Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Hauwezi Kuwatumikia Mabwana Wawili

Hauwezi Kuwatumikia Mabwana Wawili

‘Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili . . . Hamuwezi kutumikia Mungu na Utajiri.’—MT. 6:24.

1-3. (a) Watu wengi leo wana matatizo gani ya feza, na namna gani wamoja wanajaribu kuyamaliza? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.) (b) Hilo linatokeza shida gani kuhusu kuwalea watoto?

DADA Marilyn anasema hivi: “Kila siku bwana yangu James alikuwa akirudi nyumbani akiwa mwenye kuchoka, lakini mushahara wake haukutosha ili kutimiza mahitaji yetu ya kila siku.” * Dada Marilyn anaongezea hivi: “Nilitaka kumupunguzia muzigo na kumusaidia kumuuzia mutoto wetu, Jimmy, vitu fulani vizuri kama vile ambavyo wanafunzi wenzake walikuwa navyo.” Marilyn alitaka pia kuwasaidia watu wa jamaa yake na kuweka feza za kuwasaidia wakati ujao. Rafiki zake wengi walihamia katika inchi zingine ili kutafuta feza nyingi. Kwa hiyo, alipofanya mupango wa kuhamia katika inchi nyingine, alitamani kuenda lakini alikuwa na wasiwasi. Sababu gani?

2 Marilyn aliogopa kuacha familia yake ambayo alipenda sana na programu yao nzuri ya mambo ya kiroho. Lakini, aliona kwamba wengine wamehamia katika inchi za kigeni kwa muda fulani, na familia zao zilionekana kuwa na hali nzuri ya kiroho. Lakini alijiuliza namna gani angemulea mutoto wake Jimmy akiwa mbali naye. Je, angeweza kumulea vizuri mutoto wake ‘katika nizamu na muongozo wa akilini wa Yehova’ kupitia Internete?—Efe. 6:4.

3 Marilyn alitafuta muongozo. Bwana yake hakupenda awaache, hata hivyo alisema kwamba hangejaribu kumuzuia. Wazee na wengine katika kutaniko walimushauri Marilyn asiende  katika inchi nyingine, lakini dada wengi walimutia moyo aende tu. Walimuambia hivi: “Ikiwa unapenda familia yako, utaenda na huko utaendelea kumutumikia Yehova.” Ijapokuwa alikuwa na wasiwasi, Marilyn alilaga bwana yake James na mutoto wake Jimmy na kuenda katika inchi ya kigeni. Aliwaahidia hivi: “Sitakawia.”

MADARAKA YA FAMILIA NA KANUNI ZA BIBLIA

4. Sababu gani watu wengi wanahamia katika inchi zingine, lakini mara nyingi wanaachia nani daraka la kuwatunza watoto wao?

4 Yehova hapendi watumishi wake waishi katika umaskini. Watu wa zamani walihamia katika inchi zingine ili kuepuka umaskini. (Zab. 37:25; Met. 30:8) Ili kuepuka wasikufe kwa sababu ya njaa, muzee wa ukoo Yakobo aliwatuma wana wake huko Misri ili wanunue chakula. * (Mwa. 42:1, 2) Leo, watu wengi wanaohamia katika inchi za kigeni hawafanye hivyo kwa sababu ya njaa. Lakini, wanaweza kufanya hivyo ili kupata feza za kulipa madeni. Wengine wanapenda kuhama kwa sababu tu wanataka kufanya maisha ya familia yao yawe mazuri zaidi. Kwa sababu ya matatizo ya feza, wengi wanaenda kuishi mbali na familia yao katika inchi ileile ao wanahamia katika inchi nyingine. Mara nyingi wanaacha watoto wao wadogo watunzwe na muzazi mumoja, kaka ao dada, tate (ao nkambo), watu wengine wa jamaa ao marafiki. Hata ikiwa inahuzunisha kuacha bibi ao bwana na watoto, wengi wanaoenda kutumikia katika inchi zingine wanaona kwamba wanalazimishwa tu kuenda huko.

5, 6. (a) Kulingana na mafundisho ya Yesu, furaha na usalama wa kweli vinatokana na nini? (b) Yesu alifundisha wafuasi wake wasali kuhusu nini? (c) 

5 Katika siku za Yesu, watu wengi walikuwa maskini na wenye uhitaji. Na pengine walifikiri kwamba wangepata furaha na usalama ikiwa tu wangepata feza nyingi. (Mk. 14:7) Lakini Yesu alitaka watu watumainie jambo lingine kuliko feza. Alipenda watu watumainie Yehova ambaye anaweza kuwatolea utajiri usio na mwisho. Katika Mahubiri yake ya Mulimani, Yesu alionyesha kwamba furaha na usalama wa kweli havitokane na vitu vya kimwili wala uwezo wetu mbalimbali, lakini vinatokana na uhusiano wetu pamoja na Baba yetu wa mbinguni.

6 Katika sala yake ya mufano, Yesu hakutufundisha tusali ili kupata usalama kupitia vitu vya kimwili, lakini tusali ili kupata ‘mukate wetu kwa ajili ya siku hii,’ ni kusema, mahitaji yetu ya kila siku. Aliwaambia waziwazi wasikilizaji wake hivi: “Acheni kujiwekea hazina duniani . . . Badala yake, jiwekeeni hazina mbinguni.” (Mt. 6:9, 11, 19, 20) Tunaweza kuwa hakika kwamba Yehova atatubariki kama vile ameahidi. Baraka ya Mungu inatia ndani mambo mengi kuliko tu kukubaliwa naye. Hilo linaonyesha kwamba anaweza kututolea kabisa yote tunayohitaji. Bila shaka, njia moja ya kupata furaha na usalama wa kweli ni kumutumainia Yehova, Baba yetu anayetuhangaikia kuliko kutumainia feza.​—Soma Mathayo 6:24, 25, 31-34.

7. (a) Ni nani ambao Yehova amepatia daraka la kulea watoto? (b) Sababu gani wazazi wote wawili wanapaswa kusaidiana sana ili kuwalea watoto wao?

7 ‘Kutafuta kwanza uadilifu ao haki ya Mungu’ kunatia ndani kuona madaraka ya familia kama vile Yehova anavyoyaona. Sheria ya Musa ina kanuni ambayo Wakristo wanaweza kutumia. Kanuni hiyo inaonyesha kwamba wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto wao sheria za Yehova. (Soma Kumbukumbu 6:6, 7.) Hilo ni daraka ambalo Mungu amewapatia wazazi. Hilo si daraka la tate ao nkambo ya watoto wala mutu mwengine yeyote. Mufalme Sulemani alisema hivi: ‘Mwana wangu sikiliza nizamu ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.’ (Met. 1:8) Yehova alitaka wazazi wote wawili wasaidiane kuwaongoza na kuwafundisha watoto wao. (Met. 31:10, 27, 28) Wakati watoto  wanawasikiliza wazazi wao wakizungumuza kuhusu Yehova kila siku na kuona namna wanavyomutumikia, wanaweza kuiga mufano wao.

MATOKEO YASIYOTAZAMIWA

8, 9. (a) Ni mabadiliko gani yanayotokea mara nyingi wazazi wanapoenda kuishi mbali na familia yao? (b) Ni matatizo gani yanayoweza kutokea ikiwa muzazi mumoja anaishi mbali na familia?

8 Mbele ya kuenda katika inchi nyingine, wale wanaotaka kuhama wanajaribu kufikiria kwa uzito hatari na mambo ya kujinyima. Lakini ni wachache tu ndiyo wanaofikiria matokeo ya kuacha familia. (Met. 22:3) * Muda mufupi tu kisha dada Marilyn kuacha familia yake, alianza kusumbuka katika moyo wake. Hilo lilisumbua pia bwana yake na Jimmy mutoto wao. Jimmy aliendelea kumuuliza mama yake hivi: “Sababu gani uliniacha?” Marilyn hakurudi kisha miezi michache kama alivyokuwa akipanga, lakini alirudi kisha miaka fulani. Aliporudi, alikuta mabadiliko mengi yenye kuhuzunisha katika familia yake. Jimmy alishindwa kumukaribia mama yake, na haikuwa rahisi kuzungumuza naye. Marilyn anakumbuka kwa huzuni hivi: “Upendo wake kwangu ulikuwa umepotea kabisa.”

9 Wakati wazazi na watoto hawaishi pamoja katika familia, wanaweza kuteseka moyoni na kuwa na mwenendo mubaya. * Watoto wadogo wanapoachwa kwa muda murefu, jambo hilo linaweza kuwaumiza sana moyoni. Marilyn alimuambia Jimmy kwamba alienda kutumikia katika inchi ya kigeni kwa faida yake. Lakini Jimmy aliona kwamba mama yake amemuacha kabisa. Mwanzoni, Jimmy alijisikia vibaya kwa sababu mama yake alikuwa mbali naye. Lakini mama yake alipofika kuwatembelea, alichukia kumuona. Watoto wengi wanaoachwa na muzazi wanajisikia hivyo. Jimmy alijisikia kwamba hahitaji tena kumuheshimu na kumupenda mama yake.​—Soma Methali 29:15.

Hauwezi kumukumbatia mutoto wako kwenye Internete (ona fungu la 10)

10. (a) Ikiwa wazazi wanawatumia tu watoto wao zawadi kuliko kuwa pamoja nao, hilo linaweza kuwa na matokeo gani? (b) Muzazi anaweza kushindwa kufanya jambo gani ikiwa anamulea mutoto wake akiwa mbali naye?

10 Hata hivyo, Marilyn alijaribu kutuma feza na zawadi fulani ili ionekane kwamba haiko mbali na mutoto wake, lakini bila kujua, alimufanya mutoto wake apende vitu vya kimwili kuliko kupenda familia yao na hata Yehova. (Met. 22:6) Jimmy alimuambia mama yake kwamba asirudi nyumbani lakini aendelee tu kumutumia zawadi. Marilyn alitambua kwamba hangeendelea kumulea mutoto wake kupitia barua, telefone  ao video kwenye Internete. Marilyn anasema hivi: “Kupitia Internete, hauwezi kumukumbatia mutoto wako mbele alale.”

Unapoishi mbali na bibi ao bwana yako, unaweza kupambana na hatari gani? (ona fungu la 11)

11. (a) Kutumikia mbali na familia kunaweza kuwa na matokeo gani juu ya ndoa? (b) Namna gani dada mumoja alifikia kutambua kwamba alipaswa kurudi nyumbani?

11 Uhusiano wa Marilyn pamoja na Yehova na bwana yake James, ulikuwa umeharibika kabisa. Pia, uhusiano wake pamoja na ndugu na dada ulikuwa umepunguka na hakuwa anahubiri tena kwa ukawaida. Tatizo lingine alilopambana nalo ni kwamba mukubwa wake wa kazi alitaka kulala naye. Kwa kuwa Marilyn na James hawakuwa pamoja ili kuzungumuzia matatizo yao, wote wawili waliwaelezea watu wengine namna walivyojisikia moyoni na walikuwa karibu kuangukia katika uzinifu. Marilyn alikuja kutambua kwamba hata ikiwa yeye na bwana yake hawakuangukia katika uzinifu, kwa kuwa hawakuishi pamoja, hawangefuata muongozo wa Biblia wa kutimiziana mahitaji ya moyoni na ya ngono. Hawangefurahia mambo ambayo bibi na bwana wanafurahia wanapokuwa pamoja, kama vile kugusana kwa upendo, kukumbatiana ili ‘kuonyeshana mapenzi,’ ao kupatiana “haki” ya ndoa. (Wim. 1:2; 1 Kor. 7:3, 5) Hawangemuabudu tena Yehova pamoja na mutoto wao. Marilyn anakumbuka hivi: “Niliposikia kwenye mukusanyiko mumoja kwamba ibada ya familia ni ya lazima kwetu ili tuokoke siku kubwa ya Yehova, nilielewa kwamba ni jambo la lazima nirudi nyumbani. Nilipaswa kutengeneza uhusiano wangu pamoja na Yehova na familia yangu.”

MASHAURI MAZURI NA MASHAURI MABAYA

12. Ni shauri gani la Biblia tunaloweza kuwatolea wale wanaoishi mbali na familia zao?

12 Wakati Marilyn aliamua kurudi nyumbani, wamoja walimutolea mashauri mazuri, na wengine walimutolea mashauri mabaya. Wazee wa kutaniko lake walimusifu kwa sababu ya imani na ujasiri wake. Lakini wengine walioishi pia mbali na bibi ao bwana zao hawakufurahi. Kuliko kufuata mufano wake muzuri, walipenda kumushawishi abaki mbali na familia yake. Walimuambia hivi: “Ukirudi nyumbani, namna gani utapata feza za kutosha? Utalazimika kurudi tena hapa kisha muda mufupi.” Kuliko kuwa na masemi kama hayo yenye kuvunja moyo, Wakristo wanapaswa kuwashauri “wanawake vijana wawapende waume zao, wawapende watoto wao, wawe . . . wafanyakazi nyumbani, ili neno la Mungu lisitukanwe.”—Soma Tito 2:3-5.

13, 14. Sababu gani inaomba kuwa na imani ili kumuheshimu Yehova kuliko watu wa familia? Toa mufano.

13 Watu wengi wanaohamia katika inchi zingine wamekomalia katika maeneo ambamo watu wanaheshimu sana desturi za kwao na watu wa jamaa, zaidi sana wazazi kuliko mutu mwengine yeyote. Mukristo anapaswa kuwa na imani yenye nguvu ili kumuheshimu Yehova kuliko kuheshimu desturi za familia ikiwa hazimupendeze Yehova.

 14 Tuzungumuzie mufano wa Carin. Yeye anasema hivi: “Mutoto wangu Don alipozaliwa, mimi na bwana yangu tulikuwa tunatumikia katika inchi ya kigeni, na muda mufupi baadaye nilikuwa nimeanza kujifunza Biblia. Kila mutu katika jamaa yangu alitazamia kwamba nitamutuma Don nyumbani ili wazazi wangu wamulee mupaka wakati tutakuwa na maisha mazuri.” Wakati Carin alisema kwamba anapaswa kulea mutoto wake yeye mwenyewe, watu wa jamaa yake, na bwana yake, walimucheka sana na kumuita muvivu. Carin anasema hivi: “Kwa kweli, mwanzoni, sikuona ubaya wowote kumutuma Don kwa wazazi wangu wamulee kwa miaka fulani. Lakini nilijua kwamba kulea mutoto wetu, ni daraka ambalo Yehova alitutolea sisi wazazi.” Carin alipopata tena mimba, bwana yake ambaye hakuwa Shahidi, alimuomba atoshe mimba hiyo. Uamuzi ambao Carin alikuwa amechukua hapo mwanzoni ulitia nguvu imani yake na kumusaidia abaki tena imara kwa Yehova. Sasa Carin pamoja na bwana yake na watoto wao wanafurahi sana kwa kuwa wote walibaki pamoja. Ikiwa Carin angetuma mutoto wake mumoja ao wote wawili walelewe na watu wengine, matokeo yangekuwa mabaya kabisa.

15, 16. (a) Dada mumoja alijionea mambo gani kwa sababu ya kulelewa mbali na wazazi wake? (b) Sababu gani aliamua kutenda tofauti alipozaa binti yake?

15 Dada mumoja anayeitwa Vicky anasema hivi: “Muda wa miaka fulani nkambo ao tate mwanamuke muzala-mama alinilea, wakati ambapo wazazi wangu walibakia na dada yangu mudogo. Kisha, niliporudi kwa wazazi wangu, sikujisikia kuwa ninawapenda. Lakini, dada yangu mudogo alijisikia huru kuzungumuza nao, kuwakumbatia, na alifurahia urafiki wa karibu pamoja nao. Mimi sikujisikia kuwa karibu na wazazi wangu, hata nilipokuwa mutu muzima, ilikuwa vigumu kwangu kuwaambia namna nilijisikia moyoni. Mimi na dada yangu mudogo tuliwahakikishia wazazi wetu kwamba tutawatunza katika miaka yao ya uzee. Mimi nitawatunza tu kwa sababu ni wazazi wangu, lakini dada yangu mudogo yeye atafanya hivyo kwa sababu anachochewa na upendo.

16 Vicky anasema tena hivi: “Sasa mama yangu alitaka nimutumie binti yangu amulee, kama alivyonituma kwa mama yake. Nilikataa kwa busara. Mimi na bwana yangu tunapenda kumulea mutoto wetu katika njia za Yehova. Na sipendi kuharibu uhusiano wangu wa wakati ujao pamoja na binti yangu.” Vicky ametambua kwamba siri ya kufanikiwa ni kutia Yehova na kanuni zake pa nafasi ya kwanza kuliko miradi ya kupata feza na kufurahisha familia. Yesu alisema waziwazi hivi: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili,” ni kusema, Mungu na Utajiri.​—Mt. 6:24; Kut. 23:2.

YEHOVA ANAFANYA JITIHADA ZETU ‘ZIFANIKIWE’

17, 18. (a) Kila siku Wakristo wanapaswa kuchukua uamuzi gani? (b) Tutazungumuzia maulizo gani katika habari inayofuata?

17 Baba yetu Yehova, ameahidi kwamba atatusaidia tupate kabisa yale tunayohitaji ikiwa tunatia Ufalme na haki yake pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu. (Mt. 6:33) Kwa hiyo, kila siku Wakristo wa kweli wana uamuzi wa kuchukua. Yehova anaahidi kututolea ‘njia ya kutokea’ ambayo haitatuomba tuvunje kanuni za Biblia, hata kuwe jaribu la namna gani. (Soma 1 Wakorintho 10:13.) Ikiwa ‘tunamungojea [Yehova] kwa kutamani,’ na ikiwa ‘tunamutegemea’ kwa kusali atupatie hekima yake, atuongoze, na ikiwa tunatii amri na kanuni zake, Yeye “atatenda” kwa faida yetu. (Zab. 37:5, 7) Atabariki jitihada zetu za kumutumikia yeye peke yake aliye Bwana wetu wa kweli. Ikiwa tunamutia pa nafasi ya kwanza, atafanya ‘tufanikiwe’ katika maisha yetu.​—Linganisha na Mwanzo 39:3.

18 Tunaweza kufanya nini ili kumaliza matatizo yaliyoletwa kwa sababu ya kuishi mbali na familia yetu? Tunaweza kufanya nini ili kutimizia watu wa familia yetu mahitaji yao bila kuishi mbali nao? Na namna gani tunaweza kuwatia wengine moyo ili wachukue maamuzi mazuri kuhusiana na hali hiyo? Habari inayofuata itajibu maulizo hayo.

^ fu. 1 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 4 Katika kila safari ya kwenda huko Misri, wana wa Yakobo hawakufanya zaidi ya majuma matatu wakiwa mbali na familia zao. Lakini wakati Yakobo na wana wake walihamia huko Misri, walienda pamoja na bibi zao na watoto wao.​—Mwa. 46:6, 7.

^ fu. 8 Ona Amuka! ya Mwezi wa 2, 2013 yenye kichwa “Kuhamia Nchi Nyingine—Matarajio na Mambo Halisi.”

^ fu. 9 Ripoti nyingi kutoka katika inchi mbalimbali zinaonyesha kwamba kuishi mbali na bibi ao bwana ao watoto ili kutumikia katika inchi za kigeni kumeleta matatizo makubwa katika familia. Hilo linaweza kufanya bibi ao bwana asiwe mwaminifu kwa mwenzake, kuangukia katika zambi ya mwanaume kulala na mwanaume na mwanamuke kulala na mwanamuke, kufanya ngono na mutu wa jamaa. Watoto pia wanaweza kuwa na mwenendo mubaya, wanaweza kupata matatizo kwenye masomo, wanaweza kuwa wakali, wenye kuvunjika moyo, kuwa na huzuni, kushuka moyo, na kutaka kujiua.