Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tenda Kulingana na Sala Ambayo Yesu Alitoa

Tenda Kulingana na Sala Ambayo Yesu Alitoa

‘Baba, . . . mutukuze mwana wako, ili mwana wako apate kukutukuza wewe.’​—YOH. 17:1.

1, 2. Eleza mambo ambayo Yesu aliwafanyia mitume wake walipomaliza kusherehekea Pasaka katika mwaka wa 33.

 NI MANGARIBI sana ya siku 14 mwezi wa Nisani, mwaka wa 33. Yesu na mitume wake wamemaliza kusherehekea Pasaka, inayowakumbusha namna Mungu alivyokomboa mababu zao katika utumwa wa Misri. Lakini wanafunzi wake waaminifu wanangojea ukombozi mukubwa zaidi, “ukombozi wa milele.” Siku inayofuata, Kiongozi wao asiye na zambi atauawa na maadui wake. Lakini tendo hilo lenye kuchukiza litawaletea wanadamu baraka. Damu ya Yesu itakayomwangika itawatolea wanadamu nafasi ya kukombolewa katika zambi na kifo.​—Ebr. 9:12-14.

2 Ili kutusaidia tusisahau mupango huo wenye upendo, Yesu alianzisha sherehe mupya ya kila mwaka ambayo ilichukua nafasi ya Pasaka. Alifanya hivyo kwa kuvunja mukate usiotiwa chachu, na alipatia kila mumoja wa mitume wake waaminifu 11, na kusema hivi: “Huu unamaanisha mwili wangu ambao utatolewa kwa ajili yenu. Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” Alifanya hivyo pia kuhusu kikombe cha divai nyekundu, na kuwaambia: ‘Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa musingi wa damu yangu, ambayo itamwangwa kwa ajili yenu.’​—Lu. 22:19, 20.

3. (a) Ni badiliko gani kubwa ambalo lilitokea kisha kifo cha Yesu? (b) Tunapaswa kujiuliza maulizo gani kuhusiana na sala ya Yesu inayopatikana katika Yohana sura 17?

3 Kisha muda kidogo agano la zamani la Sheria ambalo Mungu alifanya na Waisraeli wa kimwili lingefikia mwisho wake. Na agano jipya kati ya Yehova na wafuasi wa Yesu lingechukua nafasi ya agano hilo. Yesu alihangaikia sana hali nzuri ya taifa hilo jipya la kiroho. Waisraeli wa kimwili hawakusikilizana na walikuwa wenye kugawanyika vibaya kidini, na hilo lilichafua jina takatifu la Mungu. (Yoh. 7:45-49; Mdo. 23:6-9) Lakini, Yesu alipenda wafuasi wake waendelee kutumika kwa umoja ili waweze kuletea jina la Mungu sifa. Yesu anafanya nini basi? Anatoa sala nzuri sana ambayo mwanadamu yeyote anaweza kufurahia kusoma. (Yoh. 17:1-26; ona picha mwanzoni mwa habari hii.) Tunapofikiria sala hiyo, tunaweza kujiuliza, “Je, Mungu alijibu sala ya Yesu?” Kila mumoja wetu anapaswa pia kujichunguza na kujiuliza hivi, “Je, ninatenda kulingana na sala hiyo?”

MAMBO AMBAYO YESU ALIKAZIA KWANZA

4, 5. (a) Maneno ambayo Yesu alisema mwanzoni mwa sala yake yanatufundisha nini? (b) Namna gani Yehova alimujibu Yesu aliposali kuhusu mahitaji yake mwenyewe?

4 Yesu aliendelea kuzungumuza na wanafunzi wake mupaka usiku sana, akiwafundisha mambo mazuri ya Mungu. Kisha aliinua macho yake kuelekea mbinguni na kusali hivi: ‘Baba, saa imefika ili mwana wako apate kukutukuza wewe, kulingana na vile ambavyo umemupa mamlaka juu ya wote wenye mwili, ili, wote ambao umemupa, yeye apate kuwapa uzima wa milele. Nimekutukuza duniani, nikiwa nimemaliza kazi ambayo umenipa niifanye. Kwa hiyo sasa wewe, Baba, nitukuze kando yako kwa utukufu niliokuwa nao kando yako kabla ya ulimwengu kuwako.’​—Yoh. 17:1-5.

5 Fikiria mambo ambayo Yesu alikazia kwanza mwanzoni mwa sala yake. Alisali kwanza kuhusu kutakaswa kwa jina la Mungu, na hilo linapatana na ombi la kwanza katika sala yake ya kielelezo inayoanza hivi: “Baba, jina lako na litakaswe.” (Lu. 11:2) Kisha, Yesu alisali kuhusu mahitaji ya wanafunzi wake, ili “apate kuwapa uzima wa milele.” Kisha hapo, Yesu alimuomba Baba yake jambo fulani, aliposema hivi: “Baba, nitukuze kando yako kwa utukufu niliokuwa nao kando yako kabla ya ulimwengu kuwako.” Yehova alijibu sala ya Mwana wake mwaminifu kwa kumutolea mambo mengi kuliko yale aliyoomba; alimupatia “jina bora kabisa kuliko” malaika wote.​—Ebr. 1:4.

‘KUPATA UJUZI JUU YA MUNGU WA PEKEE WA KWELI’

6. Ili mitume wapate uzima wa milele, walipaswa kufanya nini, na tunajua namna gani kwamba waliendelea kufanya hivyo?

6 Yesu alisali pia kuhusu jambo ambalo sisi wanadamu watenda​-zambi tunapaswa kufanya ili tupate zawadi isiyostahiliwa ya uzima wa milele. (Soma Yohana 17:3.) Alisema kwamba tunapaswa ‘kuendelea kupata ujuzi’ juu ya Mungu na Kristo. Njia moja ya maana inayotusaidia ni kujifunza kumuhusu Yehova na Mwana wake. Tunaendelea pia kupata ujuzi juu ya Mungu tunapojionea furaha inayotokana na kutumia mambo tunayojifunza kumuhusu yeye katika maisha yetu. Maneno ambayo Yesu alisema katika sala yake yanaonyesha kwamba mitume walikuwa wamefanya mambo hayo yenye kuleta uzima. Alisali hivi: “Maneno uliyonipa nimewapa, nao wameyapokea.” (Yoh. 17:8) Lakini, ili wapate uzima wa milele, walipaswa kuendelea kutafakari kuhusu mafundisho ya Mungu na kutumikisha mambo hayo katika maisha yao ya kila siku. Je, mitume waaminifu waliendelea kufanya hivyo mupaka mwisho wa maisha yao duniani? Bila shaka walifanya hivyo. Tunajua hivyo kwa sababu jina la kila mumoja wao limeandikwa kwa mwandiko usioweza kufutwa kwenye mawe 12 ya musingi ya Yerusalemu Mupya la mbinguni.​—Ufu. 21:14.

7. “Kumujua” Mungu kunamaanisha nini, na sababu gani ni jambo la maana sana tumujue?

7 Kulingana na watu wenye elimu ya luga ya Kigiriki, maneno ya Kigiriki yanayotafsiriwa “waendelee kupata ujuzi” yanaweza pia kumaanisha “wanapaswa kuendelea kutafuta ujuzi” ao “wanapaswa kuendelea kujua.” Maana hayo mawili yanazungumuzia jambo moja, na yote mawili ni ya lazima. Katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kifaransa yenye marejezo (Rbi8-F) maelezo ya chini kwenye andiko la Yohana 17:3 yanatafsiri maneno hayo hivi: “Wakujue wewe.” Kwa hiyo, maneno “waendelee kupata ujuzi” yanaonyesha kwamba mutu anapaswa kuendelea kujifunza mengi juu ya Mungu ili kufikia ‘kumujua’ Mungu vizuri. Lakini, kumujua Mutu mukubwa zaidi wa ulimwengu wote, kunamaanisha mengi zaidi ya kujua tu sifa zake na kusudi lake. Kumujua Mungu kunamaanisha kumupenda sana na kuwa na urafiki wa karibu pamoja naye. Kunamaanisha pia kupenda ndugu na dada zetu na kuwa na urafiki wa karibu pamoja nao. Biblia inafasiria jambo hilo hivi: ‘Yeye ambaye hapendi hajamujua Mungu.’ (1 Yoh. 4:8) Kwa hiyo, kumujua Mungu kunamaanisha kujitiisha kwake. (Soma 1 Yohana 2:3-5.) Bila shaka, ni pendeleo kubwa kuwa mumoja wa wale wanaomujua Yehova! Lakini, kama mufano wa Yuda Iskariote unavyoonyesha, tunaweza kupoteza pendeleo hilo. Acheni basi tujikaze ili kuchunga pendeleo hilo. Ikiwa tunafanya hivyo, tutapata zawadi isiyostahiliwa ya uzima wa milele.​—Mt. 24:13.

“KWA SABABU YA JINA LAKO”

8, 9. Ni jambo gani ambalo Yesu alihangaikia sana alipokuwa duniani, na ni desturi gani ya kidini ambayo alipinga?

8 Kisha kusoma sala ya Yesu katika Yohana sura 17, utaona waziwazi kwamba Yesu aliwapenda sana mitume wake na wale ambao wangekuwa wanafunzi wake katika siku ambazo zingefuata. (Yoh. 17:20) Wakati huohuo, tunapaswa kujua kwamba si wokovu wetu ambao Yesu alihangaikia kwanza. Jambo ambalo alihangaikia kwanza kuanzia mwanzo mupaka mwisho wa kazi yake ya kuhubiri lilikuwa kutakaswa na kutukuzwa kwa jina la Baba yake. Kwa mufano, alipokuwa katika sinagogi la Nazareti akieleza sababu gani alikuja duniani, Yesu alisoma hivi katika kitabu cha kukunjwa cha Isaya: “Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kuwatangazia maskini habari njema.” Bila shaka, Yesu alitaja jina la Mungu aliposoma maneno hayo.​—Lu. 4:16-21.

9 Miaka mingi mbele ya Yesu kuja duniani, viongozi wa dini ya Wayahudi walikataza watu kutumia jina la Mungu. Tunaweza kuwa hakika kwamba Yesu alipinga kabisa desturi hiyo isiyopatana na Maandiko. Aliwaambia wapinzani wake hivi: ‘Mimi nimekuja katika jina la Baba yangu, lakini ninyi hamunipokei; ikiwa mutu mwingine angefika katika jina lake mwenyewe, mungemupokea huyo.’ (Yoh. 5:43) Kisha, siku chache mbele ya kifo chake, Yesu alizungumuzia jambo ambalo alihangaikia sana aliposali hivi: “Baba, litukuze jina lako.” (Yoh. 12:28) Kwa hiyo, tunaelewa waziwazi sababu gani Yesu alitaja sana jina la Baba yake katika sala tunayozungumuzia sasa.

10, 11. (a) Ni katika maana gani Yesu alijulisha jina la Baba yake? (b) Sababu gani wanafunzi wa Yesu wanajulisha watu jina la Mungu?

10 Yesu alisali hivi: ‘Nimelifunua jina lako kwa watu ulionipa kutoka ulimwenguni. Walikuwa wako, nawe ukanipa, nao wamelishika neno lako. Pia, mimi simo tena ulimwenguni, bali wao wamo ulimwenguni nami ninakuja kwako. Baba Mutakatifu, walinde kwa sababu ya jina lako ambalo umenipa, ili wawe kitu kimoja kama vile sisi tulivyo.’​—Yoh. 17:6, 11.

11 Yesu aliwafundisha wanafunzi wake jina la Baba yake, lakini hilo lilimaanisha mengi zaidi ya kuwatajia tu jina hilo. Yesu aliwasaidia waelewe Yehova ni nani, ni kusema, sifa zake na namna anavyoshugulika na wanadamu. (Kut. 34:5-7) Zaidi ya hayo, akiwa katika utukufu huko mbinguni, Yesu anaendelea kusaidia wanafunzi wake wajulishe jina la Yehova katika dunia yote. Sababu gani wanafunzi wa Yesu wanajulisha watu jina la Mungu? Wanafanya hivyo ili watu wengi wawe wanafunzi wa Yesu mbele ya mwisho wa ulimwengu huu muovu. Kisha, Yehova atalitukuza jina lake kwa njia kubwa zaidi atakapowaokoa mashahidi wake waaminifu.​—Eze. 36:23.

“ILI ULIMWENGU UPATE KUAMINI”

12. Ni mambo gani matatu yanayoweza kutusaidia tufanye vizuri kazi yetu ya kuokoa maisha ya watu?

12 Alipokuwa duniani, Yesu alijikaza kusaidia wanafunzi wake wapambane na uzaifu wao mbalimbali. Hilo lilikuwa jambo la maana kwao kwa sababu lingewasaidia kumaliza kazi ambayo alikuwa ameanza. Yesu alisali hivi: “Kama vile ulivyonituma ulimwenguni, vivyo hivyo mimi pia nimewatuma ulimwenguni.” Lakini, ili wafanye vizuri kazi hiyo ya kuokoa maisha ya watu, Yesu alikazia mambo matatu ya lazima. Kwanza, alisali kwamba wanafunzi wake hawapaswe kuwa sehemu ya ulimwengu muovu wa Shetani. Pili, alisali kwamba wanafunzi wake watakaswe, ao waendelee kuwa watakatifu, kwa kutumikisha mafundisho ya kweli ya Neno la Mungu katika maisha yao. Tatu, Yesu alisali mara nyingi kwamba wanafunzi wake wapendane na kuwa na umoja kama yeye na Baba yake. Kwa hiyo, kila mumoja wetu anapaswa kujichunguza kwa kujiuliza hivi: ‘Je, ninatenda kulingana na mambo hayo matatu?’ Yesu alikuwa hakika kwamba wanafunzi wake wangefanya mambo hayo ‘ili ulimwengu upate kuamini kwamba [Mungu] alimutuma.’​—Soma Yohana 17:15-21.

Roho takatifu iliwasaidia Wakristo wa kwanza​-kwanza kulinda umoja (Ona fungu la 13)

13. Katika siku za mitume, ni nini inayoonyesha kwamba sala ya Yesu ilijibiwa?

13 Kitabu cha Matendo ya Mitume kinaonyesha waziwazi kwamba sala ya Yesu ilijibiwa. Kati ya Wakristo wa kwanza-kwanza kulikuwa Wayahudi na Watu wa Mataifa, matajiri na maskini, watumwa na mabwana; kwa hiyo mugawanyiko ungeweza kutokea kati yao. Lakini, wote walikuwa na umoja, na ndiyo sababu walilinganishwa na sehemu mbalimbali za mwili wa mutu, Yesu akiwa kichwa chao. (Efe. 4:15, 16) Huo ulikuwa muujiza kabisa katika ulimwengu wa Shetani wenye kugawanyika! Sifa zote zinapaswa kumuendea Yehova, ambaye alifanya jambo hilo liwezekane kupitia nguvu ya roho yake takatifu.​—1 Kor. 3:5-7.

Watu wa Yehova wanafanyiza familia yenye umoja ulimwenguni pote (Ona fungu la 14)

14. Sala ya Yesu imejibiwa namna gani katika siku zetu?

14 Jambo la kuhuzunisha ni kwamba umoja huo haukuendelea kisha kifo cha mitume. Lakini, kama ilivyotabiriwa, uasi​-imani mukubwa ulitokea, nao ulitokeza dini zinazojidai kuwa za Kikristo zenye kugawanyika. (Mdo. 20:29, 30) Hata hivyo, katika mwaka wa 1919, Yesu aliwakomboa wafuasi wake watiwa​-mafuta katika dini ya uongo na aliwakusanya pamoja katika “kifungo kikamilifu cha muungano.” (Kol. 3:14) Kazi yao ya kuhubiri imekuwa na matokeo gani juu ya watu wengine? “Kondoo wengine” zaidi ya milioni saba kutoka ‘mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na luga’ wamekusanywa na wanamuabudu Yehova kwa umoja pamoja na watiwa​-mafuta wa Mungu. (Yoh. 10:16; Ufu. 7:9) Bila shaka Yehova amejibu kwa njia yenye kushangaza sala ambayo Yesu alitoa aliposali hivi: “Ili ulimwengu upate kujua kwamba wewe ulinituma na kwamba uliwapenda wao kama vile ulivyonipenda mimi”!​—Yoh. 17:23.

UMALIZIO MUZURI

15. Yesu alitoa ombi gani la pekee kuhusu wanafunzi wake watiwa​-mafuta?

15 Muda kidogo mbele ya usiku wa Nisani 14, Yesu aliwaheshimu mitume wake kwa kufanya nao agano la kutawala pamoja naye katika Ufalme wake. (Lu. 22:28-30; Yoh. 17:22) Kwa hiyo, kuhusu wale wote ambao baadaye wangekuwa wafuasi wake wenye kutiwa mafuta, Yesu anasali hivi: ‘Baba, kwa habari ya kile ambacho umenipa, ninataka kwamba, mahali nilipo, wao pia wapate kuwa pamoja nami, ili wauone utukufu wangu ambao umenipa, kwa sababu ulinipenda kabla ya kuwekwa kwa musingi wa ulimwengu.’ (Yoh. 17:24) Kuliko kuwasikilia wivu Wakristo watiwa​-mafuta, kondoo wengine wanafurahia sana jambo hilo na linaonyesha pia kwamba kuna umoja kati ya Wakristo wote wa kweli wanaoishi duniani leo.

16, 17. (a) Katika umalizio wa sala yake, Yesu alisema kwamba angeendelea kufanya nini? (b) Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

16 Viongozi wa kidini, wanapofusha macho ya watu wengi ili wasione waziwazi kwamba Yehova ana watu wenye umoja na wanaomujua vizuri. Hali ilikuwa hivyo pia katika siku za Yesu. Kwa hiyo, Yesu anamalizia sala yake na maneno haya yenye kupendeza: “Baba Mwadilifu, kwa kweli, ulimwengu haujakujua wewe; lakini mimi nimekujua, na hawa wamejua kwamba ulinituma. Nami nimewajulisha jina lako nami nitalijulisha, ili upendo ulionipenda nao upate kuwa ndani yao nami katika muungano pamoja nao.”​—Yoh. 17:25, 26.

17 Hakuna mumoja kati yetu anayeweza kusema kwamba Yesu hakutenda kulingana na sala yake. Kwa kuwa yeye ndiye Kichwa cha kutaniko, Yesu anaendelea kutusaidia kujulisha jina na kusudi la Baba yake. Acheni tuendelee kujitiisha chini ya uongozi wake kwa kuhubiri na kufanya wanafunzi kwa bidii. (Mt. 28:19, 20; Mdo. 10:42) Acheni sisi pia tufanye yote tunayoweza ili kulinda umoja wetu wenye samani. Kwa kufanya hivyo, tutakuwa tukitenda kulingana na sala ya Yesu, na hilo litatukuza jina la Yehova na kutuletea furaha ya milele.