Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Unajikaza Kufikia Ukomavu wa Kristo?

Unajikaza Kufikia Ukomavu wa Kristo?

Tufikie . . . kipimo cha kimo ambacho ni cha ujazo wa Kristo.’—WAEFESO 4:13.

NYIMBO: 69, 70

1, 2. Kila Mukristo anapaswa kuwa na kusudi gani? Toa mufano.

MWANAMUKE anakazia uangalifu jambo gani wakati anachagua matunda katika soko? Hakazie tu akili yake juu ya matunda makubwa-makubwa ao ya bei chini. Lakini, anatafuta matunda yenye harufu nzuri, yenye kukomaa, na yenye kuiva. Anapenda apate matunda yenye kuiva, ni kusema, yenye kukomaa.

Mukristo mwenye kukomaa kiroho anaendelea kutafuta kanuni za Biblia zenye zitamusaidia kujua mema na mabaya

2 Kisha mutu kujifunza juu ya Yehova na kuamua kubatizwa, urafiki wake pamoja na Yehova unaendelea kukomaa. Kusudi lake ni kufikia kuwa Mukristo mwenye kukomaa. Ukomavu huo haumaanishe kuwa na miaka mingi ya kuzaliwa. Ni ukomavu wa kiroho, ni kusema, kuwa na urafiki wa sana pamoja na Yehova. Mutume Paulo alipenda Wakristo wa Efeso wakomae kiroho. Aliwatia moyo wakuwe na umoja katika imani na waendelee kujifunza juu ya Yesu ili kufikia kuwa ‘watu waliokomaa, kufikia kipimo cha kimo ambacho ni cha ujazo wa Kristo.’—Waefeso 4:13.

3. Hali ya ndugu na dada katika kutaniko la Efeso inafanana namna gani na hali ya watumishi wa Yehova leo?

3 Wakati mutume Paulo aliandikia Wakristo wa kutaniko la Efeso, kutaniko hilo lilikuwa limeanzishwa tangu miaka fulani. Wakristo wengi katika kutaniko hilo walikuwa na uzoefu, ni kusema, wenye kukomaa kiroho. Lakini, Wakristo fulani kati yao walikuwa na lazima ya kufanya urafiki wao na Yehova ukuwe nguvu zaidi. Vilevile, leo ndugu na dada wengi wamemutumikia Yehova kwa miaka mingi, na wamekomaa kiroho. Lakini, katika makutaniko Wakristo fulani hawajakomaa kiroho. Kwa mufano, maelfu ya watu wanabatizwa kila mwaka; ndiyo sababu Wakristo fulani wanahitaji kukomaa kiroho. Je, uko kati ya watu hao?—Wakolosai 2:6, 7.

NAMNA GANI MUKRISTO ANAWEZA KUKOMAA KIROHO?

4, 5. Wakristo wenye kukomaa kiroho wanatofautiana namna gani, lakini ni nini inaonyesha kwamba wote wamekomaa kiroho? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

4 Wakati unachagua matunda katika soko, unaona kwamba matunda yote haifanane kabisa. Lakini, kuna alama fulani zenye kuonyesha kwamba matunda hayo yote ni yenye kuiva. Ni hivyo pia juu ya Wakristo wenye kukomaa kiroho. Hawako sawasawa kabisa. Wanapatikana katika inchi mbalimbali na walilelewa kwa njia tofauti. Wako na miaka mbalimbali, na kila mutu iko na mambo yenye anapenda na yenye hapendi. Lakini, kuna sifa fulani zenye kuonyesha kwamba Wakristo hao wote wamekomaa kiroho. Ni sifa gani?

‘Kuna mabadiliko fulani yenye ninapaswa kufanya ili nimuige Yesu kwa uaminifu?’

5 Mukristo mwenye kukomaa kiroho anamuiga Yesu na anafuata “hatua zake kwa ukaribu [kwa uaminifu].” (1 Petro 2:21) Yesu alisema kwamba ni jambo la maana sana mutu amupende Yehova kwa moyo wake wote, kwa nafsi yake yote, na kwa akili yake yote, na kumupenda jirani yake kama yeye mwenyewe. (Mathayo 22:37-39) Mukristo mwenye kukomaa kiroho anajikaza kutii amri hiyo. Katika maisha yake, anaonyesha kwamba urafiki wake na Yehova na kuwapenda sana wengine ndiyo mambo ya lazima sana.

Wakristo wenye kuzeeka wanaweza kuiga unyenyekevu wa Yesu kwa kutegemeza vijana wenye kuongoza

(Ona fungu la 6)

6, 7. (a) Ni sifa zingine gani zenye kuonyesha kwamba Mukristo amekomaa kiroho? (b) Tunapaswa kujiuliza maulizo gani?

6 Upendo ni sifa moja kati ya sifa nyingi zenye Mukristo mwenye kukomaa kiroho anapaswa kuonyesha. (Wagalatia 5:22, 23) Anaonyesha pia sifa ya upole, kujizuia, na uvumilivu. Sifa hizo zinaweza kumusaidia apambane na magumu na hatakasirika, na kuvumilia hali zenye kuvunja moyo bila kupoteza tumaini. Wakati anafanya funzo lake la pekee, Mukristo mwenye kukomaa kiroho anaendelea kutafuta kanuni za Biblia zenye zitamusaidia kujua mema na mabaya. Kisha, wakati anatumia zamiri yake yenye kuzoezwa na Biblia, atakuwa na uwezo wa kuchukua maamuzi mazuri. Mukristo mwenye kukomaa kiroho ni munyenyekevu; kwa hiyo, anaamini kwamba sikuzote muongozo na kanuni za Yehova ni nzuri kabisa kuliko zake. * (Ona maelezo ya chini.) Anahubiri habari njema kwa bidii na anafanya yake yote ili kusaidia kutaniko liendelee kuwa na umoja.

7 Hata kama tumemutumikia Yehova kwa miaka mingi, kila mumoja wetu anaweza kujiuliza hivi: ‘Kuna mabadiliko fulani yenye ninapaswa kufanya ili nimuige Yesu kwa uaminifu? Kuna mambo yenye ninapaswa kufanya muzuri zaidi?’

“CHAKULA KIGUMU NI CHA WATU WAKOMAVU”

8. Ni nini inaonyesha kwamba Yesu alijua na kuelewa muzuri Maandiko?

8 Yesu alijua Maandiko na kuielewa muzuri. Wakati alikuwa na miaka 12, alitumia Maandiko ili kuzungumuza na walimu kwenye hekalu. Biblia inasema kwamba ‘wale wote waliokuwa wakimusikiliza walikuwa wakishangazwa daima na uelewaji wake na majibu yake.’ (Luka 2:46, 47) Kisha, wakati alikuwa anahubiri, alitumia Neno la Mungu kwa ufundi ili kunyamazisha maadui wake.—Mathayo 22:41-46.

9. (a) Mukristo mwenye kukomaa kiroho anapaswa kuwa na programu gani? (b) Sababu gani tunajifunza Biblia?

9 Mukristo mwenye anapenda kukomaa kiroho anaiga mufano wa Yesu na anafanya yake yote ili kuelewa Biblia vizuri zaidi. Anachunguza Maandiko kwa ukawaida ili kuelewa mafundisho mazito, kwa sababu anajua kwamba “chakula kigumu ni cha watu wakomavu [wenye kukomaa].” (Waebrania 5:14) Mukristo mwenye kukomaa kiroho anapenda kupata “ujuzi sahihi” wa Biblia. (Waefeso 4:13) Kwa hiyo, ujiulize hivi: ‘Ninasoma Biblia kila siku? Niko na programu ya funzo la pekee? Ninafanya ibada ya familia kila juma?’ Wakati unajifunza Biblia, utafute kanuni zenye zinaweza kukusaidia ujue mawazo ya Yehova na namna anajisikia. Kisha utumie kanuni hizo wakati unachukua maamuzi. Kufanya hivyo kutakusaidia umukaribie Yehova zaidi.

10. Mukristo mwenye kukomaa kiroho anaona namna gani sheria na kanuni za Mungu?

10 Mukristo mwenye kukomaa kiroho anapaswa kufanya mengi zaidi kuliko kujua tu mambo yenye Biblia inafundisha. Anapaswa kupenda sheria na kanuni za Mungu. Kisha anaonyesha upendo huo wakati anakuwa tayari kufanya mapenzi ya Yehova kuliko kufanya mapenzi yake. Anabadilisha hata namna yake ya kuishi, mawazo, na matendo yake. Kwa mufano, anamuiga Yesu na kujikaza kuvaa utu mupya, wenye ‘uliumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.’ (Soma Waefeso 4:22-24.) Ni lazima kukumbuka kwamba Mungu alitumia roho yake takatifu ili kuongoza watu wenye waliandika Biblia. Kwa hiyo, wakati Mukristo anajifunza Biblia, roho takatifu ya Mungu inamusaidia akomalishe ujuzi, upendo, na urafiki wake pamoja na Yehova.

USAIDIE KUENDELEZA UMOJA

11. Yesu aliona hali gani wakati alikuwa duniani?

11 Yesu alikuwa mutu mukamilifu. Hata hivyo, wakati alikuwa duniani, aliishi pamoja na watu wenye hawakamilike. Wazazi wake na ndugu na dada zake wote hawakuwa wakamilifu. Hata marafiki wa sana wa Yesu walionyesha tabia kama vile kiburi na kujipenda wenyewe. Kwa mufano, usiku moja mbele ya kifo chake, wanafunzi wake walibishana ili kujua ‘ni nani kati yao alionekana kuwa mukubwa zaidi ya wote.’ (Luka 22:24) Hata kama walikuwa na mawazo hayo yenye haikamilike, Yesu alijua kwamba wafuasi wake wangekuwa Wakristo wenye kukomaa kiroho na wangeanzisha kutaniko lenye kuwa na umoja. Usiku huohuo, Yesu alisali kwa ajili yao ili wakuwe na umoja. Alimuomba Baba yake wa mbinguni awasaidie wanafunzi wake wote wakuwe na umoja. Alisema hivi: ‘Kama vile ambavyo wewe, Baba, uko katika muungano pamoja na mimi na mimi niko katika muungano pamoja na wewe.’ Yesu aliongeza hivi: “Ili wapate kuwa kitu kimoja kama vile sisi tulivyo kitu kimoja.”—Yohana 17:21, 22.

12, 13. (a) Sisi Wakristo tunapaswa kuwa na kusudi gani? (b) Namna gani ndugu moja alijifunza kuendeleza umoja?

12 Mukristo mwenye kukomaa kiroho anaendeleza umoja katika kutaniko. (Soma Waefeso 4:1-6, 15, 16.) Kwa sababu sisi ni Wakristo, kusudi letu ni “kuunganishwa pamoja,” ni kusema, kutumika katika umoja. Ili tukuwe na umoja huo, kila Mukristo anapaswa kuwa munyenyekevu. Kwa hiyo, wakati makosa ya wengine inamukwaza, Mukristo mwenye kukomaa kiroho anafanya nguvu yake yote ili umoja wa kutaniko uendelee. Kwa hiyo, unaweza kujiuliza hivi: ‘Ninatenda namna gani wakati ndugu ao dada ananikosea? Ninajisikia namna gani wakati mutu fulani ananikosea? Ninaacha kuzungumuza naye? Ao ninajikaza kufanya amani pamoja naye?’ Mukristo mwenye kukomaa kiroho anajikaza kumaliza kutoelewena na wengine kuliko kuchochea jambo hilo.

13 Fikiria mufano wa ndugu Uwe. Zamani, alikuwa anakwazika haraka kwa sababu ya makosa ya ndugu na dada. Kisha, akaamua kutumia Biblia na kitabu Étude Perspicace des Écritures ili kujifunza maisha ya Daudi. Sababu gani aliamua kujifunza maisha ya Daudi? Kwa sababu watumishi fulani wa Mungu walimutendea Daudi vibaya. Kwa mufano, Mufalme Sauli alijaribu kumuua, watu fulani walitaka kumupiga kwa majiwe, na hata bibi yake alimuchekelea. (1 Samweli 19:9-11; 30:1-6; 2 Samweli 6:14-22) Lakini, hata kama watu walimutendea namna gani, Daudi alimupenda Yehova na kumutumainia. Daudi alionyesha pia rehema. Ndugu Uwe anasema kwamba alipaswa kumuiga Daudi. Kujifunza Biblia kulimusaidia atambue kwamba alipaswa kubadilisha mawazo yake juu ya namna ya anaona makosa ya ndugu na dada zake. Alipaswa kuacha kukumbuka makosa yao na alipaswa kuendeleza umoja katika kutaniko. Wewe pia unaweza kufanya hivyo?

UCHAGUE MARAFIKI KATI YA WALE WENYE KUFANYA MAPENZI YA MUNGU

14. Ni watu gani wenye Yesu alichagua kuwa marafiki wake?

14 Watu wote walijisikia huru kumukaribia Yesu. Wanaume na wanawake, vijana na wazee, na hata watoto, walifurahi kuwa pamoja naye. Lakini alichagua marafiki wake wa sana kwa uangalifu. Aliambia mitume wake hivi: ‘Ninyi ni rafiki zangu ikiwa munafanya ninalowaamuru ninyi.’ (Yohana 15:14) Yesu alichagua marafiki wake wa sana kati ya wafuasi wake waaminifu na wenye walimupenda Yehova na kumutumikia. Unachagua marafiki wenye kumupenda Yehova kwa moyo wao wote? Sababu gani ni lazima kufanya hivyo?

Unachagua marafiki wenye kumupenda Yehova kwa moyo wao wote?

15. Vijana wanaweza kupata faida gani kwa kufanya urafiki na Wakristo wenye kukomaa kiroho?

15 Matunda mengi inaiva muzuri wakati iko nafasi kwenye kuwa joto la jua. Vilevile, kupendwa na ndugu na dada zetu kunaweza kukusaidia ukuwe Mukristo mwenye kukomaa kiroho. Je, wewe ni kijana mwenye kufikiria namna utatumia maisha yako? Ikiwa ni hivyo, ni vizuri uchague marafiki wenye wamemutumikia Yehova kwa miaka mingi, na wenye wanaendeleza umoja katika kutaniko. Pengine wamepata magumu katika maisha yao, na wamevumilia majaribu katika utumishi wao kwa Yehova. Wanaweza kukusaidia uamue namna ya kutumia maisha yako muzuri zaidi. Kupitisha wakati pamoja nao kunaweza kukusaidia uchukue maamuzi mazuri na ukuwe Mukristo mwenye kukomaa kiroho.—Soma Waebrania 5:14.

16. Namna gani Wakristo wenye kukomaa kiroho walisaidia dada moja kijana?

16 Dada Helga anakumbuka kwamba wakati alikaribia kumaliza masomo, wengi kati ya wanafunzi wenzake walikuwa wanazungumuzia mambo yenye watafanya wakati unaokuja. Walipenda kusoma masomo ya juu ili wapate kazi nzuri sana. Hata hivyo, dada Helga alizungumuza na marafiki wake wenye kukomaa kiroho wa kutaniko lake. Anasema hivi: “Wengi kati yao walikuwa wakubwa kuliko mimi, na walinisaidia sana. Walinitia moyo nianze utumishi wa wakati wote. Kisha, nilifanya kazi ya upainia kwa muda wa miaka tano. Sasa, kumepita miaka mingi, lakini niko mwenye furaha kwa sababu nilitumia sehemu kubwa ya ujana wangu katika kazi ya Yehova. Sina huzuni hata kidogo kwa sababu niliamua kufanya hivyo.”

17, 18. Ni nini inaweza kutusaidia kumutumikia Yehova muzuri zaidi?

17 Ikiwa tunamuiga Yesu, tutakuwa Wakristo wenye kukomaa kiroho. Tutamukaribia Yehova zaidi, na tutakuwa tayari kabisa kumutumikia. Wakati Mukristo anakomaa kiroho, anamutumikia Yehova muzuri zaidi. Yesu alitia moyo wafuasi wake hivi: ‘Muache nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili wapate kuona matendo yenu mazuri na kumupa utukufu Baba yenu aliye mbinguni.’—Mathayo 5:16.

18 Tumeona namna Mukristo mwenye kukomaa kiroho anaweza kutegemeza kabisa kutaniko. Mukristo anaonyesha pia kwamba amekomaa kiroho kupitia namna anatumia zamiri yake. Namna gani zamiri yetu inaweza kutusaidia kuchukua maamuzi mazuri? Na namna gani tunaweza kuheshimu zamiri ya wengine? Tutajibu maulizo hayo katika habari yenye kufuata.

^ fu. 6 Kwa mufano, ndugu wenye kuzeeka na wenye uzoefu wanaweza kuombwa kuacha migawo fulani na kusaidia ndugu vijana wenye kupewa migawo hiyo.