Yoshua anahitaji kuwa na hekima kutoka kwa Mungu ili awaongoze vizuri. Tena atahitaji kuwa na imani katika Yehova na kuonyesha uhodari na nguvu.​—Kum. 31:22, 23.

6. (a) Andiko la Yoshua 23:6 linatuomba tuwe hodari ili kufanya nini? (b) Maandiko ya Matendo 4:18-20 na Matendo 5:29 yanatufundisha nini?

6 Yoshua alitenda kwa hekima, uhodari na imani muda wote ambao alikuwa akiyashinda mataifa ya Kanaani. Jambo hilo liliwatia kabisa Waisraeli moyo. Hata hivyo, Waisraeli hawakuhitaji tu kuwa hodari katika vita, lakini pia kuwa hodari ili kutii maagizo ya Yoshua. Katika hotuba yake ya mwisho mbele ya kufa, Yoshua alisema hivi: ‘Nanyi muwe hodari sana ili mushike na kufanya yote ambayo yameandikwa katika kitabu cha sheria ya Musa kwa kutogeuka kamwe kutoka ndani yake kwenda kuume wala kushoto.’ (Yos. 23:6) Sisi pia inatuomba kuwa hodari ili kumutii Yehova wakati wote. Kwa mufano, tunapaswa kuwa hodari wakati wanadamu wanatuomba tutende mambo ambayo Yehova anatukataza. (Soma Matendo 4:18-20; 5:29.) Ikiwa tunamutegemea Yehova katika sala, atatusaidia tuwe hodari.

NAMNA TUNAVYOWEZA KUFANIKISHA NJIA YETU

7. Yoshua alipaswa kufanya nini ili awe na uhodari na kufanikisha njia yake?

7 Tunapaswa kujifunza na kutumikisha mambo tunayojifunza katika Neno la Mungu ili tuwe na uhodari unaohitajiwa ili kufanya mapenzi ya Mungu. Yoshua alipokamata nafasi ya Musa, Yehova alimuambia hivi: ‘Uwe hodari na mwenye nguvu sana ili uangalie kufanya kulingana na sheria yote ambayo Musa mutumishi wangu alikuamuru.  . . . Kitabu hiki cha sheria kisiondoke katika kinywa chako, nawe ukisome kwa sauti ya chini muchana na usiku, upate kuangalia kufanya kulingana na yote ambayo yameandikwa ndani yake; kwa maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha utatenda kwa hekima.’ (Yos. 1:7, 8) Yoshua alifuata shauri hilo, na ‘alifanikisha njia yake.’ Ikiwa tunamuiga, tutakuwa na uhodari mwingi zaidi na tutafanikiwa katika kazi ya Mungu.

Andiko letu la mwaka wa 2013 ni: “Uwe hodari na mwenye nguvu. . . . Yehova Mungu wako yupo pamoja nawe.”​—Yoshua 1:9

8. Andiko la mwaka wa 2013 ni andiko gani, na unawaza maneno ya andiko hilo yatakusaidia namna gani?

8 Bila shaka, Yoshua alipata nguvu aliposikia tena maneno haya ya Yehova: “Uwe hodari na mwenye nguvu. Usitetemeke wala usiwe na hofu, kwa maana Yehova Mungu wako yupo pamoja nawe kila mahali unapoenda.” (Yos. 1:9) Yehova yupo pamoja nasi pia. Kwa hiyo, hata ikiwa tunapambana na majaribu ya namna gani, ‘tusitetemeke wala kuwa na hofu.’ Tutapendezwa zaidi sana na maneno haya: “Uwe hodari na mwenye nguvu.  . . . Yehova Mungu wako yupo pamoja nawe.” Maneno hayo ya Yoshua 1:9 yamechaguliwa kuwa andiko la mwaka wa 2013. Hakika andiko hilo na maneno na matendo ya watu wengine waliotenda kwa imani na uhodari yatatutia nguvu katika siku zinazokuja.

WALITENDA KWA UHODARI

9. Namna gani Rahabu alitenda kwa imani na uhodari?

9 Yoshua alipotuma wapelelezi wawili huko Kanaani, Rahabu aliyekuwa kahaba, aliwaficha na hakuonyesha maadui njia ambayo wapelelezi walifuata. Kwa kuwa alitenda kwa imani na uhodari, yeye na watu wa jamaa yake waliokolewa wakati muji wa Yeriko uliharibiwa. (Ebr. 11:30, 31; Yak. 2:25) Bila shaka, Rahabu aliacha maisha yake ya ukahaba ili amupendeze Yehova. Leo, watu wanaogeuka na kuwa Wakristo wametenda kwa imani, uhodari na wamejikaza kubadili maisha yao kama Rahabu ili wamupendeze Mungu.

10. Ni katika hali gani Ruthu alichukua musimamo kuhusu ibada safi, na alipata baraka gani?

10 Kisha kifo cha Yoshua, Ruthu Mumoabu alishikamana na ibada safi kwa uhodari. Bwana yake aliyekuwa amekufa alikuwa Muisraeli, kwa hiyo, inawezekana Ruthu alijua mambo fulani kuhusu Yehova. Mama-mukwe yake mujane aliyeitwa Naomi, aliamua kuondoka Moabu ili kurudi Bethlehemu. Walipokuwa njiani, Naomi alimusihi Ruthu arudi kwao, lakini Mumoabu huyo alijibu hivi: “Usiniombe nikuache, nigeuke nisifuatane nawe . . . Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu.” (Rut. 1:16) Ruthu alitenda kulingana na maneno yake. Baadaye, Boazi, mutu wa jamaa ya bwana ya Naomi, alimuoa Ruthu nao wakazaa mutoto aliyekuwa kambo ao tate ya Daudi na Yesu. Bila shaka, Yehova anabariki wale wanaotenda kwa imani na uhodari.​—Rut. 2:12; 4:17-22; Mt. 1:1-6.

WENGI WALIHATARISHA MAISHA YAO

11. Namna gani Yehoyada na Yehosheba walitenda kwa uhodari, na hilo lilitimiza nini?

11 Tunapata nguvu zaidi ya kutenda kwa uhodari na imani tunapoona kwamba Mungu yupo pamoja na wale wanaofanya mapenzi yake, na wanaotafuta kwanza faida za waamini wenzao. Kwa mufano, fikiria Kuhani Mukubwa Yehoyada na bibi yake Yehosheba. Kisha kifo cha Mufalme Ahazia, Athalia, mama yake, aliua wazao wa mufalme waliobaki na akachukua ufalme. Yehoyada na Yehosheba walihatarisha maisha yao kwa kumuokoa mutoto wa Ahazia aliyeitwa Yehoashi na kumuficha kwa miaka sita. Katika mwaka wa saba, Yehoyada alifanya mupango wa kumutangaza Yehoashi kuwa mufalme na kumuua Athalia. (2 Fal. 11:1-16) Baadaye, Yehoyada alimusaidia Mufalme Yehoashi kutengeneza hekalu. Na wakati Yehoyada alikufa, mwenye miaka 130, alizikwa pamoja na wafalme “kwa sababu alikuwa ametenda mema katika Israeli na kwa Mungu wa kweli na kwa nyumba Yake.” (2 Nya. 24:15, 16) Zaidi ya hayo, kwa kuwa Yehoyada na bibi yake walitenda kwa uhodari, hilo lilifanya kizazi cha kifalme kilindwe kuanzia Daudi mupaka Masiya.

12. Namna gani Ebed-meleki alitenda kwa uhodari?

12 Ebed-meleki, aliyekuwa towashi katika nyumba ya Mufalme Sedekia, alihatarisha maisha yake kwa ajili ya Yeremia. Mufalme alimutia Yeremia mikononi mwa wakubwa wa Yuda ambao walimusingizia kuwa anawachochea watu waasi, na wakamutupa katika tangi lenye matope ili akufe. (Yer. 38:4-6) Ebed-meleki alimuomba mufalme Sedekia amusaidie Yeremia. Kufanya hivyo kulihatarisha maisha yake kwa sababu Yeremia alichukiwa. Sedekia alikubali na akamupa Ebed-meleki wanaume 30 ili waende kumuokoa Yeremia. Kupitia Yeremia, Mungu alimuhakikishia Ebed-meleki kwamba ataokoka wakati Yerusalemu itashambuliwa na watu wa Babiloni. (Yer. 39:15-18) Mungu anawabariki watu wanaotenda kwa uhodari.

13. Namna gani Waebrania watatu walitenda kwa uhodari, na tunaweza kujifunza nini kutokana na mufano wao?

13 Miaka 600 hivi mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, watumishi wa Yehova watatu Waebrania walijionea waziwazi kwamba Mungu anawabariki watu hodari na wenye imani. Mufalme Nebukadneza aliwakusanya wakubwa wa Babiloni na kuwaomba waabudu sanamu kubwa ya zahabu. Mutu yeyote ambaye angekataa kuabudu sanamu hiyo, angetupwa katika tanuru ya moto. Waebrania hao watatu walimuambia Nebukadneza kwa heshima: ‘Mungu ambaye tunamutumikia anaweza kutuokoa. Yeye atatuokoa kutoka katika tanuru inayowaka moto na kutoka mukononi mwako, Ee mufalme. Lakini kama sivyo, ujue hivi, Ee mufalme, kwamba sisi hatuitumikie miungu yako, na sanamu ambayo umeisimamisha hatutaiabudu.’ (Dan. 3:16-18) Andiko la Danieli 3:19-30 linaonyesha waziwazi namna Waebrania hao watatu walivyookolewa kimuujiza. Hata ikiwa sisi hatutatupwa katika tanuru ya moto, tunapatwa na majaribu mbalimbali na tunaweza kuwa hakika kwamba Mungu atatubariki kwa sababu ya imani na uhodari wetu.

14. Kulingana na andiko la Danieli sura ya 6, namna gani Danieli alitenda kwa uhodari, na matokeo yalikuwa nini?

14 Danieli alionyesha uhodari na imani wakati maadui wake walitunga sheria fulani na kumuchochea Mufalme Darius aikubali; sheria hiyo ilisema hivi: ‘Mutu yeyote atakayetoa ombi kwa mungu yeyote au mwanadamu kwa siku 30 isipokuwa kwako, Ee mufalme, atupwe ndani ya shimo la simba.’ (Dan. 6:6-10) Danieli aliposikia tu kwamba Mufalme alikubali jambo hilo, ‘aliingia nyumbani mwake, kisha, huku madirisha yaliyo katika chumba chake cha dari yakiwa yamefunguliwa kwa ajili yake kuelekea Yerusalemu, alikuwa akipiga magoti na kusali mara tatu kwa siku na kutoa sifa mbele za Mungu wake, kama vile alivyokuwa akifanya kwa ukawaida kabla ya hayo.’ (Dan. 6:6-10) Nabii hodari Danieli alitupwa katika shimo la simba, lakini Yehova alimuokoa.​—Dan. 6:16-23.

15. (a) Akila na Priska walituachia mufano gani wa imani na uhodari? (b) Maneno ya Yesu yaliyo katika andiko la Yohana 13:34 yanamaanisha nini, na namna gani Wakristo wengi wameonyesha upendo kama huo?

15 Katika hali ambazo Biblia haitaje, Akila na Priska ‘walihatarisha shingo zao wenyewe kwa ajili ya nafsi ya Paulo.’ (Mdo. 18:2; Rom. 16:3, 4) Walitenda kwa uhodari kulingana na maneno haya ya Yesu: ‘Ninawapa ninyi amri mupya, kwamba mupendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mupendane vivyo hivyo.’ (Yoh. 13:34) Sheria ya Musa iliomba mutu amupende jirani yake kama anavyojipenda mwenyewe. (Law. 19:18) Lakini amri ya Yesu ilikuwa ‘mupya’ kwa kuwa ilitaja upendo ambao unaweza kutuchochea hata tutoe maisha yetu kwa ajili ya wengine, kama vile Yesu alivyofanya. Wakristo wengi wameonyesha upendo wenye uhodari kwa ‘kuhatarisha shingo zao wenyewe’ ili wasiwatoe ndugu zao mikononi mwa maadui wanaotaka kuwatesa ao kuwaua.​—Soma 1 Yohana 3:16.

Wakristo wa kwanza-kwanza walikataa kukana imani yao

16, 17. Wakristo fulani wa kwanza-kwanza walishindana na jaribu gani, na hali yao inafanana namna gani na ile ya Wakristo fulani wa leo?

16 Wakristo wa kwanza​-kwanza walimuabudu Yehova pekee yake kwa uhodari kama Yesu alivyofanya. (Mt. 4:8-10) Walikataa kuchoma uvumba ili kuonyesha heshima kwa mutawala wa Roma. (Ona picha.) Katika kitabu chake Daniel Mannix aliandika hivi: “Ni Wakristo wachache tu ndio waliokana imani hata ikiwa mazabahu iliyokuwa na moto unaowaka juu yake yaliwekwa katika uwanja kwa ajili yao. Mufungwa aliombwa kuchukua uvumba kidogo tu na kuutupa katika moto; akifanya hivyo anapewa kikaratasi cha kuonyesha kama ametoa zabihu na kisha alifunguliwa. Pia alielezwa vizuri kwamba hakuwa akimuabudu mutawala wa Roma; lakini kwa kufanya hivyo, alikuwa anaonyesha tu kwamba anatambua hali ya kimungu ya mutawala, ambayo inashikamana na cheo chake cha kuwa Mukubwa wa Serikali ya Roma. Hata hivyo, Wakristo wachache sana ndio waliotumia nafasi hiyo ili kufunguliwa.”

17 Mara nyingi Wakristo waliofungwa katika kambi za mateso za Nazi walilazimishwa kutia sinyatire juu ya vikaratasi ili kuonyesha kama wanamukana Yehova na kisha wangefunguliwa. Lakini ni wachache tu ndio waliotia sinyatire. Wakati wa mauaji ya kikabila yaliyotokea hivi karibuni huko Rwanda, Mashahidi Watutsi na Wahutu walihatarisha maisha yao kwa kufichana. Inaomba kuwa na imani na uhodari ili kushinda majaribu kama hayo.

KUMBUKA, YEHOVA YUPO PAMOJA NASI!

18, 19. Ni mifano gani iliyo katika Biblia ya watu waliotenda kwa imani na uhodari inayotusaidia katika kazi yetu ya kuhubiri?

18 Tuna pendeleo la kushiriki katika kazi kubwa inayopita kazi zote ambazo Mungu amekwisha kuwapatia watumishi wake hapa duniani, ni kusema, kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Tunafurahia sana mufano muzuri ambao Yesu alituachia. Yeye, ‘alisafiri kutoka jiji mupaka jiji na kutoka kijiji mupaka kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.’ (Lu. 8:1) Kama yeye, tunahitaji imani na uhodari ili kuhubiri habari njema ya Ufalme. Kwa musaada wa Mungu, tunaweza kutenda kwa uhodari kama Noa, ‘muhubiri wa haki,’ aliyehubiri kwa bidii katika ‘ulimwengu wa watu wasiomuogopa Mungu’ uliokuwa karibu kuangamizwa na garika.​—2 Pet. 2:4, 5.

19 Sala inatusaidia katika kazi yetu ya kuhubiri. Wakati wanafunzi fulani wa Yesu waliteswa, walimuomba Yehova awasaidie ‘waseme neno la Mungu kwa ujasiri,’ sala yao ilijibiwa. (Soma Matendo 4:29-31.) Ikiwa unasikia haya kidogo ya kuhubiri nyumba kwa nyumba, umuombe Yehova imani na uhodari zaidi, naye atajibu sala zako.​—Soma Zaburi 66:19, 20. *

20. Ni nani wanaotutegemeza sisi watumishi wa Yehova?

20 Si rahisi kushikamana na ibada ya kweli katika ulimwengu huu muovu na wenye majaribu mengi. Hata hivyo, hatuko pekee yetu. Mungu yupo pamoja nasi. Mwana wake, ambaye ni Kichwa cha kutaniko yupo pia pamoja nasi. Tuko pia na Mashahidi wenzetu zaidi ya 7 000 000 duniani pote. Basi, acheni sisi wote pamoja tuendelee kuwa na imani na kutangaza habari njema na kuchunga katika akili yetu andiko letu la mwaka wa 2013: “Uwe hodari na mwenye nguvu. . . . Yehova Mungu wako yupo pamoja nawe.”​—Yos. 1:9.

^ Utapata mifano mingi ya watu waliotenda kwa uhodari katika habari “Uwe Hodari na Mwenye Nguvu Sana” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 2, 2012.