Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

 KICHWA | SHETANI ANAKUWAKA KABISA?

Shetani Ni Mufano Tu wa Mambo Mabaya?

Shetani Ni Mufano Tu wa Mambo Mabaya?

Ni vyepesi sana kusema kama Shetani tunayesoma juu yake katika Biblia ni mufano tu wa mambo yote mabaya. Lakini ni vile kabisa Biblia inafundisha? Ikiwa ni vile, sababu gani Biblia inasema kuwa Shetani alizungumuza na Yesu Kristo na Mungu Mweza-Yote mwenyewe? Ona mifano mbili ya mazungumuzo kama hayo.

WAKATI SHETANI ALIZUNGUMUZA NA YESU

Wakati Yesu alianza utumishi wake, Ibilisi alipima kumushawishi kupitia njia tatu. Kwanza, Shetani alijaribu kumushawishi Yesu atumie uwezo Mungu alimupatia kwa njia ya kutafuta faida zake mwenyewe ili kumaliza njaa yake. Kisha, Shetani alipima kumujaribu Yesu atie maisha yake katika hatari kwa njia ya kipumbavu na ajifikirie sana yeye mwenyewe. Na mwisho, Shetani alimuambia Yesu kuwa atamupatia mamlaka juu ya falme zote za dunia ikiwa tu atamufanyia tendo ndogo la ibada. Yesu alipinga vishawishi hivyo vitatu vya ujanja kwa kutaja Maandiko kila wakati.—Mathayo 4:1-11; Luka 4:1-13.

Yesu alikuwa anazungumuza na nani? Alikuwa anazungumuza na mufano fulani wa ubaya uliokuwa ndani yake? Kulingana na Maandiko, Yesu ‘alijaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini bila kuwa na zambi.’ (Waebrania 4:15) Tena Biblia inasema hivi: ‘Yeye hakufanya zambi, wala udanganyifu haukupatikana kinywani mwake.’ (1 Petro 2:22) Yesu alibakia mukamilifu, aliendelea kuonyesha uaminifu. Hakuacha ubaya wowote ukomae ndani yake. Ni wazi kuwa Yesu hakuwa anazungumuza na sehemu yoyote mbaya iliyokuwa ndani yake; alikuwa anazungumuza na mutu wa kwelikweli.

Mazungumuzo hayohayo yanafunua mambo mengine yenye kuonyesha kwamba Shetani anakuwaka kabisa.

  • Kumbuka kuwa Ibilisi alimuonyesha Yesu falme zote za dunia na kumuambia atamupatia falme hizo ikiwa anamufanyia tendo fulani la ibada. (Mathayo 4:8, 9) Ikiwa Shetani hakukuwa mutu wa kwelikweli, hangemutolea Yesu falme hizo. Tena, Yesu hakukataa kuwa Shetani ana mamlaka hayo kubwa.

  • Kisha Yesu kupinga vishawishi hivyo, Ibilisi ‘alimuacha mupaka wakati mwengine unaofaa.’ (Luka 4:13) Katika hali hii, je, Shetani anaonekana kuwa mufano tu wa mambo mabaya ao adui asiyechoka?

  • Ona kuwa ‘malaika walikuja na kuanza kumuhudumia’ Yesu. (Mathayo 4:11) Malaika hao walikuwa watu wa roho wa kwelikweli, waliomutolea Yesu vitia-moyo na musaada aliokuwa nao lazima? Bila shaka. Basi, tuko na sababu ya kusema kama Shetani ni mufano wa mambo mabaya wala haiko kiumbe wa roho?

 WAKATI SHETANI ALIZUNGUMUZA NA MUNGU

Mufano wetu wa pili ni juu ya habari ya Ayubu, mwanaume aliyemuogopa Mungu. Habari hiyo inasema juu ya mazungumuzo mawili kati ya Ibilisi na Mungu. Katika mazungumuzo yote hayo mawili, Mungu alimusifu Ayubu kwa sababu ya uaminifu wake. Shetani alisema kama Ayubu alimutumikia Mungu kwa sababu tu ya faida zake mwenyewe, akisingizia kuwa Mungu aliuza uaminifu wa Ayubu. Kwa kweli, Ibilisi alisema kama alimujua Ayubu vizuri kupita namna Mungu alimujua. Yehova alimuruhusu Shetani achukue vitu vyote Ayubu alikuwa navyo, watoto wake, na hata afya yake. * Kisha wakati kupita, ilionekana wazi kuwa Yehova alisema kweli juu ya Ayubu, na Shetani alionekana kuwa muongo. Mungu alimubariki Ayubu kwa sababu ya uaminifu wake.—Ayubu 1:6-12; 2:1-7.

Katika mazungumuzo hayo kati ya Yehova Mungu na Shetani, je, Yehova alikuwa anazungumuza na ubaya fulani uliokuwa ndani yake mwenyewe? Biblia inasema hivi: “Mungu wa kweli, njia yake ni kamilifu.” (2 Samweli 22:31) Neno la Mungu linasema tena hivi: ‘Mutakatifu, mutakatifu, mutakatifu ni Yehova Mungu, Mweza-Yote.’ (Ufunuo 4:8) Mutu mutakatifu ni mutu aliye safi, mwenye kutakata, na mwenye kutenganishwa na zambi. Yehova ni mukamilifu na hana ubaya wowote. Hawezi kuwa hata na ubaya wowote.

Mazungumuzo ya Shetani pamoja na Mungu yalimuletea Ayubu matokeo mabaya

Hata hivyo, watu fulani wanaweza kusema kama hata Ayubu hakukuwa mutu wa kwelikweli, kwa hiyo mazungumuzo hayo yote yalikuwa ya mufano. Lakini, wazo hilo linapatana na akili? Maandiko mengine ya Biblia yanaonyesha kuwa Ayubu alikuwa mutu wa kwelikweli. Kwa mufano, katika andiko la Yakobo 5:7-11, Ayubu anatumiwa kuwa mufano wa kuchochea Wakristo wavumilie nyakati ngumu na pia kuwa kikumbusho cha kuwafariji kuwa Yehova anabariki uvumilivu kama huo. Mufano huo unaweza kuwa na nguvu gani ikiwa Ayubu hakuwa mutu wa kwelikweli na ikiwa mashambulizi hayo ya Shetani yalikuwa tu ya kuwazia? Tena, andiko la Ezekieli 14:14, 20 linataja watu watatu wenye haki, ni kusema, Noa, Danieli, na pia Ayubu. Kama Noa na Danieli, Ayubu alikuwa mutu wa kwelikweli, mwanaume mwenye imani kubwa. Ikiwa Ayubu alikuwa mutu wa kwelikweli, mushambulizi wake, yule aliyemuletea mateso, anapaswa kuwa pia mutu wa kwelikweli.

Kwa kweli, Biblia inaonyesha kuwa Shetani ni kiumbe wa roho wa kwelikweli. Lakini, unaweza kujiuliza, ‘Leo Shetani iko hatari kwangu na kwa familia yangu katika dunia hii?’

SHETANI IKO HATARI WAKATI WETU?

Wazia hali hii: kikundi cha watu wabaya kinaingia gafula katika muji wenu. Ni wazi kuwa kila mutu atakosa usalama na tabia za watu katika muji zitaharibika. Sasa fikiria hali yenye kufanana na hiyo: Shetani na mashetani wake, viumbe wa roho wa kwelikweli, waliomuasi Mungu kama Shetani, wanatupwa kwa gafula kwenye dunia. Hilo lingeleta matokeo gani? Fikiria mambo unaona na kusikia kwenye vyombo vya kutangaza habari mahali unaishi na katika dunia yote.

  • Hauone kama matendo mabaya na ya jeuri yanaongezeka, ijapokuwa bidii inafanywa katika dunia yote ili kuyazuia?

  • Hauone kama mambo ya kujifurahisha yanayoonyesha kuzungumuza na mashetani yanaongezeka, ijapokuwa wazazi wengi hawapendezwe na mambo hayo?

  • Hauone kama mazingira yanaendelea kuharibika sana, hata ikiwa watu wanajikaza wakiwa na nia nzuri ya kuyalinda?

  • Inaonekana kama jambo fulani haliendeke kabisa kati ya watu, kwamba nguvu fulani inawachochea kuelekea musiba, sivyo?

Biblia inaonyesha ni nani analeta matatizo hayo. Inasema hivi: ‘Yule joka mukubwa akatupwa chini, yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa; akatupwa chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye. . . . Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.’ (Ufunuo 12:9, 12) Kisha kuchunguza uhakikisho mbalimbali, watu wengi wamesema kuwa Shetani ni mutu wa roho aliye hatari, yule anayechochea kwa bidii dunia inayotuzunguka.

Unaweza kujiuliza namna ya kupata ulinzi na hilo ni hangaiko nzuri. Habari inayofuata itakutolea musaada unaofaa.

^ fu. 12 Yehova ni jina la Mungu kama inavyoonyeshwa katika Biblia.