Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

KICHWA

Mambo Yenye Mungu Amekufanyia

Mambo Yenye Mungu Amekufanyia

‘Kwa maana Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamutoa Mwana wake muzaliwa​-pekee, ili kila mutu anayemuamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.’​—Yohana 3:16.

Hilo ni andiko ambalo linajulikana sana kati ya maandiko mengine ya Biblia na linalotajwa na watu wengi. Inasemekana kwamba hakuna andiko lingine ambalo “linazungumuzia kwa kifupi sana uhusiano kati ya Mungu na wanadamu na njia ya wanadamu ya kuokolewa.” Hiyo ndiyo sababu katika inchi nyingi, andiko hilo la “Yohana 3:16” linatumiwa mara nyingi wakati wa matukio makubwa, linaandikwa kwenye vibandiko vya motokari, kwenye michoro ya ukuta, na nafasi zingine.

Inawezekana wale wanaotumia andiko hilo wanaamini kwamba upendo wa Mungu unawahakikishia kuwa watapata wokovu wa milele. Wewe una mawazo gani? Upendo wa Mungu una maana gani kwako? Na unawaza Mungu amefanya nini inayoonyesha kuwa anakupenda?

“MUNGU ALIUPENDA ULIMWENGU SANA”

Watu wengi wanakubali kwamba Mungu ndiye aliumba ulimwengu muzima, vitu vyenye kuonekana, na wanadamu. Viumbe vilivyo na uzima vimeumbwa kwa njia ya ajabu na isiyoeleweka hivi kwamba kunapaswa kuwa mutu mukubwa mwenye akili aliyefanya viumbe hivyo. Watu wengi wanamushukuru Mungu kila siku kwa sababu ya zawadi ya uzima. Wanatambua pia kwamba wanamutegemea Mungu ili wapate mambo yote ya maana yanayoendeleza uzima wao, kama vile hewa, maji, chakula, na mizunguko ya asili ya dunia. Vitu hivyo vyote vinawasaidia waendelee kuishi na kufurahia mambo wanayofanya.

Tunapaswa kumushukuru Mungu kwa vitu vyote hivyo kwa sababu kwa kweli ni yeye ndiye Muumbaji wetu na Mutegemezaji wetu. (Zaburi 104:10-28; 145:15, 16; Matendo 4:24) Tunamushukuru Mungu kwa sababu ya upendo ambao anatuonyesha tunapofikiria mambo anayoendelea kufanya ili kuendeleza uzima wetu. Mutume Paulo alisema hivi: ‘[Mungu] mwenyewe anawapa watu wote uhai na pumuzi na vitu vyote. Kwa maana kupitia kwake tuna uhai na tunaenda na kuwako.’​—Matendo 17:25, 28.

Zaidi ya kutuhangaikia kimwili, Mungu anatuonyesha upendo wake katika njia nyingi. Tofauti na wanyama, Mungu ametupatia uwezo wa kumujua na kumuabudu na pia anatusaidia kutosheleza uwezo huo. (Mathayo 5:3) Kupitia njia hiyo, wanadamu watiifu wana tumaini la kuwa sehemu ya familia ya Mungu, ni kusema, “watoto” wake.​—Waroma 8:19-21.

Kama vile andiko la Yohana 3:16 linavyosema, Mungu alituonyesha upendo wake kwa kumutuma mwana wake, Yesu, katika dunia ili atufundishe juu ya Mungu na Baba yake na ili akufe kwa ajili yetu. Hata hivyo, watu wengi hawajue sababu gani ilikuwa lazima Yesu akufe kwa ajili ya wanadamu na namna gani kifo chake kinaonyesha kwamba Mungu anatupenda. Tuone basi namna Biblia inavyofasiria sababu gani Yesu alikufa na faida ya kifo chake.

‘ALIMUTOA MWANA WAKE MUZALIWA​-PEKEE’

Wanadamu wote wanapatwa na magonjwa, wanazeeka, na wanakufa. Lakini mwanzoni Yehova Mungu hakukusudia mambo yawe hivyo. Aliwapatia wanadamu wa kwanza tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani. Lakini walipaswa kufanya tu jambo moja: Walipaswa kumutii. Mungu alisema kwamba ikiwa wangeamua kutomutii, wangekufa. (Mwanzo 2:17) Hata hivyo, mwanadamu wa kwanza aliamua kutomutii Mungu, na hivyo akajiletea kifo yeye pamoja na wazao wake. Mutume Paulo alisema hivi: ‘Kupitia mutu mumoja zambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia zambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya zambi.’​—Waroma 5:12.

Lakini, Mungu ni ‘mupenda​-haki.’ (Zaburi 37:28) Hata ikiwa Mungu hangeweza kusamehe tendo hilo la mwanadamu wa kwanza la kukosa kutii kimakusudi, Mungu hakuwahukumu wanadamu wote kuteseka na kufa milele kwa sababu ya kutotii kwa mwanadamu mumoja. Tofauti na hilo, kwa kutumia kanuni ya haki ya “nafsi kwa nafsi,” amesawazisha vipimo vyake vya haki, na akafanya iwezekane kwa wanadamu watiifu kupata tena uzima wa milele. (Kutoka 21:23) Ulizo ni hili, Ingewezekana namna gani uzima mukamilifu wa kibinadamu ambao Adamu alipoteza upatikane tena? Jibu ni: Mutu fulani alipaswa kutoa, ao kuzabihu, uzima unaolingana na ule wa Adamu, ni kusema, uzima mukamilifu wa kibinadamu.

Yesu alikuja duniani bila kulazimishwa na akatoa uzima wake ili kukomboa wanadamu kutoka katika zambi na kifo

Ni wazi kwamba, hakuna muzao yeyote wa Adamu ambaye angeweza kulipia uzima huo, lakini Yesu yeye angeweza. (Zaburi 49:6-9) Kwa sababu Yesu alizaliwa bila kuriti zambi, alikuwa mukamilifu kama Adamu. Kwa kutoa uzima wake, Yesu aliwakomboa wanadamu kutoka katika utumwa wa zambi. Kwa kufanya hivyo, aliwatolea wazao wa Adamu na Eva tumaini la kufurahia uzima huohuo mukamilifu ambao Adamu na Eva walipoteza. (Waroma 3:23, 24; 6:23) Tunapaswa kufanya nini ili tufaidike na tendo hilo la upendo?

‘KILA MUTU ANAYEMUAMINI’

Tunaposoma tena andiko hilo la Yohana 3:16, tunaona maneno haya: ‘Kila mutu anayemuamini [Yesu] asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.’ Hilo linamaanisha kwamba ili tupate uzima wa milele, tunapaswa kufanya jambo fulani. Ikiwa tunataka kupata “uzima wa milele,” tunapaswa kumuamini Yesu na kumutii.

Unaweza kujiuliza hivi: ‘Sababu gani tumutii? Je, Yesu hakusema kwamba ‘kila mutu anayemuamini’ atapata uzima wa milele?’ Ndiyo, kuamini ni jambo la maana. Hata hivyo, ni jambo la maana kukumbuka kwamba katika Biblia, kuwa na imani kunatia ndani mambo mengi. Kulingana na kitabu kimoja, neno linalotumiwa na Yohana katika luga ya zamani linamaanisha “kumutegemea, si kumutolea tu sifa.” (Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words) Ili kukubaliwa na Mungu, mutu anapaswa kufanya mengi zaidi kuliko kukubali tu kwamba Yesu ni Mwokozi. Mutu anayeamini anapaswa pia kujikaza kufanya mambo ambayo Yesu alifundisha. Ikiwa hakuna matendo, aina yote ya imani ni bure. Biblia inasema hivi: “Imani bila matendo imekufa.” (Yakobo 2:26) Kwa maneno mengine, kila mutu anayemuamini Yesu anapaswa kuonyesha imani yake kwa matendo, ni kusema, kuishi kulingana na mambo anayoamini.

Paulo anafasiria maneno hayo hivi: ‘Upendo alio nao Kristo unatulazimisha, kwa sababu hili ndilo tumehukumu, kwamba mutu mumoja [Yesu] alikufa kwa ajili ya wote . . . naye alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yao na kufufuliwa.’ (2 Wakorintho 5:14, 15) Shukrani yetu ya kutoka moyoni kwa ajili ya zabihu ya Yesu inapaswa kutuchochea tufanye mabadiliko katika maisha yetu, ni kusema, hatutaishi tena kwa ajili yetu sisi wenyewe, lakini tutaishi kwa ajili ya yule aliyetoa uzima wake kwa ajili yetu, yaani, Yesu. Hilo linamaanisha kwamba, kufanya mambo ambayo Yesu alifundisha ndilo linapaswa kuwa jambo la kwanza katika maisha yetu. Mabadiliko hayo yanapaswa kuonekana katika kanuni zinazotuongoza, mambo tunayochagua, na kila jambo tunalofanya. Wale wanaomuamini na kumutii Yesu watapata nini?

‘ASIANGAMIZWE BALI AWE NA UZIMA WA MILELE’

Sehemu ya mwisho ya andiko la Yohana 3:16 inazungumuzia ahadi ya Mungu kwa wale wanaoamini zabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo na ambao wanaishi kulingana na kanuni za Mungu. Mungu anakusudia watu hao waaminifu ‘wasiangamizwe bali wawe na uzima wa milele.’ Hata hivyo, matumaini mbili tofauti yanawangojea wale wanaofaidika na upendo wa Mungu.

Yesu aliahidi kwamba kikundi kimoja kitapata uzima wa milele mbinguni. Aliwaambia waziwazi wanafunzi wake waaminifu kwamba ataenda kuwatayarishia nafasi ili waweze kutawala pamoja naye katika utukufu. (Yohana 14:2, 3; Wafilipi 3:20, 21) Wale watakaofufuliwa ili kuishi mbinguni “watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala wakiwa wafalme pamoja naye ile miaka elfu.”​—Ufunuo 20:6.

Ni hesabu ndogo tu ya wafuasi wa Kristo ndio watakaopata pendeleo hilo la kuishi mbinguni. Kwa kweli, Yesu alisema hivi: ‘Musiogope, kundi dogo, kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa ninyi ufalme.’ (Luka 12:32) Hesabu hiyo ya “kundi dogo” itakuwa ya watu ngapi? Andiko la Ufunuo 14:1, 4 linasema hivi: ‘Nami nikaona, na, tazama! Mwana​-Kondoo [Yesu Kristo aliyefufuliwa] amesimama juu ya Mulima Sayuni [mbinguni], na pamoja naye 144 000 wakiwa na jina lake na jina la Baba yake limeandikwa juu ya mapaji ya nyuso zao. . . . Hao walinunuliwa kutoka kati ya wanadamu wakiwa matunda ya kwanza kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo.’ Tukilinganisha hesabu hiyo na mamiliare ya watu ambao wameishi duniani, watu 144 000 ni “kundi dogo” kabisa. Kwa sababu inasemekana kwamba watakuwa wafalme, watatawala juu ya nani?

Yesu alizungumuza pia juu ya kikundi cha pili cha watu waaminifu ambao watafaidika na baraka za Ufalme wa mbinguni. Kama inavyoonyeshwa katika andiko la Yohana 10:16, Yesu alisema hivi: ‘Nami nina kondoo wengine, ambao si wa zizi hili; hao pia nitawaleta, nao wataisikiliza sauti yangu, nao watakuwa kundi moja, muchungaji mumoja.’ “Kondoo” hao wana tumaini la kupata uzima wa milele duniani, tumaini lilelile ambalo Adamu na Eva walikuwa nalo mwanzoni. Tunajua namna gani kwamba watu hao wataishi milele duniani wakati unaokuja?

Mara nyingi, Biblia inazungumuza juu ya hali nzuri zitakazokuwa katika Paradiso inayokuja duniani. Ikiwa unapenda kujua hilo, unaweza kufungua Biblia yako na kusoma maandiko haya: Zaburi 37:9-11; 46:8, 9; 72:7, 8, 16; Isaya 35:5, 6; 65:21-23; Mathayo 5:5; Yohana 5:28, 29; Ufunuo 21:4. Maandiko hayo yanatabiri mwisho wa vita, njaa, magonjwa, na kifo. Yanazungumuza juu ya wakati watu wazuri watafurahia kujenga nyumba zao, kulima mashamba yao, na kulea watoto wao katika hali zenye amani. * Je, tumaini hilo halikufurahishe? Tuna sababu nzuri ya kuamini kwamba ahadi hizo zote zitatimizwa hivi karibuni.

MUNGU AMETUFANYIA MAMBO MENGI

Unapofikiria mambo ambayo Mungu amekufanyia na ambayo amefanyia wanadamu wote, ni wazi kwamba ametufanyia mambo mengi sana. Tuna uzima, akili, afya ya muzuri kwa kadiri fulani, na vitu vya lazima ili kutegemeza uzima wetu. Zaidi ya hayo, zawadi ya Mungu ya zabihu ya ukombozi kupitia Yesu, aliyekufa kwa ajili yetu, inaweza kutuletea baraka nyingi sana, kama tunavyosoma katika andiko la Yohana 3:16.

Kuishi milele katika hali zenye amani bila kuogopa magonjwa, vita, njaa, ao kifo, utakuwa mwanzo wa furaha na baraka ambazo hazitakuwa na mwisho. Ni wewe mwenyewe unapaswa kuamua ikiwa unapenda kupata baraka hizo. Kwa kweli, ulizo linalobakia ni, Wewe unafanya nini ili umupendeze Mungu?

^ Ili kupata habari zingine kuhusu unabii huo mbalimbali, soma sura ya 3 ya kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.