Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Ni Nani Anayeweza Kufasiri Unabii?

Ni Nani Anayeweza Kufasiri Unabii?

Ni Nani Anayeweza Kufasiri Unabii?

Inasemekana kwamba fundo la Gordius lilikuwa fumbo gumu zaidi kufumbua katika siku za Aleksanda Mkuu. Watu waliamini kwamba yeyote ambaye angefungua fundo hilo angekuwa mwenye hekima na angepata ushindi mkubwa. * Hekaya moja inasema kwamba Aleksanda alifumbua fumbo hilo kwa kukata lile fundo mara moja kwa upanga.

KWA muda mrefu, watu wenye hekima walijitahidi kufungua mafundo tata na pia kufafanua vitendawili, kufasiri unabii, na hata kutabiri wakati ujao.

Lakini, mara nyingi walishindwa kufanya hivyo. Kwa mfano, watu wenye hekima wa Babiloni walishindwa kufasiri mwandiko uliotokea kimuujiza kwenye ukuta wa jumba la Mfalme Belshaza wakati wa karamu yenye kelele nyingi. Nabii Danieli aliyekuwa mzee ndiye tu aliyeweza kufasiri ujumbe huo wa kinabii. Nabii huyo wa Yehova Mungu alijulikana kwa “kufungua mafundo.” (Danieli 5:12) Unabii huo uliotabiri kuharibiwa kwa Milki ya Babiloni, ulitimia usiku huohuo!—Danieli 5:1, 4-8, 25-30.

Unabii Ni Nini?

Unabii umefafanuliwa kuwa ufunuo wa matukio ya wakati ujao, hata kabla hayajatokea. Unabii wa kweli ni ujumbe ulioongozwa na roho ya Mungu, ambao umeandikwa au kusemwa, yaani, ufunuo kuhusu mapenzi na kusudi la Mungu. Katika Biblia kuna unabii mbalimbali kuhusu kutokea na kutambuliwa kwa Masihi, “umalizio wa mfumo wa mambo,” na pia ujumbe mbalimbali wa hukumu kutoka kwa Mungu.—Mathayo 24:3; Danieli 9:25.

Leo, watu wanaosemekana kuwa na hekima, yaani, wataalamu wa sayansi, uchumi, afya, siasa, mazingira, na taaluma nyinginezo, hujaribu kutabiri wakati ujao. Ingawa matabiri yao yanatangazwa sana kwenye vyombo vya habari na yanapendwa na watu wengi, matabiri hayo ni makisio tu yanayotegemea ujuzi au maoni fulani ya kibinafsi. Isitoshe, kwa kila utabiri unaotolewa, kunakuwa na matabiri mengine chungu nzima yenye kuupinga. Kwa kweli, ni jambo hatari kutabiri wakati ujao.

Chanzo cha Unabii wa Kweli

Hivyo, basi, ni nani aliye chanzo cha unabii wa kweli, na ni nani anayeweza kufasiri unabii huo? Mtume Petro aliandika: “Hakuna unabii wa Andiko unaotokana na fasiri yoyote ya kibinafsi.” (2 Petro 1:20) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “fasiri,” au “tafsiri,” linamaanisha “kusuluhisha au kufunua,” likionyesha kwamba “kinachofunguliwa kilikuwa kimefungwa.” Hivyo, Biblia fulani inatafsiri hivi maneno ya Petro: “Hakuna unabii wala Andiko linaloweza kufunguliwa na . . . mtu binafsi.”

Fikiria baharia akifunga kwa ustadi fundo tata kwa kutumia kamba. Anapomaliza kufunga, mtu wa kawaida anaweza kuona jinsi nyuzi za kamba zinavyojipinda na kuingia ndani ya fundo hilo, lakini asijue jinsi ya kulifungua. Vivyo hivyo, leo watu wanaweza kuona mambo fulani ambayo yatatokeza hali ngumu baadaye, lakini wasijue kwa hakika jinsi hali itakavyokuwa wakati huo.

Manabii wa kale walioongozwa na roho ya Mungu, kama vile Danieli, hawakuchunguza hali zilivyokuwa siku zao, kisha wakajaribu kufafanua wakati ujao usioeleweka kwa kutoa unabii. Kama wangejaribu kufanya hivyo, wangekuwa wakitoa unabii kulingana na mawazo yao. Kwa hiyo, huo ungekuwa utabiri wa kibinadamu, ubashiri usio na msingi kamili. Badala yake, Petro aliongezea kusema: “Unabii haukuletwa wakati wowote kwa mapenzi ya mwanadamu, bali wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.”—2 Petro 1:21.

‘Tafsiri Ni za Mungu’

Miaka 3,700 hivi iliyopita, wanaume wawili walifungwa gerezani huko Misri. Kila mmoja wao aliota ndoto yenye kutatanisha. Kwa kuwa hawangeweza kuzungumza na watu wenye hekima kuhusu ndoto zao, walimweleza Yosefu, mfungwa mwenzao wakisema: “Tumeota ndoto, wala hatuna mtafsiri.” Mtumishi huyo wa Mungu, aliwatia moyo wamweleze ndoto zao, akiwaambia: “Je, tafsiri si za Mungu?” (Mwanzo 40:8) Ni Yehova Mungu pekee anayeweza kufafanua unabii, kama vile baharia mwenye uzoefu anavyoweza kufungua mafundo tata. Hiyo ni kwa sababu Mungu ndiye chanzo cha unabii huo. Tunafaa kumtegemea aufafanue. Ndiyo, Yosefu hakukosea aliposema kuwa Mungu ndiye anayeweza kutoa ufafanuzi.

Basi, ‘tafsiri ni za Mungu’ katika maana gani? Jambo hilo limethibitika katika njia mbalimbali. Unabii fulani wa Biblia umeandikwa pamoja na utimizo wake. Hivyo, ni rahisi kuuelewa, kama vile ilivyo rahisi kufungua mafundo fulani ambayo baharia anaeleza waziwazi jinsi ya kuyafungua.—Mwanzo 18:14; 21:2.

Unabii mwingine unaweza kufafanuliwa kwa kuchunguza muktadha. Nabii Danieli aliona katika maono ya kinabii ‘kondoo-dume mwenye pembe mbili’ ambaye alipigwa na kuangushwa na “mbuzi-dume” ambaye alikuwa na “pembe yenye kuonekana wazi kati ya macho yake.” Muktadha unaonyesha kwamba kondoo huyo mwenye pembe mbili aliwakilisha “wafalme wa Umedi na Uajemi,” naye mbuzi, “mfalme wa Ugiriki.” (Danieli 8:3-8, 20-22) Miaka zaidi ya 200 baadaye, “ile pembe kubwa,” yaani, Aleksanda Mkuu, alianza kushambulia Uajemi. Mwanahistoria Myahudi Yosefo alidai kwamba Aleksanda alionyeshwa unabii huo alipokuwa akifanya mashambulizi yake karibu na Yerusalemu, naye akaamini kwamba ulimrejelea yeye.

‘Tafsiri ni za Mungu’ katika maana nyingine. Yosefu, mtumishi mwaminifu wa Yehova Mungu, aliongozwa na roho takatifu kuelewa maana ya zile ndoto tata ambazo wafungwa wenzake walimweleza. (Mwanzo 41:38) Leo, watumishi wa Mungu wasipokuwa na uhakika kuhusu maana ya unabii fulani, wao husali ili kupata roho ya Mungu, kisha hujifunza na kuchunguza kwa bidii Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake. Kwa mwongozo wa Mungu wanaweza kupata maandiko ambayo yanawasaidia kuelewa maana ya unabii fulani. Jambo hilo halitokei kimuujiza kupitia mwanadamu yeyote. Linatoka kwa Mungu kwa sababu unabii unaeleweka kupitia roho yake na Neno lake. Kwa hiyo, ufafanuzi wa unabii unategemea Biblia bali si watabiri wa kibinadamu.—Matendo 15:12-21.

Pia, ‘tafsiri ni za Mungu’ kwa sababu yeye ndiye huamua na kutoa mwongozo kuhusu wakati ambapo unabii fulani unapaswa kueleweka na watumishi wake waaminifu duniani. Unabii unaweza kueleweka kabla ya kutimia, wakati wa kutimia, au baada ya kutimia. Kwa kuwa Mungu ndiye chanzo cha unabii, anaufunua wakati wake unaofaa.

Katika simulizi kuhusu Yosefu na wafungwa wenzake wawili, alieleza maana ya ndoto siku tatu kabla ya ndoto hizo kutimia. (Mwanzo 40:13, 19) Baadaye, Yosefu alipoletwa mbele ya Farao mwenye nguvu ili aeleze maana ya ndoto za Farao huyo, kipindi cha miaka saba ya mavuno mengi kilikuwa karibu kuanza. Kwa msaada wa roho ya Mungu, Yosefu alieleza maana ya ndoto za Farao ili mipango ifanywe kuhifadhi mavuno ambayo yangekuwa mengi.—Mwanzo 41:29, 39, 40.

Unabii mwingine unaeleweka kikamili na watumishi wa Mungu baada kutimia. Matukio mengi kuhusu maisha ya Yesu yalikuwa yametabiriwa karne nyingi kabla hajazaliwa, lakini mitume wake walielewa utimizo wa unabii huo baada ya Yesu kufufuliwa. (Zaburi 22:18; 34:20; Yohana 19:24, 36) Pia, kulingana na Danieli 12:4, unabii fulani ‘ulifungwa kwa muhuri’ “mpaka wakati wa mwisho” ambapo Danieli alisema, “ujuzi wa kweli utakuwa mwingi.” Tunaishi wakati ambapo unabii huo unaendelea kutimia. *

Jinsi Unabii wa Biblia Unavyokuhusu

Yosefu na Danieli walisimama mbele ya wafalme wa siku zao na kutoa unabii uliohusu mataifa na falme mbalimbali. Wakristo wa karne ya kwanza walisimama mbele ya watu wa siku zao wakiwa wasemaji wa Yehova, Mungu wa unabii, na kuwanufaisha sana wale waliosikiliza ujumbe wao.

Leo, Mashahidi wa Yehova duniani kote wanatangaza ujumbe wa unabii—habari njema za Ufalme wa Mungu—na kuwaeleza watu kwamba unabii wa Yesu kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo” unaendelea kutimia. (Mathayo 24:3, 14) Je, unajua unabii huo na jinsi unavyokuhusu? Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia uelewe na kunufaika na unabii ambao bila shaka ni muhimu sana.

[Maelezo ya Chini]

^ Hekaya za Wagiriki zinasema kwamba huko Gordium, mji mkuu wa Frigia, gari la kukokotwa la mwanzilishi wa mji huo aliyeitwa Gordius, lilikuwa limefungwa kwa fundo tata sana kwenye nguzo fulani, na yeyote ambaye angelifungua angeshinda Asia wakati ujao.

^ Ona mfululizo wa makala za kwanza wenye kichwa “Mambo 6 Yaliyotabiriwa Katika Biblia Yanayotimia Sasa,” katika toleo la Mei 1, 2011, la gazeti hili.

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Yosefu na Danieli walimtukuza Mungu walipotoa ufafanuzi wa unabii