Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Dunia Itakwisha Mwaka wa 2012?

Je, Dunia Itakwisha Mwaka wa 2012?

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Je, Dunia Itakwisha Mwaka wa 2012?

▪ “Watu wanaoamini kwamba dunia itakwisha hivi karibuni wamekuwa wakimiminika katika kijiji fulani nchini Ufaransa. . . . Wanaamini kwamba dunia itakwisha tarehe 21 Desemba 2012, ambayo itakuwa mwisho wa mzunguko wa miaka 5,125 katika kalenda ya kale ya Wamaya.”—Shirika la Habari la BBC.

Dunia itaendelea kuwepo kwa muda mrefu sana, ingawa viongozi wa kidini, watu wanaodai kuwa wanasayansi, na wabashiri wengi wa karne ya 21 wamebashiri kwamba dunia itapatwa na msiba mkubwa. Ndiyo, dunia haitakwisha mwaka wa 2012. Kwa hakika, Dunia itaendelea kuwepo mwaka huo na pia kwa miaka mingi itakayofuata.

Biblia inatuambia hivi: “Kizazi chapita na kingine chaja, lakini dunia yadumu daima.” (Mhubiri 1:4, Biblia Habari Njema) Pia, fikiria maana ya maneno yaliyoandikwa kwenye Isaya 45:18: ‘Yehova, Mfanyizaji wa dunia na Mtengenezaji wake, Yeye aliyeifanya imara, ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu, amesema hivi: “Mimi ni Yehova, wala hakuna mwingine.”’

Je, baba mwenye upendo anaweza kutumia saa nyingi kubuni na kumtengenezea mvulana wake kigari cha kuchezea au kumtengenezea binti yake mtoto bandia wa kuchezea, kisha muda mfupi baadaye aharibu vitu hivyo ambavyo vilikusudiwa kuwafurahisha? Huo ungekuwa ukatili! Vivyo hivyo, Mungu aliumba dunia ili hasa ifurahiwe na viumbe wake wa kibinadamu. Mungu aliwaambia hivi wenzi wa kwanza wa ndoa, Adamu na Hawa: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha.” Baadaye, “Mungu akaona kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa chema sana.” (Mwanzo 1:27, 28, 31) Mungu hajasahau kusudi lake kuelekea dunia; hataruhusu dunia iharibiwe. Yehova alikazia hivi kuhusu mambo yote aliyoahidi: ‘Hayatarudi kwangu bila matokeo, bali hakika yatatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika yatafanikiwa katika yale ambayo nimeyatuma.’—Isaya 55:11.

Hata hivyo, ni mapenzi ya Yehova “kuwaharibu wale wanaoiharibu dunia.” (Ufunuo 11:18) Anatoa ahadi hii katika Neno lake: “Wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake. Nao waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila, watang’olewa kutoka ndani yake.”—Methali 2:21, 22.

Hilo litatukia wakati gani? Hakuna mwanadamu anayejua. Yesu alisema: “Kuhusu siku ile au saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika mbinguni wala Mwana, ila Baba.” (Marko 13:32) Mashahidi wa Yehova hawajaribu kutabiri wakati ambapo Mungu atawaharibu waovu. Hata ingawa wako macho ili kuona “ishara” ya ule mwisho na wanaamini kwamba wanadamu wanaishi katika kipindi ambacho Biblia inakiita “siku za mwisho,” hawawezi kujua hasa “ule mwisho” utakuja wakati gani. (Marko 13:4-8, 33; 2 Timotheo 3:1) Hilo wanamwachia Baba yao wa mbinguni na Mwana wake.

Kwa sasa, Mashahidi wa Yehova wanajishughulisha na kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Ufalme huo ni serikali ya kimbingu ambayo itatawala na kubadili Dunia kuwa paradiso yenye amani, ambayo ‘waadilifu wenyewe wataimiliki, na kukaa milele juu yake.’—Zaburi 37:29.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 10]

Image Science and Analysis Laboratory, NASA-Johnson Space Center