Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Mungu Ana Watu Wanaomtumikia kwa Utaratibu?

Je, Mungu Ana Watu Wanaomtumikia kwa Utaratibu?

Je, Mungu Ana Watu Wanaomtumikia kwa Utaratibu?

KUNA utaratibu, au mpangilio, katika uumbaji wote wa Mungu. Kwa mfano, chembe ndogo ya chachu ina mpangilio wa kustaajabisha. Idadi ya sehemu za chembe hiyo ni karibu sawa na idadi ya sehemu zinazofanyiza ndege kubwa aina ya Boeing 777. Hata hivyo, sehemu hizo zote zimepangwa vizuri, kila moja mahali pake, katika chembe hiyo ya mviringo yenye ukubwa wa mikroni tano. * Tofauti na ndege, chembe za chachu zinaweza kuzaana. Utaratibu katika chembe hizo unastaajabisha kama nini!—1 Wakorintho 14:33.

Utaratibu haupatikani katika vitu vinavyoweza kuonekana kwa macho tu. Biblia inaonyesha kuwa viumbe katika makao ya roho wana utaratibu wa hali ya juu sana, unaopatana na kusudi la Muumba. Nabii Danieli aliona katika maono malaika wengi sana kwenye ua wa Mungu mbinguni: “Kulikuwa na maelfu elfu walioendelea kumtumikia, na elfu kumi mara elfu kumi walioendelea kusimama mbele zake.” (Danieli 7:9, 10) Fikiria utaratibu unaopaswa kuwapo ili idadi hiyo kubwa ya malaika—zaidi ya milioni mia moja—wasikilize na kufanya yale ambayo Mungu anawaagiza wawafanyie watumishi wake duniani!—Zaburi 91:11.

Ingawa Muumba, Yehova Mungu, ndiye anayeweka utaratibu uliopo katika viumbe wake wote, yeye si kama mtawala asiye na hisia zozote. Badala yake, yeye ni Mungu mwenye upendo na furaha, anayewatakia hali njema viumbe wake wote. (1 Timotheo 1:11; 1 Petro 5:7) Jambo hilo linaonekana wazi katika njia ambayo alishughulika na taifa la kale la Israeli na Wakristo wa karne ya kwanza.

Israeli la Kale—Taifa Lenye Utaratibu Mzuri

Yehova Mungu alimtumia Musa kuhakikisha kwamba Waisraeli wanafanya ibada ya kweli kwa utaratibu mzuri. Fikiria mipango ya kupiga kambi walipokuwa katika nyika ya Sinai. Bila shaka, kungekuwa na mvurugo kama kila familia ingeruhusiwa kupiga kambi popote ilipochagua. Yehova aliwapa Waisraeli maagizo hususa kuhusiana na mahali ambapo kila kabila lingepaswa kupiga kambi. (Hesabu 2:1-34) Sheria ya Musa pia ilikuwa na maagizo hususa kuhusu afya na usafi—kwa mfano, kuhusu kuondoa kinyesi cha binadamu.—Kumbukumbu la Torati 23:12, 13.

Waisraeli walipoingia katika Nchi ya Ahadi, walikuwa taifa lenye utaratibu mzuri katika njia nyingi. Taifa hilo liligawanywa katika makabila 12 na kila kabila likagawiwa sehemu yake ya ardhi. Sheria ambayo Yehova alitoa kwa taifa hilo kupitia Musa ilihusu kila sehemu ya maisha ya Waisraeli—ibada, ndoa, familia, elimu, biashara, chakula, kilimo, ufugaji, na kadhalika. * Ingawa sheria nyingine zilieleza mambo waziwazi na kwa undani, zote zilikuwa wonyesho wa jinsi Yehova alivyowajali watu wake. Pia, zilichangia furaha miongoni mwao. Kwa kufuata mipango hiyo yenye upendo, Waisraeli walifurahia uhusiano wa pekee pamoja na Mungu.—Zaburi 147:19, 20.

Ingawa ni kweli kwamba Musa alikuwa kiongozi stadi, kufaulu au kutofaulu kwake kulitegemea ushikamanifu wake kwa utaratibu na mwongozo ambao Mungu alitaka ufuatwe, bali si ustadi wake akiwa kiongozi. Kwa mfano, Musa aliamuaje njia ambayo Waisraeli wangefuata nyikani? Yehova aliwaongoza kwa kutumia nguzo ya wingu mchana, na nguzo ya moto usiku. (Kutoka 13:21, 22) Ingawa Mungu aliwatumia wanadamu, yeye mwenyewe ndiye aliyewapanga na kuwaongoza watu wake. Alifanya vivyo hivyo katika karne ya kwanza.

Wakristo wa Karne ya Kwanza Walikuwa Wenye Utaratibu Mzuri

Mitume na wanafunzi wa Yesu walihubiri kwa bidii, hivyo makutaniko mengi ya Kikristo yakaanzishwa katika sehemu nyingi za Asia na Ulaya katika karne ya kwanza. Ingawa makutaniko hayo yalikuwa yametawanyika, hayakufanya mambo bila mwongozo, wala kwa njia yao wenyewe. Badala yake, yalikuwa na utaratibu mzuri na yalinufaika kutokana na usimamizi wenye upendo wa mitume. Kwa mfano, mtume Paulo alimpa Tito mgawo wa kwenda Krete “ili kupanga mambo yote huko.” (Tito 1:5, The Jerusalem Bible) Paulo pia aliliandikia kutaniko la Korintho kwamba ndugu fulani walikuwa na “uwezo wa kupanga mambo.” (1 Wakorintho 12:28, The New Testament in Modern Speech) Lakini ni nani aliyesaidia kutaniko hilo kuwa na utaratibu huo? Paulo alisema kwamba Mungu ‘ameliweka,’ kutaniko “katika mpango.”—1 Wakorintho 12:24, Biblia Habari Njema.

Waangalizi katika kutaniko la Kikristo hawakuwa mabwana wakubwa juu ya waamini wenzao. Badala yake walikuwa “wafanyakazi wenzi” waliofuata mwongozo wa roho ya Mungu, na walitazamiwa kuwa “vielelezo kwa kundi.” (2 Wakorintho 1:24; 1 Petro 5:2, 3) Yesu Kristo aliyefufuliwa ndiye “kichwa cha kutaniko,” bali si mwanadamu wala kikundi fulani cha watu wasio wakamilifu.—Waefeso 5:23.

Wakati kutaniko la Korintho lilipoanza kufanya mambo tofauti kabisa na makutaniko mengine, Paulo aliwaandikia hivi: “Kwani! Je, neno la Mungu lilitoka kwenu, au je, liliwafikia ninyi tu?” (1 Wakorintho 14:36) Paulo alitumia swali hilo lisilohitaji jibu ili kurekebisha maoni yao na kuwasaidia waelewe kwamba hawakupaswa kufanya mambo kwa kufuata njia zao wenyewe. Makutaniko yaliongezeka na kusitawi yalipofuata mwongozo wa mitume.—Matendo 16:4, 5.

Wonyesho wa Upendo wa Mungu

Namna gani leo? Watu fulani wanaweza kusita kujiunga na shirika fulani la kidini. Hata hivyo, Biblia inathibitisha kwamba wakati wote Mungu ametumia watu wake wenye utaratibu na umoja ili kutimiza kusudi lake. Alihakikisha kwamba waabudu wake katika Israeli la kale, na vilevile Wakristo wa karne ya kwanza, wanamwabudu kwa utaratibu.

Kwa hiyo, ni jambo linalopatana na akili kusema kwamba Yehova Mungu bado anawaongoza watu wake kama alivyofanya zamani. Ndiyo, Yehova anaonyesha kuwa anawapenda na kuwajali waabudu wake kwa kuhakikisha kwamba wana utaratibu na umoja. Leo, Yehova anatumia watumishi wake wenye utaratibu na umoja kutimiza kusudi lake kwa wanadamu. Mtu anaweza kuwatambua jinsi gani? Fikiria mambo yanayofuata:

Wakristo wa kweli wamepangwa kwa utaratibu ili kutimiza kazi fulani. (Mathayo 24:14; 1 Timotheo 2:3, 4) Yesu aliwaamuru wafuasi wake wahubiri habari njema za Ufalme kwa mataifa yote, kazi ambayo haingewezekana bila kuwa na watu kutoka katika mataifa yote ambao wanaifanya kwa utaratibu na kwa umoja. Kwa mfano, unaweza kumlisha mtu mmoja peke yako, lakini kama ingekupasa kulisha maelfu ya watu, hata mamilioni, ungehitaji kikundi cha watu chenye utaratibu mzuri na kinachofanya kazi kwa ushirikiano. Ili kutimiza kazi yao, Wakristo wa kweli wanatumikia “bega kwa bega,” au “kwa moyo mmoja.” (Sefania 3:9; BHN) Je, ingewezekana kufanya kazi inayohusisha mataifa, lugha, na jamii mbalimbali bila kuwa na watu wenye utaratibu na umoja? Jibu ni wazi.

Wakristo wa kweli wana mpangilio mzuri wa kutegemezana na kutiana moyo. Mtu anayepanda mlima akiwa peke yake anaweza kuamua ni upande gani wa mlima anaotaka kupanda, na si lazima ajishughulishe na wapandaji wengine wasio na uzoefu. Hata hivyo, akipatwa na aksidenti au tatizo lingine, atakuwa katika hatari kubwa, kwa sababu hakutakuwa na yeyote wa kumsaidia. Kwa hiyo, si jambo la hekima hata kidogo kujitenga na wengine. (Methali 18:1) Ili Wakristo watimize amri ya Yesu, ni lazima wasaidiane na kutegemezana. (Mathayo 28:19, 20) Kutaniko la Kikristo linaandaa maagizo, mafundisho, na mashauri yenye kutia moyo kutoka katika Biblia—mambo ambayo yanahitajiwa sana ili wote waendelee kumtumikia Mungu bila kuacha. Ni wapi ambapo mtu angepata mafundisho kuhusu njia za Yehova kama hakungekuwa na mikutano ya Kikristo yenye utaratibu na umoja kwa ajili ya mafundisho na ibada?—Waebrania 10:24, 25.

Wakristo wa kweli wamepangwa kwa utaratibu ili kumtumikia Mungu kwa umoja. Kondoo wa Yesu wanaposikiliza sauti yake, wanakuwa “kundi moja” chini ya uongozi wake. (Yohana 10:16) Hawajatawanyika katika makanisa na vikundi tofauti-tofauti; wala hakuna mgawanyiko kati yao kuhusu mafundisho. Badala yake, wote ‘husema kwa upatano.’ (1 Wakorintho 1:10) Ili kukaa pamoja kwa umoja, tunahitaji utaratibu, nao utaratibu unahitaji mpangilio. Mungu anawabariki tu wale wanaomwabudu kwa umoja.—Zaburi 133:1, 3.

Kumpenda Mungu kikweli na kupenda kweli ya Biblia kumewavuta wengi kwenye kikundi cha watu ambao pia wanampenda Mungu na Neno lake Biblia. Wakiwa kikundi cha watu wenye utaratibu na umoja, Mashahidi wa Yehova duniani kote wanajitahidi kufanya mapenzi ya Mungu. Wana uhakika katika ahadi hii ya Mungu: “Mimi nitakaa katikati yao na kutembea katikati yao, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.” (2 Wakorintho 6:16) Unaweza kufurahia baraka hizo ukimwabudu Yehova Mungu ukiwa pamoja na watu wake wenye utaratibu na umoja.

[Maelezo ya Chini]

^ Mikroni, au mikromita, milioni moja ni sawa na mita moja.

^ Ona Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 214-220 au Étude perspicace des Écritures, Buku la 2, ukurasa wa 154-160, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Kambi ya Waisraeli ilipangwa kwa utaratibu mzuri

[Picha katika ukurasa wa 14, 15]

Utaratibu unahitajiwa ili kuhubiri katika mataifa yote

Kuhubiri nyumba kwa nyumba

Kutoa misaada wakati wa msiba

Makusanyiko

Ujenzi wa majengo ya ibada